Habari za Punde

Matembezi ya Vijana wa UVCCM Mkoa wa Kusini Unguja

KIONGOZI Mkuu wa Matembezi Machano Ali Machano,akinunua matunda aina ya embe kwa wajasiriamali wadogo wadogo wa kijiji cha Pete wakati msafara wa matembezi ukipita katika kijiji hicho.
BAADHI ya Vijana wa Chama Cha Mapinduzi wanaoshiriki matembezi  wakinunua bidhaa za katika soko la Kikungwi Wilaya ya Kusini Unguja.
BAADHI ya vijana wa UVCCM wakiwa katika matembezi ya kuadhimisha miaka 60 ya Mapinduzi wakiongozwa na Kiongozi Mkuu wa matembezi Machano Ali Machano,wakinunua mazao ya baharini aina ya Chaza kwa mjasiriamali wa Soko la Kikungwi Wilaya ya Kusini Unguja.
BAADHI ya Viongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi UVCCM wakiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar Mussa Haji Mussa,wakiwa katika Matembezi ya kuadhimisha miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika maeneo ya Kijiji cha Pete Wilaya ya Kusini Unguja.

Na.Is-Haka Omar - Zanzibar.

WANANCHI wa Mkoa wa Kusini Unguja,wameshauri kuthamini na kuunga mkono juhudi za Serikali za kuweka mazingira rafiki na shirikishi ya kila mwananchi kujiajiri mwenyewe kupitia fursa za ujasiriamali.

Ushauri huo umetolewa na Kiongozi Mkuu wa Matembezi ya UVCCM ya kuadhimisha miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar Machano Ali Machano,wakati akizungumza na wajasiriamali wa matunda njiani wakati wa matembezi kutoka Kijiji cha Mtule hadi Tunguu Wilaya ya Kati Unguja.

Amesema fursa ya kila mwananchi kujiari na kufanya biashara yoyote iliyokuwa halali bila kusumbuliwa na kuwekewa vikwazo ni sehemu ya mafanikio iliyofikiwa katika kipindi cha miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Machano,alifafanua kuwa pamoja na mambo mengine Matembezi hayo ni jukwaa la Vijana wa Chama Cha Mapinduzi kushiriki na kuendeleza mambo mema yaliyotekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jamii.

“Kupitia matembezi haya tunawaomba wananchi waliojiajiri katika ujasiriamali mbalimbali waendelee kufanya kazi zao kwa bidii ili wapate kujikwamua kiuchumi na kwamba UVCCM itaunga mkono juhudi hizo”, alisema Machano.

Katika maelezo yake Machano,alifafanua kuwa ndani ya kipindi cha miaka 60 ya Mapinduzi Serikali imetekeleza kwa ufanisi mkubwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2023 kwa kujenga miundombinu ya barabara,maji safi na salama,afya,elimu,kilimo na ufugaji ndani ya Wilaya hiyo.

Alisema dhamira ya kufanya Mapinduzi ilikuwa ni kuwakomboa wananchi kutoka katika utawala wa kigeni na wajitawale wenyewe katika nyaja za kiuchumi,kisiasa na kijamii.

Aidha,katika matembezi hayo yameambatana na kazi za ujenzi wa Taifa kwa kupanda miti zaidi ya 2000 katika eneo la Chuo cha Mafunzo na Uongozi cha CCM Tunguu pamoja na kuzindua mradi wa ufugaji wa kuku wa Chuo hicho.

Matembezi hayo yanajumuisha zaidi ya vijana 1000 kutoka Mikoa yote ya Tanzania baada ya kumalizika katika mikoa yote ya Pemba sasa yanaendelea katika Mikoa ya Unguja, ‘’Kauli mbiu ikiwa ni Miaka 60 ya Mapinduzi,Miundombinu ni msingi wa maendeleo’’.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.