Habari za Punde

Wafanyabiashara Watakiwa Kutosafirisha Bidhaa za Vyakula Vinavyoingia Nchini Kutoka Nje ya Nchi

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Masjid Shifaa (Msikiti Maiti) Muembetanga Wilaya ya Mjini Unguja leo 3-2-2023.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi amepiga marufuku kwa wafanyabiashara kusafirsha bidhaa za vyakula vyote vinavyoingia nchini kutolewa nje ya nchi.

Alhajj Mwinyi alitoa marufuku hiyo wakati akiwatubia wananchi na waumini wa Kiislam walipotekeleza ibada  ya sala ya Ijumaa huko Masjid Shifaa - Mwembetanga, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Aidha, aliwaagiza wafanyabiashara kutoa chakula chote kilichomo kwenye maghala badala ya kukifungia ili kuepusha uhaba wa chakula nchini na kukwepa kuongeza bei.

Alhajj Mwinyi, alisema kitendo walichokifanya wafanyabiashara hao cha kufungia chakula kwenye maghala kimeleta athari kubwa kwa wananchi wa visiwa vya Unguja na Pemba na kueleza kwamba Pemba kulikua na hali mbaya zaidi ya upungufu wa chakula hata hivyo, alieleza baada ya kufanya mazungumzo na wafanyabiashara mbalimbali wa bidhaa na vyakula hali ya sasa kwa Pemba imetengemaa.

“Nimewaambia wafanyabiashara Serikali si vyema ikafanya biashara lakini mkitufikisha sehemu lazima tufanye biashara nitawaambia Serikali na Shirika la biashara la ZSTC watoe fedha walete wao chakula wauze, kwasababu hatuwezi kuwavumilia wafanyabiashara kuongeza bei kwa makusudi kwa kupenda wao huku wanaumiza watu” Alionya Al hajj Mwinyi.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha chakula zinaendelea kushuka bei nchini.

Akizungumzia kuelekea mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan, Al hajj Mwinyi alitoa agizo kwa wafanyabiashara hao kuongeza chakula cha kutosha ili kuepuka uhaba wa chakula hasa kwenye bidhaa muhimu za unga, mchele, sukari na mafuta ya kupikia na kueleza kuwa hadi sasa  bandarini kuna meli zenye tani hadi 10 za chakula zikiendelea kushusha mizigo.

Rais Dk. Mwinyi alieleza, licha ya changanoto ya wafanyabiashara waliochangia kupanda kwa bei za vyakula ambapo alieleza tabia za baadhi ya wafanyabiashara kupandisha bei au kuhodhi mali kuonekane kuna uhaba wa bidhaa ili wapandishe bei pia alieleza tatizo jengine ni ufanisi mdogo wa bandari, meli kukaa sana bandarini kabla ya kushusha mizigo.

Al hajj Mwinyi aliongeza Serikali inampango madhubuti wa kuhakikisha bandari inaongezewa ufanisi wa hali ya juu ili kutoa fursa kwa mizigo hasa ya chakula kushushwa haraka ili vyakula viendelee kuwepo sokoni.

Akizungumzia masuala ya kuimarisha afya na kufanya mazoezi, Alhajj Mwinyi, alieleza Kutofanya mazoezi kunachangia magonjwa yasioambukiza yakiwemo presha, moyo na saratani hali aliyoieleza kurudisha nyuma maendeleo ya taifa.

“Imethibitika kwa utafiti kwamba moja ya sababu inayochangia magonjwa yasioambukiza ni kutofanya mazoezi, tujitahidi kufanya mazoezi ili tulinde afya zetu” Alishauri Al hajj Mwinyi.

Aliwataka wananchi kujenga tabia ya kufanya mazoezi kila siku pamoja na kuwaasa kupunguza kula vyakula vinavyochochea zaidi magonjwa hayo.

Alisema taifa lenye watu wasiokuwa na afya haliwezi kupata maendeleo, sababu hospitali zitajaa wagonjwa na uwezo wa serikali utapungua kwa kutibu watu badala ya watu hao kuzalisha kuiongezea kipato Serikali.

Alisema wananchi wamejijenga utamaduni wa kupanda gari kila sehemu wanazokwenda hali aliyoieleza kutotoa fursa kwao ya kufanya mazoezi nakuongeza kuwa kutembea sana kwa gari badala ya miguu  kunachochea magonjwa hayo kwa kiasi kikubwa.

Akihutubu kwenye sala ya Ijumaa msikitini hapo, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Khalid Ali Mfaume aliwataka waumini wa dini ya kiislam kuchukua tahadhari na kuwa makini na shari za hamasa za kushajihisha ushoga duniani.

Alisema dunia imeharibika na kuenea kwa mawakala wanaoshajihisha uchafu huo kila kona hivyo, alieza hatua iliyofikia sasa kila kitu kinachoshabihiana na mfumo wa maisha  ya mwanadaamu kuwekewa nembo ama alama ya kushajihisha ushoga na kutolea mfano kwenye mavazi yakawaida kama nguo, mikanda, viatu na kwenye mahitaji ya lazima ya binaadamu.

Aidha, aliwaasa wazazi na walezi majumbani kuwa makini kufuatilia mienendo ya watoto wao, ikiwemo michezo na vitu vya kuchezea wanavyowanunulia pamoja na kuwaeleza kuwa makini na katuni wanazopenda kuangalia watoto ili kuhakikisha mazingira ya watoto hao hayaathiriwi na mfumo na hamasa za kishetani wanaohubiri ushoga.

Hata hivyo, aliongeza kusema mabadiliko ya uchumi na kupanda kwa gharama za maisha hazijasababishwa na uchumi pekee bali, dhambi za walimwengu na vitendo vichafu vya ushoga na udhalilishaji kijinsia vimechangia kukwamisha ugumu wa maisha duniani.

Msikiti wa Masjid Shifaa - Mwembetanga, ulizinduliwa raism na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi tarehe 07/05/2021 .

IDARA YAMAWASILIANO,

IKULU

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.