Habari za Punde

Watendaji kutoka Taasisi mbali mbali za SMZ kutoa maoni yao yatakayosaidia kuimarisha mpango kazi wa Kitaifa wa wanawake amani na usalama

Na. Maulid Yussuf -- Zanzibar

Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Bi.Abeida Rashid Abdalla amewataka watendaji kutoka Taasisi mbali mbali za Serikali kutoa maoni yao yatakayosaidia kuimarisha mpango kazi wa Kitaifa wa  wanawake amani na usalama.

Akifungua mkutano wa wadau wa kupokea maoni ya uboreshaji wa rasimu ya mpango kazi huo uliofanyika katika ukumbi wa Zanzibar Beach resort Mazizini nje kidogo ya Mji wa Zanzibar bi Abeida amewataka washiriki  hao kuangalia  kila Taasisi na Idara kuwa kuna kitu gani ambacho wanaweza kuingiza kwenye mpango kazi  kwa lengo kuwezesha utekelezaji wake.

Aidha amewataka kuangalia masuala ya faraja na ahuweni,  kwa kuwa ni eneo ambalo halijashughulikiwa katika kiwango cha kutosha katika rasimu ya mpango kazi.

Pia amesema bado kuna nafasi ya kutoa maoni katika njia ya maandishi na kupeleka sehemu husika na kuwataka wadau hao kufanya vikao kama hivyo  kwa upande wa Pemba kwani itaisaidia  kuongeza  ushiriki, umililiki na uwelewa.

Nae Mwakilishi Mkaazi wa UN Women Tanzania  Ms Hodan Addou, amesema Tanzania ni nchi ya Amani na haina vita ila imezungukwa na nchi ambazo zina vita,  hivyo kuwepo kwa mpango kazi huo kutaongeza na kuchangia juhudi za Serikali za kuhakikisha usawa wa kijinsia na ushiriki wa wanawake katika masuala ya uongozi, ulinzi na usalama  katika vyombo vya maamuzi.

Ms Hoddan amepongeza juhudi za Serikali zote mbili chini ya uongozi wa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar Dkt  Hussein Ali Mwinyi za kuwezesha usawa wa kijinsia na ushiriki wa wanawake katika ngazi mbalimbali hasa za uongozi.

Mpango kazi huu ni utekelezaji wa maamuzi namba 1325 ya Baraza kuu la usalama la Umoja wa Mataifa  ambalo limetaka nchi wanachama kuwa na mpango kazi wa aina hiyo ambapo Tanzania imeridhia maamuzi hayo.

mwisho

IMEANDALIWA NA KITENGO CHA UHUSIANO WIZARA YA MAENDELEO YA JAMII JINSIA WAZEE NA WATOTO. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.