Habari za Punde

Serikali Yapongeza Mchango wa Taasisi za Kidini katika Kuletea Maendeleo Taifa

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu, Mhe George Simbachawene akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa 51 wa Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya Tanzania Jijini Dar es Salaam.

Na.Mwandishi Wetu.

Serikali inatambua mchango wa Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya katika maendeleo ya Sekta ya Elimu kupitia taasisi zake za elimu; Sekta ya Afya kupitia hospitali na namna mnavyo jitolea kuchangia damu salama katika benki yetu ya damu; pamoja na Sekta ya maji kupitia mpango wenu wa kuchimba visima vya maji maeneo mbalimbali Nchini.

Hayo yamesemwa na waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene wakati wa uzinduzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa 51 wa Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya Tanzania Jijini Dar es Salaam leo 30/09/2022 kwa niaba ya Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyekuwa Mgeni Rasmi.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu anawapongeza Sheikh Tahir Mahmood Chaudhry – Amir na Mubashir Mkuu, pamoja  na Wasaidizi wako wa Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya kwa uongozi mahiri unaolenga kudumisha Amani na Utulivu hapa nchini. kupitia kauli mbiu yenu ya, Upendo kwa wote bila chuki kwa yeyote”

Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi na rafiki kwa ustawi wa Taasisi hizo ili ziendelee kuwa sehemu ya kuliletea maendeleo Taifa letu, alisema Waziri.

Nyote mnatambua kuwa Nchi yetu kupitia ibara ya 3(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, 1977 haiegemei upande wowote katika masuala ya dini - Secular State. Hata hivyo, sehemu kubwa ya watu wake wanaamini katika Mungu kupitia dini zenye madhehebu mbalimbali, alisema Waziri.

“Kwa msingi huu, nchi yetu kupitia ibara ya 19 ya Katiba, inatambua uhuru wa kuabudu kwa mtu mmoja mmoja au kundi la watu katika madhehebu na dini zao ili mradi tu wafuate masharti ya Katiba na Sheria za Nchi.”  

Aidha nichukue fursa hii adhimu kuwasihi katika siku zote tatu mtakazo kuwa hapa, muendelee kuliombea taifa letu amani, utulivu, upendo na mshikamano ili kwa pamoja tuendelee kulijenga taifa bora licha ya changamoto mbalimbali tunazo kumbana nazo.

Kwa namna ya pekee nawaomba muiombee Nchi yetu dhidi ya majanga mbalimbali likiwemo janga la njaa linaloweza kusababishwa na ukame, ukosefu wa mvua za kutosha au mafuriko, changamoto za kiuchumi zinazo sababishwa ama na sisi wenyewe au mataifa mengine, magonjwa, dhiki na mmomonyoko wa maadili.

Naye Naibu Amir Shekhe Abdurahman Mohamed amesema Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya  inashika mafundisho ya Kiislamu kwa usahihi wake.

 Shida inakuwepo pale waumini wanapofundishwa dini na wakaiacha, na kuwaikilisha dini kwa sura ambayo sio yenyewe, hili ni jambo ambalo  Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya inaliepuka.

“Maisha ya binadamu ni roho na mwili; lazima apate mafunzo ya kupata maendeleo ya kimwili na wakati huo huo apate maendeleo ya kiroho, chochote ukikiacha kingine kinapoteza maana yake,” alisema Shekhe Abdurahman.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu, Mhe George Simbachawene akisalimiana na viongozi mbalimbali wa Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu, Mhe George Simbachawene akitembelea maonesho moja ya banda la  maonesho ya vitabu vya Jumuiya ya Waislam Waahmadiyya Tanzania.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Sera Bunge na Uratibu, Mhe George Simbachawene akipokea zawadi ya vitabu kutoka kwa Sheikh Tahir Mahmood Chaudhry – Amir na Mubashir Mkuu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.