Habari za Punde

Wananchi Watakiwa Kutoa Taarifa za Madereva Wazembe

Na Issa Mwadangala.

Abiria wanaosafiri kwenda sehemu mbalimbali ndani na nje ya Mkoa wa Songwe wametakiwa kutoa taarifa za madereva wasiofuata sheria za usalama barabarani ili hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yao.

Hayo yamesemwa Disemba 28, 2023 na Kamanda wa Polisi mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Theopista Mallya baada ya kufanya oparesheni ya ukaguzi wa magari ya abiria katika eneo la Chimbuya na Mahenje wilayani Mbozi.

Kamanda Mallya aliwataka abiria wanaosafiri kwenye mabasi kutoka Songwe kwenda maeneo mengine kutofumbia macho vitendo vya ukiukwaji wa sheria za usalama barabarani na badala yake aliwataka kukemea vitendo hivyo na kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa.

Aidha, alisisitiza na kuwataka makondakta na madereva kutokuzidisha abiria pia kutoa tiketi kwa abiria wao kama sheria na taratibu za usafirishaji abiria zinavyoelekeza.

Jeshi la Polisi nchini linaendelea na operesheni za ukaguzi wa vyombo vya moto ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa jamii kuhusu masuala ya usalama barabarani ili kutokomeza ajali za barabarani hasa kwa watumiaji wa vyombo vya moto na watembea kwa miguu kwa lengo la kupunguza ajali ambazo zinaepukika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.