Habari za Punde

Wakala wa Chakula na Dawa Zanzibar (ZFDA) Wafanya ziara ya Kushtukiza

Baadhi ya mapolo ya mchele  yakiwa katika vifungashio visivyo vya asili katika ghala linalomilikiwa na Saleh Hassan khamis huko Mpendae Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi
Afisa Wakala wa Chakula na Dawa  Zanzibar (ZFDA) akiwa katika ukaguzi kuangalia usalama wa chakula na uhalali wa uwepo wa ghala la Saleh Hassan khamis huko Mpendae Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi.
Kaimu Mkurugenzi Idara ya usalama wa Chakula Wakala wa Chakula na Dawa ZFDA khadija Ali Sheha akizungumza na   Waandishi wa Habari kuhusiana na maghala yasiyo rasmi wakati alipokua akifanya ukaguzi kuangalia usalama na uhalali wa ghala linalomilikiwa na Saleh Hassan khamis huko  Mpendae Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi
Mmiliki wa ghala lisilorasmi Saleh Hassan Khamis akizungumza na waandishi wahabari wakati walipofika katika ukaguzi wa kushtukiza uliofanywa na ZFDA katika ghala hilo liliyopo Mpendae Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi.
Kaimu Mkuu wa ukaguzi na uteketezaji  ZFDA Eyduu Muhammed Naimu akilifunga ghala linalomilikiwa na  Saleh Hassan khamis baada ya kukosa sifa za kuhifadhia Bidhaa,wakati wa ukaguzi uliofanywa na ZFDA  kubaini uhalali wa Ghala hilo na usalama wa bidhaa zinazohifadhiwa hapo. Machi 16.2023.
Picha na Fauzia Mussa -Maelezo Zanzibar. 

Na Fauzia Mussa. Maelezo Zanzibar                                                            

Wakala wa chakula na Dawa Zanzibar (ZFDA) wamelifungia ghala  iliyokua ikihifadhi bidhaa mbalimbali ukiwemo mchele  kutokana na ghala hiyo kukosa sifa za kuhifadhia bidhaa za vyakula.


Akizungumza wakati wa ukaguzi wa kushtukiza kuangalia usalama wa chakula,na uhalali wa uwepo wa ghala hilo huko Mpendae Kaimu Mkurugenzi Idara ya usalama wa chakula ZFDA Bi.Khadija Ali Sheha amesema ukaguzi huo umebaini kuwa ghala hilo halijasajiliwa na haliko katika hali ya usafi na haliruhusu hewa kupita hali inayopelekea chakula kinachihifadhiwa hapo kutokua salama.

 

Alisema kuwa usalama wa chakula ni jukumu la kila mmoja  hivyo ameitaka jamii kutoa taarifa mapema mara tu wanapoona hali isiyokuwa ya kawaida katika maghala ya kuhifadhia chakula

 

"Kwa pamoja sasa tushirikiane kulinda Afya zetu  kwa kuyafichuwa maghala kama haya ambayo yanahatarisha Afya za watu na kuitia hasara Serikali" alishauri kaimu huyo.

 

Aidha katika ukaguzi huo ZFDA wamebaini kuwa mmiliki wa ghala hilo amekua akiziba vifungashio vya asili kwa baadhi ya bidhaa zilizozuiliwa kusafirishwa nje ya Zanzibar ikiwemo mchele aina ya mapembe katika maboksi na vipolo ili kurahisisha usafirishaji  Jambo ambalo ni kosa kisheria.

 

Kwa upande wake mmiliki wa ghala hilo Bw.Saleh Hassan Khamis amesema kuwa amekua akizifunga tena bidhaa hizo katika mapolo na maboksi ili kuzihifadhi na kuziweka salama wanapokua safarini bila kufahamu kufanya hivyo kama ni kosa kisheria, hivyo Bw.Saleh ameiomba ZFDA kuwapatia elimu Wafanyabiashara ili kuepuka makosa yasiyotarajiwa.

 

Nae Sheha wa Shehia ya Mpendae Bw.Suleiman Ali Makuu amewasihi wafanya Biashara kuwa waaminifu na kuwataka  wafuate  Sheria zilizowekwa na Serikali ili kuepuka matatizo wakati wanapofanya Biashara zao.

 

Katika Ukaguzi huo  mbali na bidhaa nyengine jumla ya polo mia tatu za mchele aina ya mapembe yenye ujazo wa kilo hamsini yamekutikana katika ghala hilo ambalo halijasajiliwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.