Habari za Punde

Wasanii Waunga Mkono Juhudi za Serikali Dhidi ya Vitendo vya Ukatili

 

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima akizungumza na kufungua Kikao hicho na kuwapongeza Wasanii hao kwa hatua hiyo na kusema vita ya ukatili inahitaji ushirikiano wa Jamii yote siyo Serikali peke yake.
Wasanii mbalimbali wa Sanaa Tanzania wakimsikiliza Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dorothy Gwajima. 

Na. WMJJWM, Dar es salaam 
Wasanii wa filamu nchini wamejitokeza kuunga mkono juhudi za Serikali kwenye ya Mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili ndani ya jamii.

Hayo yamebainika katika kikao cha wadau wa Tamasha la Tanzania Development Festival linalotekeleza "Kampeni ya twende pamoja ukatili sasa basi"  kilichofanyika Oktoba 08, 2022 Jijini Dar es salaam.

Mmoja wa wasanii hao Bw. Hillary Daudi (Zembwela) akizungumza kwa niaba ya wenzake amesema Kada ya wasanii  wapo tayari kushirikiana na Serikali kuwa mabalozi wa kukemea vitendo vya ukatili na kuvitokomeza.

"Sisi dhamira yetu ni kuungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hii kupambana na suala hili la ukatili hadi liishe, tunachohitaji ni ushirikiano tu" amesema Hillary.

Ameongeza kuwa, matamasha watakayofanya ni ya kipekee tofauti na matamasha mengi kwani watakwenda kutoa elimu na uelewa kwa wananchi.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima akifungua kikao hicho amewapongeza wasanii hao kwa hatua hiyo na kusema vita ya ukatili inahitaji ushirikiano wa Jamii yote siyo Serikali peke yake.

Amewahakikishia wasanii hao ushirikiano wa Serikali na kuwataka kuunganisha nguvu na Makundi mengine yenye dhamira moja ili tatizo hilo liwe historia.

"Mnastahili kuenzi katika kipindi hiki kwakujitokeza kushirikiana na Serikali ni jambo kubwa, Ushirikiano mmepata, Ninyi ni askari mwamvuli wa Wizara hii, kundi hilo linakuwa la pili baada ya SMAUJATA, mtengeneze Muungano, Sisi kama Serikali ni fursa, Ninyi ni wazalendo"

Awali, akieleza lengo la Tamasha hilo linalokwemda na kaulimbiu ya "Twende pamoja, Tanzania ukatili sasa basi, Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu kutoka 
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Timotheo Mgonja alisema kuwa, lengo la Tamasha hilo ni kuwashirikisha Wadau wote ili kwa pamoja watokomeze ukatili.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Wadau mbalimbali ikiwemo Wizara, Taasisi na baadhi ya wasanii wa filamu pamoja na Wadau mbalimbali wanaoshughulika na Masuala ya Kijamii.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.