Habari za Punde

SMZ Ina Nia ya Dhati ya Kujinufaisha Zaidi na Matunda ya Baharini Kupitia Sera Yake ya Uchumi wa Buluu

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Balozi wa Canada Nchini Tanzania Kyle Nunas, alipofika  Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Balozi wa Canada Nchini Tanzania Kyle Nunas, alipofika  Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na mgeni wake Balozi wa Canada Nchini Tanzania.Mhe.Klye  Nunas, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar .

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema ina nia ya dhati ya kujinufaisha zaidi na matunda ya baharini kupitia sera yake ya Uchumi wa buluu kwa kuvuna mengi zaidi kuliko inavyoendelea kunufaika ili kuimarisha uchumi wa nchi.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Balozi wa Canada nchini Tanzania, Kyle Nunas aliefika kumtembelea.

Alisema, kupitia sekta ya uchumi wa buluu Zanzibar pia inanufaika na biashara kupitia bahari kwa mipaka jirani ya Dar es Salaam, Tanga, Mombasa na na visiwa jirani vikiwemo Comoro.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alimueleza balozi huyo kwamba Utalii ni sekta namba moja ya uchumi wa Zanzibar ambapo alisema Serikali imejikita kuimarisha miundombinu yote ikiwemo ujenzi wa babdari jumuishi ya Mangapwani ambayo itatoa fursa zaidi za uchumi, kutanua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Abeid Amani Karume kwa kuongeza jengo jipya la (Terminal 4), kuboresha barabara, kuongeza hoteli za kisasa na nyumba za wageni pamoja na kuimarisha vivutio vya utalii.

Dk. Mwinyi alieleza, Zanzibar kwasasa inapokea ndege nyingi za kimataifa kiasi cha kuongeza idadi kubwa ya watalii nchini, pia alimueleza mgeni wake huyo kwamba Serikali ina nia ya kulifufua eneo kongwe la hoteli ya bwawani kwa kujengwa kumbi kubwa za mikutano kwaajili ya watalii ili kuongeza mapato ya nchi.

Akizungumzia sekta za afya na elimu, Rais Dk. Mwinyi alimueleza balozi huyo kwamba Serikali pia inaendelea kuboresha upatikanaji wa huduma bora hasa kwenye maeneo ya vijijini ili kujenga uwiano sawa wa huduma na sehemu za mijini.

Kwa upande wa afya, Rais Dk. Mwinyi alieleza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inazingatia kukuza huduma ya afya ya kinga kwa mama na mtoto na mapambano dhidi ya magonjwa ya kuambukiza.

Alisema, uhisusiano wa diplomasia baina ya Tanzania na Canada ni wa muda mrefu pia alieleza Zanzibar ikiwa sehemu ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, imefaidika na uhusiano huo hasa kupitia sekta za Afya na Elimu.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Balozi Kyle Nunas ameisifu Tanzania ikiwemo Zanzibar kwa kubarikiwa kuwa na amani na utulivu na siasa za kistaarabu katika kuimarisha ustawi wa nchi yake.

Balozi Kyle Nunas alimueleza Rais Dk. Mwinyi, kwamba Canada inaungamkono zaidi masuala ya haki za binaadamu hasa kwa makundi maalumu wakiwemo wanawake wa wasichana ambapo imeelekeza sera na miradi mingi kwenye eneo hilo.

Alisema Canada imevutiwa zaidi na ustaarabu wa Tanzania hasa katika kuimarisha demokrasia, uhuru wa vyombo vya Habari pia balozi huyo alimueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba nchi yao inavutiwa kuiona Tanzania inavyoendeleza siasa za kistaarabu na mazungumzo ya busara kwa kambi pinzani.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.