Habari za Punde

SMZ Imepiga Hatua Kubwa Kwenye Kukidhi Ukuaji wa Sekta ya Usafiri wa Aanga kwa Kufanikisha Miradi Kadhaa ya Sekta Hiyo kwa Nia ya Kuongeza Ufanisi na Kukuza Utalii wa Nchi

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia na kulifungua Kongamano la 6 la Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, linalofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar Wilaya ya Mjini Unguja Jijini Zanzibar leo 15-5-2024

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, imesema imepiga hatua kubwa kwenye kukidhi ukuaji wa sekta ya usafiri wa anga kwa kufanikisha miradi kadhaa ya sekta hiyo kwa nia ya kuongeza ufanisi na kukuza utalii wa nchi kwa maendeleo ya Taifa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo alipofungua Kongamano la Sita la Usafiri wa Anga la Jumuiya ya Afrika Mashariki, hoteli ya Verde, Mtoni Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema, Sekta ya Utalii ni muhimu kwa mikakati ya maendeleo ya uchumi wa nchi na Usafiri wa Anga ni kichocheo kikuu cha ukuaji wa Uchumi hasa kwenye kufikia malengo ya nchi iliyojiwekea kupitia sekta ya utalii na biashara kuna haja ya kusaidia ipasavyo sekta ya usafiri wa anga.

Akizungumzia mafaniko ya sekta ya usafiri wa Anga kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Rais Dk. Mwinyi alisema, Serikali imekamilisha mradi wa ujenzi wa jengo jipya la abiria (Terminal 3) kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume ambalo kwasasa linafanyakazi kwa ufanisi mkubwa wa kutoa huduma za usafiri wa anga Zanzibar.

Pia alieleza, Serikali imeanza ujenzi wa jengo jipya la abiria (Terminal 2) lenye ukubwa wa mita za mraba 16,000 litakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya abiria 1,300,000 kwa mwaka ambalo awali lilijengwa mwaka 1974 kwa sasa linahitaji marekebisho makubwa pamoja na ujenzi wa sehemu ya kuegesha magari yenye uwezo wa kuhudumia magari zaidi ya 200 kwa wakati mmoja.

Dk. Mwinyi pia alisema, Serikali inatekeleza mradi wa ujenzi, ukarabati na uboreshaji wa jengo la zamani la (Terminal 1) kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume ambalo awali lilijengwa miaka ya 1950 pamoja na kutekeleza mradi wa ujenzi wa Kituo cha biashara, kitakachojumuisha maduka, migahawa, huduma za kibenki na ofisi, ujenzi wa eneo la kuhifadhi na kusafirisha chakula pamoja na  ujenzi wa vituo vipya vya kutolea huduma za mafuta ya anga kwa makampuni ya Oilcom, GBP na Lake Oil.

Alieleza, Serikali pia inatekeleza mradi wa ujenzi na utanuzi wa Uwanja wa ndege wa Pemba unaojumuisha upanuzi wa urefu wa njia ya kurukia ndege kutoka mita 1,525 hadi mita 2,510, ujenzi wa maegesho ya ndege (apron) yenye uwezo wa kuchukua ndege mbili kubwa aina ya Code C (B 737-800) na ndege 8 ndogo za Code B na ujenzi wa jengo jipya la abiria lenye ukubwa wa mita za mraba 9,170 pamoja na ujenzi wa Uwanja cha ndege wa Nungwi unaolenga kuhudumia zaidi shughuli za utalii zinazoongezeka Zanzibar.

Dk. Mwinyi alieleza, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inazingatia mikataba yote ya usafiri wa anga ya kimataifa ili kuhakikisha ukuaji wa sekta hiyo unaendelea kuwa salama.

Pia alieleza, Tanzania inajivunia mafanikio yaliyofikiwa kwenye sekta ya usafiri wa anga kwa kuendelea kushirikiana na nchi washirika chini ya mwavuli wa Taasisi ya Udhibiti wa Usalama wa Usafiri wa Anga ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, katika kuoanisha kanuni za usafiri wa anga ndani ya ukanda huo kwa lengo la kuoanisha taratibu, kuimarisha usalama, na kuongeza ufanisi.

Alisema, Serikali imeboresha mradi wa Masafa ya Mbali (VHF) unaojumuisha ufungaji wa vituo 18 vipya na redio kwenye Viwanja vya Ndege 12, na uwekaji wa mifumo ya kinasa sauti katika viwanja vinne vya ndege, Uwekaji wa Mfumo wa Kutua kwa ndege (ILS) kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume.

Aidha, Dk. Mwinyi alieleza mwaka jana Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipata asilimia 87 katika kuhakikisha usalama na ufanisi kwenye Mpango wa Kimataifa wa Ukaguzi wa Usalama wa Kimataifa, uliofanywa na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO) ukiwa na lengo la kukuza usalama wa usafiri wa anga duniani kupitia ukaguzi na ufuatiliaji wa mara kwa mara wa utendaji wa usalama wa anga wa Nchi Wanachama.

Hivyo, aliwata wadau na washirika wa usafiri wa anga kuimarisha ushirikiano ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua kwa usalama sambamba na kuwa himiza kujadili na kutoa mapendekezo sio tu jinsi changamoto zilizoainishwa katika maeneo hayo zinavyoweza kutatuliwa, bali pia kubainisha jinsi fursa zinazohusiana na maeneo hayo zinavyoweza kutumika kikamilifu kwa manufaa ya usalama wa anga, uwezo, ufanisi na ulinzi wa mazingira kwenye Ukanda wa nchi za Afrika Mashariki.

Naye, Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi, Dk. Khalid Muhamed Salum alisema Sekta ya usafirishaji wa Anga inakisia zaidi ya abiria milioni tatu husafiri kwa anga kila siku kutokana na umuhimu wa haraka wa safari zake.

Hivyo aliwasiri washiriki wa kongamano hilo wakiwemo nchi wanachama kujadili kwa kina masuala ya usalama, gharama na ufanisi ili kuwe kupatikane tija kwa changamoto zilizomo kwenye sekta hiyo.

Sambamba na kuahidi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoa ushirikiano kwa wadau hao ikiwemo Serikali ya Jamuhiri ya Muungano wa Tanzania.

Kongamano la Sita la Usafiri wa Anga la Jumuiya ya Afrika Mashariki, umewakutanisha wadau wa tasnia hiyo kwa siku mbili mfululizo ukiwa na kauli mbiu “Mustakabali wa Usafiri wa Anga: Kudumisha Mifumo ya Usafiri wa Anga yenye Ustahimilivu, Uendelevu, Ubunifu na Usalama" limezishirikisha nchi wanachama kutoka mataifa ya Afika Kusini, Burundi, Jamuhuri ya Demokrasia ya Congo, Kenya, Ethiopia, Somalia, Sudani Kusini, Rwanda na mwenyeji Tanzania ikiwemo Zanzibar. Mwezi Febuari mwaka 2020 kongamano kama hilo lilifanyika jijini Bujumbura, Burundi.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.