Habari za Punde

Waziri Mkuu wa Jmhuri ya Muungano wa Tnzania Mhe.Kassim Majaliwa Akagua Mabasi Mapya na Miundombinu ya Awamu ya Pili ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua mabasi ya  awamu ya pili ya maradi wa mabasi yaendayo  haraka (BRT - 2) kwenye Bandari ya Dar es Salaam, Agosti 13, 2025.  Wa pili kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, William Lukuvi na Kulia ni Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Zainab Katimba .
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa ndani ya basi  wakati alipokagua mabasi mapya ya  awamu ya Pili ya maradi wa mabasi yaendayo  haraka (BRT - 2) kwenye Bandari ya Dar es Salaam.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, William Lukuvi  (kushoto kwake) wakikagua kituo cha mabasi yaendayo haraka Mbagala Rangi Tatu wakati Waziri Mkuu alipokagua mabasi mapya ya  awamu ya Pili ya maradi wa mabasi yaendayo  haraka (BRT - 2) kwenye Bandari ya Dar es Salaam, na vituo vikuu vya mabasi hayo, Gerezani na Mbagara Rangi tatu
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akishuhudia abiria waliokuwa wakilipa nauli ya  mabasi yaendayo haraka  kwa kutumia kadi wakati alipotembelea kituo cha mabasi hayo awamu  pili cha Gerezani jijini Dar es salaam, Agosti 13, 2025. Kushoto ni Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Zainab Katimba.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiagana na viongozi baada ya kukamilisha ziara ya kukagua mabasi mapya ya awamu ya pili ya mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT - 2) na vituo vya mabasi hayo Mbagala  Rangi Tatu na Gerezani jijini Dar es salaam, Agosti 13, 2025. Kutoka kushoto ni Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Zainab Katimba, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, William Lukuvi na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Jim Yonaz.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amewaagiza waendeshaji wa awamu ya pili ya mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (BRT-2) kuhakikisha wanafanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha maeneo yaliyobaki yatakayowezesha mradi huo kuanza kutoa huduma ndani ya muda mfupi.

 

Amesema hayo leo Jumatano (Agosti 13, 2025) wakati alipokagua mabasi mapya kwa ajili ya awamu ya pili ya mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT-2) pamoja na miundombinu ikiwemo kituo kikuu cha mabasi hayo cha Mbagala Rangi tatu na kituo cha gerezani, jijini Dar es Salaam. Pia alitembelea ujenzi wa kituo maalum cha kujazia gesi kwa ajili ya mabasi hayo, kinachojengwa katika kituo cha Mbagala Rangi Tatu.

 

“Tunataka mradi huu uanze kutoa huduma kwa Watanzania hasa wakazi wa Dar es salaam, mradi huu utaongeza ufanisi wa usafiri wa umma katika jijini la Dar es Salaam na kutoa huduma ya kisasa, salama na ya haraka kwa wananchi.”

 

Kadhalika Mheshimiwa Majaliwa amemwagiza Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya utoaji huduma ya Usafiri ya Mofat Mohammad Kassim kuhakikisha anakamilisha haraka taratibu za utoaji wa mabasi 99 yaliyopo bandarini ili kuwezesha huduma hiyo kuanza kwa wakati.

 

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali  inataka kuona katika awamu ya pili ya mradi wa BRT, tiketi za usafiri kupitia mabasi hayo zinakuwa za kielektoniki badala ya tiketi za karatasi kama ilivyokuwa awali. “Tukifanya hivi itatusaidia kumonitor kiasi cha fedha kinachokusanywa.”

 

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa Watanzania kuchangamkia fursa za ajira zitakazotokana na mradi huo ikiwemo udereva. 

 

“Nendeni mkasome masuala ya udereva kupitia Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), mradi huu utahitaji idadi kubwa ya madereva wenye ujuzi”.

 

Akizungumza baada ya kukagua kituo cha kujazia gesi kwenye mabasi hayo kilichopo kwenye kituo kikuu cha Mbagala Rangi Tatu, Mheshimiwa Majaliwa ameiagiza kampuni ya Lake Oil inayotekeleza mradi huo kuhakikisha wanakamilisha usimikaji wa mitambo ili waanze kutoa huduma.

 

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu aliambana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi, Naibu Waziri Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Zainab Katimba, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi pamoja na watendaji wengine wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Wakala ya Mabasi Yaendayo Haraka (DART) na Chuo cha Taifa cha usafirishaji (NIT).

(mwisho)

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,                                

JUMATANO , AGOSTI 13, 2025


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.