Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amewasili Mkoani Tanga kwa Ziara ya siku Sita ya kichama pamoja na kukagua miradi mbali mbali ya maendeleo.
Alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Tanga Mhe. Hemed amepokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe Omar Tebweta Mguma, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa tanga Ndugu Rajab Abdallah pamoja na Viongozi mbali mbali wa Chama na Serikali.
Mara baada ya mapokezi hayo Mhe. Hemed alifika Ofisi za Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Tanga kupokea taarifa za maendeleo ya chama mkoani hapo kupitia maelekezo yaliyomo katika ilani ya chama cha mapinduzi 20202 -2 2025 na utekelezaji wa shughuli za serikali katika Mkoa wa Tanga ambapo amewataka Viongozi hao kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan hasa katika kudumisha Umoja, Amani na utulivu iliyopo .
Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutenga fedha nyingi na kuzielekeza katika miradi mbali mbali ya maendeleo katika Mkoa huo hatua ambayo inawapa faraja wananchi wa Tanga katika kuwaletea huduma mbali mbali za kijamii ikiwemo Afya, Elimu, miundombinu, ujasiriamali na sekta nyenginezo.
Pia Mhe. Hemed amewataka viongozi hao kuungana na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Dkt. Hussein Ali Mwinyi katika kupinga matendo maovu ikiwemo matumizi ya madawa ya kulevya na udhalilishaji na kueleza kuwa Taifa linapoteza nguvu kazi ya vijana kwa kujihusisha na mtendo hayo.
Pamoja na hayo Mhe. Hemed amewataka Viongozi wa Mkoa huo kushirikiana kuhakikisha Mapato yanakusanywa kwa mujibu wa Sheria bila ya kumuonea Mwananchi yoyote ili kupata fedha zitakazotumika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo.
Aidha Mhe. Hemed ambae pia ni mlezi wa Mkoa wa Tanga kichama amewataka wanachama wa Chama Cha Mapinduzi kuvunja makundi na badala yake waungane katika kukipigania Chama kuwaletea maendeleo watanzania.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Tanga Ndg. Rajab Abdallah pamoja na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Tanga Suleiman Mzee Suleiman (Charas) wamemshukuru Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kuendelea kumsaidia Mwenyekiti wa Chama Cha Mapindzui Taifa katika kuwaleteae maendeleo watanzania.
Aidha wameeleza kuwa hali ya kisiasa Mkoani Tanga ni ya kuridhisha ambapo Uongozi wa Serikali ya mkoa inashirikiana na Uongozi wa CCM Mkoa wa Tanga katika kutekeleza ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020 – 2025 ili kuhakisha watanzania wanapata Maendeleo chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia suluhu Hassan .
No comments:
Post a Comment