Habari za Punde

Haki za Watumishi Zilindwe Katika Sehemu za Kazi

Na.OMWKR 

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, amewataka wataalamu wa Rasilimali watu na Utawala kuhakikisha kwamba haki za watumishi katika sehemu za kazi zinalindwa sambamba na kuthamaniwa utu wao.

Mhe. Makamu ameyasema hayo alipomuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Husein Ali Mwinyi katika maadhimisho ya siku ya Rasilimali watu duniani  yaliyofanyika katika hoteli ya New Aman wilaya ya mjini Mkoa wa Mjini Magharib Unguja.

Mhe. Othman amewataka wataalamu hao kuhakikisha kwamba wanasimamia vyema maadili , weledi na uadilifu , usawa na ushirikishwaji  hasa kwa watu wa makundi maalumu katika sehemu za kazi.

Aidha amehimiza kuwepo mipango maalum na endelevu  ya kuwajengea  uwezo watumishi kwa kutoa mafunzo mbali mbali yenye lengo la kuongeza ufanisi na kuleta tija katika sehemu za kazi na taifa kwa jumla.

Mhe. Othman ameeleza kwamba hatua hiyo inatokana na ukweli kwamba hivi sasa taaluma ya rasilimali watu imegeuka kuwa chombo muhimu cha kuleta mabadiliko ya kiutendaji na kwamba taaluma hiyo kwa sasa inazidi kuwa ni mkakati wa msingi katika kuzidisha ufanisi kwenye taasisi mbali mbali za kazi.

Hivyo, Mhe. Othman amesisititiza kwamba kutokana na hali hiyo taifa linawajibu wa kuendeleza, kulinda na kuenua taaluma hiyo ili izidi  kutoa mchango katika jitihada za taifa za kufanikisha kuleta maendeleo ya nchi.

Amesema kwamba kwa upande wa serikali itaendelea kukuza mazingira bora kupitia uimarishaji na kufanya mageuzi makubwa katika mifumo ya utoaji huduma na kiutumishi  wa umma kwa kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuhimiza matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa rasilimali watu na kuleta maendeleo ya kiuchumi nchini.

Mhe. Othman amesema kwamba ni vyema juhudi hizo zikaungwa mkono kwa ushirikiano wa sekta zote kwa kuzingatia kwamba hivi sasa sekta binafasi nayo inaendelea kuwa na mchango mkubwa  katika ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi.

Mhe. Othman amesisitiza kwamba maendeleo ya taifa yatategemea sana ubora wa watu wake wenye ujuzi , maadili, moyo wa kizalendo na uwezo mkubwa wa kutoa matokeo bora katika kazi mbali mbali za kiutumishi  wanazozifanya.

Amesema kutokana na hali hiyo, serikali za Tanzania zinafanya juhudi kubwa katika uwekezaji wa rasilimali watu kwa kuwapatia watumishi  ujuzi na taaluma za aina mbali mbali ili wawe chachu ya kufanikisha mipango mbali mbali ya maendeleo ya taifa inayowekwa.

Aidha Mhe. Othman ametaka Taasisi hiyo kuwasaidia  watumishi na viongozi mbali mbali wa Zanzibar kuwajenga kwenye utamaduni wa uwajibikaji bora na kujenga nidhamu ya kazi na kuwafanya wafanyakazi watambue kwamba kazi wanayofanya ni yao na sio ya muajiri .

Naye waziri wa Nchi Ofisi ya rais Katiba, Sheria , Utumishi na Utawala bora  Haroun Ali Suleiman, amesema kwamba ni muhimu kwa taasisi na wadau mbali mbali kukutana kujadili kuweza kuzipatia ufuimbuzi changamoto mbali ,mbali zinazoikabili Jumuiya hiyo ya wanataaluma.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumiya ya Wanataaluma ya Raslimali watu Tanzania Christopher Kabalika Mwansasu, ameipongeza serikali kwa kuboresha maeneo ya huduma , kuimarisha mifumo ya rasilimali watu pamoja na kuwekeza kwenye nguvu kazi ya rasilimali watu ili kuliwezesha taifa kujiandaa na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani.

Amesema kwamba Sekta ya rasilimali watu ni muhimu katika kutoa mchango wa kukabiliana na mabadiliko yanayotokea duniani na kuwa mshindani sahihi katika kusimamia kazi kwa viwango vya juu ili  kuleta maendeleo kwani dhima ya wataalamu ni kusimamia viango bora vya kazi na kufikia malengo ya kuwakilisha na kuendeleza ujuzi wa wanachama katika majukwaa ya kitaifa na kimataifa ambako masuala ya rasilimali watu yanajadiliwa.

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha wanataaluma ya Rasilimali watu  Tanzania, (THRAPA),  Denes Dehua amesema kwamba lengo kuu la taasisi hiyo ni kukuza  viwango vya taaluma  kwa watumishi pamoja na kulinda maadili  katika maendeleo ya rasilimali watu kwa kushirikiana na vyombo mbali mbali ikiwemo serikali.

Mwisho

Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kupitia Kitengo chake cha Habari Leo Jumanne Mei 20, 2025.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.