Habari za Punde

Iachieni ZFA Ifanye Kazi Zake Bila Bughudha - Waziri


Na Abdi Shamnah

WAZIRI wa Habari,Utamaduni,Utalii na Michezo, Said Ali Mbarouk amewataka wadau wa michezo nchini, kukipa nafasi Chama cha Soka Zanzibar (ZFA) kufanya shughuli zake bila bughdha, na kuonya kutowavumilia wale wanaolenga kukivuruga.

Akizungumza katika ufunguzi wa michuano ya soka Jimbo la Magogoni  ‘Jihad Cup’ inayoendelea katika kiwanja cha Welezo, Mbarouk amesema ni wajibu wa wadau wa soka nchini kukipa ushirikiano na kukiunga mkono Chama hicho katika juhudi zake za kukuza soka badala ya kulenga kukidhoofisha.


Alisema Wizara yake haitakuwa tayari kuona kunakuwepo watu wa aina hiyo kwani hawasaidii Serikali katika azma yake ya kuendeleza soka nchini, zaidi ya kuibua migogoro.

Mbarouk alisema tayari Uongozi wa Wizara yake, umekubaliana kwa dhati na BTMZ na ZFA kufanya kazi ya kuimarisha soka na kukiachia jukumu chama hicho la kuandaa mikakati ili Zanzibar iweze kupata mafanikio katika kipindi kifupi kijacho.

Alisema wadau wote wanakaribishwa kutoa mawazo yao wa mujibu wa sheria na kanuni za nchi na aliwataka waelewe kuwa vyombo hivyo vipo kwa mujibu wa Katiba.

Alivitaka vilabu vyote nchini kuviunga mkono vyombo hivyo, kwa kuzingatia umuhimu wa kuwepo mashirikiano kati ya wadau wote, kuanzia ngazi ya klabu hadi Serikali.

Akizungumzia uanzishwaji wa Jihad Cup, Waziri Mbarouk alimpongeza Mwakilishi wa Jimbo la Magogoni Abdillah Jihad kwa uamuzi wake wa kuanzisha michuano hiyo na kusema itakuza ushirikiano na kuibua vipaji vya soka jimboni humo.

Aliwataka washiriki wa michuano hiyo kuzingatia suala la nidhamu na kukubali matokeo ya mchezo, kwa kigezo kuwa michezo sio ugomvi.  
Akitilia umuhimu wa hilo, Waziri Mbarouk aliahidi kuitunuku shilingi 100,000/- timu yoyote itakayoibuka na ushindi wa nidhamu, wakati ambapo mshindi wa kwanza wa michauno hiyo kuahidi kumzawadia 250,000/- na mshindi wa pili shilingi 150,000/-.

Nae Makamu wa Rais ZFA, Al Haji Ameir , alisema michuano hiyo inafanyika kulingana na kalenda ya ZFA , inayoainisha kuwepo kwa mashindano ya majimbo, hivyo aliwataka wachezaji wanaoshiriki kujituma, kwa kigezo kuwa makocha wa ZFA wa U.15, U.17 na U.20 watafika kutafuta vipaji.

Jumla ya timu tisa zilizo katika makundi mawili zinashiriki katika michuano hiyo, ambazo ni Danger boys,Sayari FC, Grenada, Maisara FC na Supper Eagles.Nyengine ni University,New Africa,Taifa jipya na Eleven fighter.

Mshindi wa kwanza wa michuano hiyo atazawadi Kombe,Jezi seti moja,mipira mitatu na sh.150,000/ wakati mshindi wa pili ataondoka na jezi seti moja,mipira miwili na sh.100,000/ na mshindi wa tatu atapata jezi seti moja, mipira miwili na sh.50,000/.

Katika pambano la fungua dimba timu ya Maisara ilianza vizuri michuano hiyo kwa kuondoka na ushindi baada ya kuibamiza Grenada kwa bao 1-0.    

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.