Habari za Punde

Balozi Seif: Msitafsiri kur-ani kwa maslahi binafsi


Na Othman Khamis, OMPR
MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amewatahadharisha waumini wa dini ya kiislamu, wenye tabia kuitafsiri kur-ani kwa manufaa yao binafsi.

Alisema tabia hiyo ni mbaya na yenye kumchukiza Mwenyezi Mungu na kwamba wakati umefika kwa waislamu kuachana nayo tabia hiyo mara moja.

Balozi Seif alieleza hayo katika viwanja vya Chuo cha Kiislamu cha Al-Haramain jijini Dar es Salaam, kwenye kilele cha maadhimisho ya mashindano ya kuhifadhi kur-ani.

Balozi Seif aliutaka umma wa kiislamu kuhakikisha unaondosha mifarakano na kuwa wamoja katika kutekeleza maamuru ya Mwenyezi Mungu.

Balozi Seif Ali Iddi aliitaka jamii ya kiislamu kuhakikisha inawarithisha kwa kuwahifadhisha watoto wao kitabu kitukufu cha kur-ani, kwani ndio msingi utakaolijenga Taifa lenye watu wenye maadili.


Alisema endapo jamii ya kiislamu itajikita katika kuwarithisha na kuwahifadhisha kur-ani, Taifa litakuwa na vijana walioshiba kimaadili hali ambayo italisaidia Taifa kuepukana na matatizo mbali mbali yaliyopo hivi sasa.

Alisema kusoma na kuhifadhi kur-an ni wajibu wa kila muislamu ili ipatikane faida  ambayo imekusanya mahitaji ya viumbe vyote hapa duniani.

“Ndani ya kitabu hichi kuna mahitaji yetu yote ya kilimwengu na kesho akhera. Tutapataje mahitaji yetu yote bila ya kuifahamu kur-ani?”.  Alihoji Balozi Seif.    

Akizungumzia suala la mwezi mtukufu wa Ramadhani, Balozi Seif aliwaasa waumini wenye tabia ya kuswali kila ifikapo mwezi huo kuacha tabia hiyo inayokwenda kinyume na maamrisho ya dini.    
                        
Alisema si vyema kwa waumini kuchagua mwezi wa kufanya ibada kwani muumini anawajibika kusimamisha swala kila siku katika kipindi chote cha siku 365 za mwaka mzima pamoja na kufanya mambo yote ya kheri.        
                  
Balozi Seif aliipongeza kamati ya maandalizi ya mashindano hayo pamoja na wafadhili wote kwa juhudi za kufanikisha jambo hilo la kheri litakalowajengea hatma njema ya baadaye.                                                 

Awali akisoma risala Mwenyekiti wa kamati ya wanawake wa kiislamu Tanzania, Ukti Shamim Khan alisema lengo la mashindano hayo ni kuwatia moyo vijana kuipenda kur-ani ambayo itawasaidia kuongoka kwa kuelekea kwenye ucha Mungu. 

Ukti Shamim alielezea masikitiko yake kuona walimu wanaowaandaa Vijana hao kwa muda mrefu sasa wanasahauliwa, ambapo alisema kuwa kazi hiyo nzito kinyume na kuangaliwa kama walimu wengine wa skuli za kawaida zinazotoa elimu ya dunia. 

Akimkaribisha mgeni rasmi katika hafla hiyo Kaimu Mufti Mkuu wa Tanzania Sheikh Ali Muhidini, alisema kur-ani lazima ifanywe kuwa dira katika maisha ya kila siku ya muumini.

Sheikh Muhidini alisema ukosefu wa vijana wengi kutoelekezwa katika elimu ya dini kumesababisha utitiri wa watoto wa mitaani unaosababishwa na ukosefu wa malezi bora.      
 
Katika mashindano hayo zawadi mbali mbali zilitolewa ikiwa pamoja na Laptop Printer, televisheni, misahafu na fedha kwa washindi waliofungua akaunti ya Amana katika Benki ya Watu wa Zanzibar.
   
Mashindano hayo yamefadhiliwa na Benki ya Watu wa Zanzibar, Amana Benki pamoja na Rehema Foundatin inayofadhili wanafunzi katika vyuo mbali mbali ndani na nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.