Habari za Punde

Rais wa Zanzibar naMwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Azungumza na Waziri wa Kilimo wa Iran Ikulu Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dr.Gholamreza Nouri (kulia kwa Rais wa Pili ) mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 18-10-2024, akiwa na ujumbe wake.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameitaja Sekta ya Kilimo kuwa eneo muhimu litakaloimarisha ushirikiano wa dipolomasia baina ya Tanzania na Iran.

Dk. Mwinyi amehimiza Ushirikiano huo kwa kuisifu Iran kuwa ni wabozi kwenye teknolojia ya kilimo.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Dr. Gholamreza Nouri aliefika na ujumbe wa wataalamu 15 kutoka sekta mbalimbali za maendeleo za nchi hiyo.

Dk. Mwinyi amesema Kilimo ni sekta kubwa ya Uchumi wa Tanzania Bara kulingana na kubarikiwa kuwa na eneo kubwa kijiografia, hivyo, ameisihi Iran kuimarisha ushirikiano kwa kubadilishana uzoefu, mbinu na teknolojia kwenye eneo hilo.

Kuhusu Zanzibar, Rais Dk. Mwinyi amesema inajikita zaidi kwenye kilimo cha viungo (Spices) kutokana na sehemu kubwa ya uchumi wake kutegemea soko la Utalii ambao unachangia asilimia kubwa ya uchumi wa nchi.

Pia, Dk. Mwinyi alimweleza mgeni wake huyo kuhusu kuzihuisha na kuziimarisha sehemu za historia katika kukuza soko la Utalii wa Urithi na kuboresha ushirikiano uliopo baina ya Tanzania hasa Zanzibar na Iran kwenye eneo hilo la utalii.

Halikadhalika, Rais Dk. Mwinyi amegusia Sekta ya Usafirishaji wa baharini na kuiomba Irani kuongeza ushirikiano kwenye eneo hilo ili kuimarisha biashara na uchumi kupitia bandari za pande mbili hizo za ushirikiano.

Akizungumzia ushirikiano na sekta binafsi baina ya Tanzania kususan Zanzibar na Iran, Rais Dk. Mwinyi amamuahidi Waziri huyo kwamba “Chamber of Commerce” ya Zanzibar itaimarisha ushirikiano na ya Iran kuona Uchumi endelevu baina ya pande mbili hizo.

Naye, Waziri Dr. Gholamreza alisifu ushirikiano mzuri wa Diplomasia uliopo baina ya Iran na Tanzania na kuongeza kuwa katika kuboresha ushirikino wao wameikaribisha Tanzania nchini kwao na kuwaahidi kuwapa eneo la kufungua ubalozi wa Tanzania nchini Iran.

Pia Waziri huyo, amesema watasaini makubaliano na Tanzania hasa Zanzibar kwenye sekta mbalimbali za maendeleo ikiwemo Kilimo, Utalii, Elimu, Biashara na Sekta ya uhandisi pamoja na kuahidi kutoa ushirikiano na kubadilishana uzoefu, mbinu na teknolojia kwenye maeneo hayo.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akimkabidhi zawadi maalumu ya Mlango wa Zanzibar mgeni wake Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dr.Gholamreza Nouri, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo. 18-10-2024
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akikabidhiwa zawadi maalumu ya picha na mgeni wake Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dr.Gholamreza Nouri, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo. 18-10-2024
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na mgeni wake Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dr.Gholamreza Nouri, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo. 18-10-2024.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.