Habari za Punde

Sekta ya Uvuvi na Kilimo ni Utajiri - DKT.YONAZI

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi  akizungumza wakati wa kikao chake na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa alipomtembelea ofisini kwake wakati wa ziara yake ya kikazi kukagua utekelezaji wa program ya Kuendeleza sekta ya Kilimo na Uvuvi ya AFDP inayoratibiwa na Ofisi yake mkoani Morogoro.
Mkurugenzi wa Uzalishaji Wakala wa Mbegu za kilimo (ASA) Dkt. Justine Ringo akimuonesha Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi mitambo ya kuchakata mbegu za kilimo wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa program kuendeleza kilimo na uvuvi inayoratibiwa na ofisi yake.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi akikagua mbegu za mpunga zilizohifadhiwa katika vifungashio katika mashine za kuchakata mbegu za kilimo za Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) kilichopo katika Mkoa wa Morogoro.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi (mwenye suti ya blue) pamoja na timu aliyoongozana nayo wakikagua moja ya bwawa la kuhifugia samaki lililopo katika Kituo cha Viumbe Maji (DAQ) kilichopo Kingolwira mkoani Morogoro wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa program ya AFDP.

 (PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)

NA.MWANDISHI WETU                                                                                                   

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshugulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amesema sekta ya kilimo na uvuvi zinatija katika kujiletea maendeleo ya taifa letu kwa kuzingatia fursa zilizopo.

Ametoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya Kuendeleza sekta ya Kilimo na Uvuvi ya AFDP inayoratibiwa na ofisi yake Mkoani  Morogoro.

Dkt. Yonazi alitembelea baadhi ya Wilaya zinazotekeleza mradi huo ikiwemo Morogoro Mjini na Kilosa ambapo alikagua utekelezaji huo katikaTaasisi ya Utafiti wa Mbegu (TIRA), Taaasisi ya Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA), Taasisi ya Udhibiti wa Ubora wa Mbegu (TOSCI) pamoja na Kituo cha Viumbe Maji (DAQ) kilichopo Kingolwira mkoani Morogoro.

Alifafanua kuwa Tanzania inautajiri mwingi kupitia fursa zinazotokana na sekta hizo huku akieleza kuwa nchi ya Tanzania itakuwa kituo cha maarifa ya kujifunza kilimo na uvuvi kwa nchi za Afrika Mashariki kutokana na jitihada za Serikali katika kuwekeza katika sekta hizo.

Aliongezea kuwa kupitia mradi wa kuendeleza sekta ya kilimo na uvuvi utasaidia kuendelea kuboresha miundombinu muhimu kwa lengo la kuhakikisha ufugaji unakuwa sehemu ya pato la taifa na kuchangia kasi ya maendeleo pamoja na kuliingizia taifa fedha za kigeni.

“Tanzania imeendelea kuwekeza katika sekta ya uvuvi na kilimo, na hii itaipa nafasi nchi yetu kuwa kituo cha maarifa ya kujifunza masuala ya kilimo na nchi zinazotuzunguka, ni muda sahihi kuendelea kuweka nguvu zaidi kwa kuzingatia mazingira yetu ya uwekezaji,”alisema

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa alipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuleta miradi hiyo katika mkoa wake huku akiitaja Morogoro kwa mafanikio makubwa eneo la kilimo na uvuvi kwa kuzingatia ardhi yenye rutuba kwa mkoa wa Morogoro.

“Mkoa wetu una mvua nyingi na umeendelea kuwa mzalishaji mzuri wa mazao ikiwemo mpunga. Tumeendelea kuwa wa kwanza kwa uzalishaji wa mpunga nchini,  namba sita kwa uzalishaji wa ndizi, namba nne kwenye G5 katika uzalishaji wa chakula nchini, malengo yetu ni kufanya vizuri zaizi ili kusogea kutoka nafasi ya nne kitaifa kuwa nafasi nzuri zaidi,”Mhe. Mwassa

Aliongezea kuwa, mkoa wake umeendelea kutoa kipaumbele katika masuala ya kilimo kwa kuendelea kutenga bajeti.

Awali akieleza lengo la mradi wa AFDP Mratibu wa program hizo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Salimu Mwijaka alisema, hadi sasa mradi umefikia mikoa 11 ikiwemo; Morogoro, Geita, Lindi,Tanga, Pwani, Dodoma, Singida, Manyara,Tabora, Geita, Shinyanga na Mwanza na kueleza umejipanga kufanya vizuri kwa matokeo yenye tija.

“Mradi huu umejikita katika maboresho maeneo mengi ikiwemo ya kuboresha networking ya distribution ya mbegu, na kuhakiksiha tunaboresha maeneo ya umwagiliaji, upatikanaji wa vifaa kama matrekta katika mashamba, udhibiti wa mbegu katika maabara aidha upande wa samaki tumeendelea kujenga na kuongeza uwezo wa vitotoreshi vya vifaranga vya samaki, kuboresha mabwawa ya kufugia samaki,“alisema Mwijaka

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Kituo cha Ukuzaji viumbe Maji cha Kingolwira Bi.Gillness silayo alieleza faida za program ambayo utaleta unafuu kwa kutatua changamoto wanazokabiliana nazo ikiwemo uchakavu wa mabwawa na ukosefu wa maji.

“Mradi IFAD utatusaidia kuboresha mabwawa yetu 20 hivyo kuongeza makusanyo ya maduhuri, pamoja na hilo mradi utatuchimbia visima vitavyotatuta changamoto ya maji katika ufugaji wa samaki,”alisema Gillness

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.