Habari za Punde

Alhaj Dk. Hussein Ametowa Shukrani kwa Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, baada ya kumalizika kwa hafla ya Iftari maalum aliyowaandalia katika ukumbi wa Chuo cha Amali Mkokotono Wilaya ya Kaskazini "B" Unguja. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi amejumuika kwenye futari ya pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni kawaida yake kufuturu na wananchi kila mwaka katika kutekeleza ibada ya mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Katika hafla hiyo iliyofanyika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo ya Amali, Mkokotoni wilaya ya Kaskazini A, Unguja alikowaandalia futari wananchi wa Mkoa huo imehudhuriwa pia na Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi.

Al hajj Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwashukuru wananchi wa Mkoa wa Kaskazini kwa mwitikio mkubwa waliomuonesha kujumuika nae kwenye futari ya pamoja aliyowaandalia.

“Leo ni siku yetu ya kwanza tangu tumeanza kufutarisha, tumeanza na Mkoa huu wa Kaskazini Unguja, nawashukuru wananchi nyote kwa muitikio muliouonesha, ushirikiano wenu tokea maandalizi hadi kukamilika kwa shuhuli yetu….”

“….Unapowaalika watu na wakakuitikia basi hunabudi kutoa shukurani kwao, nawashukuru sana nyote kwa ushiriki wenu na kwa niaba ya wenzenu hakika mumewawakilisha vyema wenzenu, nayaona makundi yote mupo hapa” Alieleza Al hajj Dk. Mwinyi.

Akizungumza kwenye halfa hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Haroun Ali Suleiman alisifu jitihada za rais Dk. Mwinyi katika kuungamkono masuala ya dini na kushajihisha mambo yenye heri na maendeleo ya nchi.

Alisema taifa linamshughudia anavyoshiriana na wananchi wa visiwa vya Unguja na Pemba kwenye mambo mbalimbali ya kijamii na hairati, ikiwemo kushiriki kwenye ibada za sala za jamaa maeneo tofauti ya visiwa vya Zanzibar, kufungua misikiti pamoja na kufutari pamoja na wananchi wake jambo alilolieleza ni la kupigiwa mfano kwa kiongozi wan chi na kumsifu Dk. Mwinyi kwamba ni Rais wa watu wote.

Kwa upande wao, wananchi wa mkoa huo wamesifu juhudi za maendeleo zinazofanywa na awamu ya nane ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kueleza kasi ya maendeleo ya mkoa huo imezidi maradufu.

Walisema maendeleo kwenye sekta ya miundombinu ikiwemo maji safi, barabara na kiwanja cha ndege ndani ya mkoa huo zimefungua fursa nyingi za uchumi na maendeleo katika usatawi wa mkoa wao.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mkuu wa Mkoa huo, Ayoub Mohamed Mahmoud alisema Mkoa huo unazidi kufunguka kimaendeleo kwa kuimarika na kuongezeka kwa huduma za maji safi, afya, elimu, kilimo, ujenzi mkubwa wa bandari jumuishi ya Mangapwani, huduma hizo zina badari ya Mkokotoni.

Alisema, kukua kwa sekta ya utalii kwenye mkoa huo na biashara ndogondogo zimeufungua mkoa kibiashara na uwekezaji.

“Tunakushukuru na kukupongeza kwa dhati kwa kutuandalia futari hii wananchi wa Mkoa wa Kaskazini pia tunakupongeza kwa kazi kubwa ya maendeleo unayoifanya kwenye Mkoa wetu” Alishukuru RC Ayoub.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.