Habari za Punde

"Serikali imekusudia kampuni zote za mafuta kushushia mafuta yao hapa Mangapwani" -Dk. Mwinyi.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia katika viwanja vya Mangapwani wakati wa ufunguzi wa Bohari ya Mafuta ya Kampuni ya United Petroleum Zanzibar, katika eneo la Bandari Jumuishi Mangapwani Zanzibar Mkoa wa Kaskazini Unguja leo 4-3-2023 
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema eneo la Mangapwani kwa sasa litakuwa kituo kiuu cha biashara ya mafuta nchini.

Akizungumza kwenye ghafla ya uzinduzi wa Bohari ya mafuta Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amezitaka Wizara zinazohusika kuziambia kampuni zote za mafuta kuelekeza shughuli zote za mafuta kwenye eneo hilo.

"Serikali imekusudia kampuni zote za mafuta kushushia mafuta yao hapa Mangapwani" Alisema D.k Mwinyi.

Alisema hatua za awali za ujenzi wa bandari hiyo ni kuanza kwa ujenzi wa barabara kubwa ya kilomita 60 ambayo alieleza itakuwa barabara ya kwanza kubwa na yenye ubora kwa Zanzibar na uwezo wa kuhudumia magari makubwa ya kubebea mizigo mizito kulingana na uhalisia wa bandari yenyewe.

Dk. Mwinyi alisema bandari jumushi ya Mangapwani itahusisha bandari ya makontena itakayokuwa na gati ya urefu wa kilomita moja itakayohudumia sio Zanzibar pekee bali ukanda mzima wa Afrika Mashariki na makontena yatakayoshushwa bandarini hapo yaende hadi Dar es Salaam, Mombasa, Beira hadi Durban Afrika Kusini yakitokea Zanzibar.

"Tunataka bandari hii isihudumie Zanzibar pekee, tunataka Dar es Salaam, Mombasa, Beira hadi Durban Afika Kusini waitumie bandari hii " alieleza Dk. Mwinyi.

Bandari nyengine inayotarajiwa kujengwa eneo hilo Dk. Mwinyi alieleza ni bandari ya nafaka itakayohusisha ushushwaji wa bidhaa zote za vyakula ikiwemo mchele, maharage, mahindi, unga wa ngano na vyakula vyengine ambavyo vitashushwa kwa muda mchache ili viwafikie wananchi kwa wakati, ujenzi mwengine ni wa bandari ya mafuta itakayohifadhi lita milioni 21.

Rais Dk. Mwinyi alieleza bandari nyingine itakayojengwa kwenye eneo hilo ni bandari ya uvuvi itakayokidhi Sera ya Uchumi wa Buluu nchini, alisema bado Serikali haijavuna vyakutosha rasilimali za bahari na ujenzi wa bandari ya kisasa ya uvuvi inalengo la kuleta meli kubwa zitakazovuna vizuri matunda ya baharini wakiwemo Samaki wakubwa.

Vilevile Dk. Mwinyi alieleza Serikali inatarajia kuwa na mafuta ya kutosha na kuweka akiba ili Zanzibar iuze mafuta hadi nchi nyingine zisizokuwa na bahari na ujenzi wa bandari jumushi ya Mangapwani ni ufumbuzi wa changamoto zizilizopo kwenye bandari ya Malindi ambako meli hutumia siku 5, 7 hadi 10 kushusha mizigo hiyo, hali inayosababisha kupunguza uchumi wa nchi.

Akizungumzia kwenye hafla hiyo Waziri wa Maji, Nishati na Madini, Shaib Hassan Kaduara alisema Wizara hiyo inagusa maisha ya watu ya kila siku na kueleza nia ya Serikali kuwaondoshea wananchi changamoto zote zinazotokana na masuala ya maji, umeme na mafuta.

Alisema katika jitihada za Serikali kupunguza kero hizo, inatarajia kuzindua tangi kubwa la maji safi na salama Chakechake Pemba, lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita milioni moja ambalo litakua la kwanza kwa ukuwa kwa Zanzibar nzima.

Naye, Mkurugenzi wa masuala ya ushirika wa makampuni ya Bakhresa, Hussein Sufiani aliishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara na kutatua changamoto zinazowakabili wafanyabiasha pamoja na kuwafanikishia mradi wao huo wa Bohari ya Mafuta ya Mangapwani.

Aliihakikishia Serikali kwamba kampuni za Bakhresa zitaendelea kushirikiana na taasisi za Serikali zinazohusika na usimamizi wa majukumu yao ya kila siku na kuahidi kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja wao.

Baadae Rais Dk. Mwinyi alifanya ziara ya kushtukiza kwa kutembelea ujenzi wa mtaro Meli Kumi njia ya Bumbwini, ujenzi wa Soko la Chuini na Soko la Jumbi na Mwanakwerekwe kukagua ujenzi na maendeleo ya miradi hiyo ilivyofikia. Pia alitembelea eneo la waanika madagaa,  Mangapwani.

IDARA YA MAWASILIANO

IKULU, ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.