Na Haji Nassor
TIMU za Unguja zimeendelea kuambulia bakora katika Ligi Kuu ya Zanzibar inayoendelea katika uwanja wa Gombani, baada ya juzi Mundu kuchezea kipigo cha mabao 3-1 mikononi mwa Jamhuri.
Licha ya wavuvi wa kijiji cha Nungwi kujitahidi kuwabana wenyeji wao, lakini walijikuta wakishindwa kuvuka mkondo na kulazimika kukubali matokeo hayo.
Jamhuri ilianza kuzisalimia nyavu katika dakika ya 20 kupitia kwa Ali Othman, kabla Bakari Khamis hajaiongezea timu hiyo bao la pili katika dakika ya 24, ambapo matokeo hayo yalidumu hadi mapumziko.
Iliichukua Jamhuri dakika kumi tangu kuanza kipindi cha pili kuandika goli la tatu, mara hii likiwekwa kimiani na Ali Othman tena.
Jitihada za Mundu kuambulia angalau goli la kufutia machozi zilizaa matunda mnamo dakika ya 70, pale Ibrahim Msanjiwa alipoachia shuti la mbali lililokwenda nyavuni moja kwa moja.
No comments:
Post a Comment