SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar
imezitaka taasisi za umma kubadili mifumo ya zamani ya utendaji na utoaji huduma kwa wananchi kwa kuanzisha mifumo ya kisasa ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha utendaji wao kuenda na kasi ya matumizi ya
teknolojia.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali
Mwinyi aliyasema hayo kwenye maadhimisho ya siku ya Sheria, Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja.
Alisema wakati huu wa sayansi na teknolojia mifumo ya uendeshaji taasisi kwa kutumia karatasi na kalamu imepitwa na
wakati, hivyo alizitaka taasisi za umma zikiwemo taasisi za sheria na wadau
wake kubadili mifumo ya utendaji wao ili kuendana na kasi ya teknolojia.
Alisema matumizi ya TEHAMA
hurahisisha utendaji na kuondosha usumbufu pia kusaidia jitihada za
Serikali za kukuza uchumi wa nchi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa kuokoa
fedha nyingi zinazogharamia shughuli zinazotekelezwa kwa mifumo ya zamani na
badala yake gharama ya fedha hizo zitaelekezwa kwenye shughuli nyengine za
maendeleo.
Akizungumzia haki mtandao Mahakamani, Rais Dk. Mwinyi alisema ni muhimu kwa
ujenzi wa taasisi bora za kisheria kwani mfumo unaendana na mabadiliko ya
sayansi na teknolojia yanayotokea duniani.
Hata hivyo, aliipongeza Mahakama Kuu ya Zanzibar kwa mara ya kwanza kuanzisha
mfumo wa kielektroniki wa kusajili mawakili ambao alieleza kwa sasa watafungua mashauri
na kufuatilia uendeshaji wa mashauri hayo wakiwa nyumbani, vijijini au Ofisini.
Alisema mfumo huo
wa kisasa utasaidia kuokoa muda unaotumika kwenye taasisi za sheria kufanyia
kazi nyengine za kuinua vipato vyao, kuimarisha uwazi, uwajibikaji, utawala
bora, ukusanyaji mzuri wa mapato na kuimarisha uchumi wa nchi pamoja na kusaidia
kukuza imani ya wananchi na wawekezaji wa ndani na nje kwenye vyombo vya
sheria.
Akizungumiza faida za matumizi ya TEHAMA kwenye taasisi za Sheria, Dk.
Mwinyi alisema usikilizaji wa haraka wa mashauri na kutolewa maamuzi,
upatikanaji wa takwimu sahihi, ufuatiliaji bora na usimamizi bora wa mashauri.
“Kwa kupitia haki mtandao, hakutakuwa na ulazima kwa Waheshimiwa Majaji
wa Mahkama Kuu kusafirishwa kwenda Pemba kusikiliza mashauri, kwani mashauri
hayo yatasikilizwa na kuamuliwa kwa mfumo wa Tehama tuu, Shahidi hatalazimika
kufika kwenye jengo la mahakama kutoa ushahidi, inaweza kuandaliwa mifumo ya
kutoa ushahidi wake kupitia hata simu yake tu ya mkononi, utaratibu huu
mienendo ya kesi itapatikana kwa haraka” alifafanua Dk. Mwinyi.
Rais, Dk. Mwinyi aliahidi kutoa kipaumbele kwa bajeti ya matumizi ya
Tehama kwa mahakama kuu Zanzibar ili kuimarisha miundombinu ya taasisi za
sheria nchini, na kusema kwamba Serikali itatumia zaidi ya bilioni nne kwa
ujenzi wa Majengo manne ya Mahakama kuu na za wilaya kwa Unguja na Pemba ambazo
zinaendana na mifumo ya Tehama. Aidha, aliitaka mahakama hiyo kupitia taasisi
zake kujipanga na kuwasilisha Serikalini mpangokazi na bajeti kwa ajili ya
utekelezaji wa adhma hiyo.
Pia alitoa wito kwa Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria,
Utumishi na Utawala Bora kupitia Ofisi ya Wakala wa Serikali Mtandao
kuzisimamia na kuzishauri ipasavyo taasisi zote za sheria katika kufikia lengo
hilo la haki mtandao nchini.
Hata hivyo, aliiataka Mahakama kushirikiana na wadau wengine wa haki kwa maboresho yoyote kwenye mhimili wa Mahkama alisema
yataleta matokeo chanya yenye ufanisi kwa ushirikiano imara na wadau.
Akizungumzia uanzishwaji wa Mahkama Maalum ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu
Uchumi, Rais Dk. Mwinyi alisifu jitihada zilizofikiwa na Mahakama Kuu ya
Zanzibar kwa hatua waliyofikia na kueleza kufarajika kwake kusikia tayari wameunda
kamati ya wataalamu kwaajili ya kusimamia na kuratibu mchakato wa kuanzishwa
Mahakama hiyo.
Alieleza Kuanzishwa kwa mahkama hiyo, kutaisaidia Serikali mapambano
dhidi ya vitendo vya ufisadi na matumizi mabaya ya Ofisi na rasilimali za umma ambayo
huzorotesha uchumi wa nchi na ustawi wa jamii hali aliyoieleza inarejesha nyuma
juhudi za Serikali za kuwaletea wananchi maendeleo.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma alisema
karne ya 21 inazitaka taasisi zote na watendaji wake kuwa na mabadiko ya fikra na
kimtazamo yanayoendana na teknolojia iliopo duniani, nakuongeza kuwa mabadiliko
ya teknolojia kwenye Mahakama Kuu ya Zanzibar yatasaidia utoaji wa haki na
kukuza uchumi wa Zanzibar kwa kuleta mageuzi makubwa ya mabadiliko ya utendaji
wao. Hivyo, aliwataka majaji kutumia jitihada za ziada ili kuendana na kasi ya
huduma mtandao kwa sasa.
Naye, Jaji Mkuu wa Zanzibar Khamis Ramadhan
Abdalla, alisema maadhimisho ya siku ya sheria ni kuanza mwaka mpya wa mahakama
na kueleza miongoni kwa mikakati ya mabadiliko yao kwenye ufanisi wa
utendajikazi wao ni kuwafikia wananchi kwa haraka, kuendelea kutoa huduma bora
kwa wananchi na kuwa karibu nao kwaajili ya kuwahudumia pamoja na kutoa
mahakama rafiki zenye huduma za haraka.
Madhamisho ya Sheria yaliambatana na wiki ya
sheria iliyoanza Febuari 06 mwaka huu kwa kutekelezwa shughuli mbalimbali za
kisheria ikiwemo kutoa elimu kwa umma juu ya masuala ya sheria, kutambua
mchango wa makaadhi kwa kutunukiwa vyeti vinara bora watoaji haki, kupokea
mawakili wapywa, kuzindua mfumo wa kuwasajili mawakili kwa njia ya mtandao pamoja
na kuhitimishwa kwa matembezi yaliyoandaliwa na taasisi ya “Zanzibar Maisha bora
Foundation” yaliyoongozwa na Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Mama Mariam Mwinyi
yakiwa na kauli mbiu “Kupinga vita dhidi ya Udhalilishaji wa kijinsia.”
Aidha, maadhimisho ya Sheria pia yalihudhuriwa na
ujumbe kutoka Mahakama kuu ya Tanzania ulioongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe.Prof. Ibrahim
Juma yalikua na kaulimbiu, “Haki mtandao ya kukuza uchumi na Ustawi wa jamii” ni
maadhimisho ya 12 tokea kuanzishwa kwake mwaka 2012.
IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment