Habari za Punde

Dk. Shein: Wakulima kurahisishiwa kulima, kuvuna


Na Rajab Mkasaba, IKULU
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amezindua uvunaji mpunga wa NERICA kwa kutumia ‘Combine Harvester’ mpya huko katika shamba la kilimo Bambi na kueleza kuwa hatua hiyo ina lengo la kuwakomboa na kuwarahisishia  wakulima namna ya kulima na kuvuna.

Dk. Shein alieleza kuwa serikali imechukua hatua hiyo ikiwa ni hatua ya kuleta mapinduzi ya kilimo hali ambayo itawasaidia wakulima katika kupunguza muda wao wa kazi na kuweza kulima na kuvuna kwa ufanisi zaidi.

Alisema kuwa mashine hizo za kuvuna zina uwezo wa kuvuna eka moja kwa dakika 45 zitasaidia kufanikiwa kwa mapinduzi ya kilimo huku akitoa agizo kwa wizara ya Kilimo na Maliasili kuongeza matrekta 20 mwakani hadi kufikia 54.

Alisema hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kwani pia mipango ya kuziongeza ‘Combine Haverstoe’ upo hadi kufikia 45 awamu kwa awamu.


Dk. Shein alisema serikali ina mipango ya kujikita zaidi kwenye kilimo cha mpunga cha umwagiliaji, huku zaidi ya heka 2000 zikitengwa kwa kilimo hicho Unguja na Pemba.

Alibainisha mambo makubwa matano ambayo serikali imefanya juhudi za makusudi katika kuwasaidia wakulima ikiwa ni pamoja na punguzo la asilimia 75 la bei ya mbegu, mbolea, dawa pamoja na kuongeza Mabibi Shamba na Mabwana Shamba na wataalamu.

Alieleza juhudi za kuiimarisha taasisi ya utafiti Kizimbani ambayo tayari wameshajitokeza wahisani kuiunga mkono ikiwemo serikali ya Norway na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Tanzania.

Dk. Shein alisema kuwa bonde la Cheju  litalimwa kwa kilimo cha umwagiliaji maji na kuepuka mitihani iliyotokea katika msimu uliopita ambapo serikali itatoa taarifa maalum kwa lengo la kuwatazama wakulima ambao mpunga wao umeharibika.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja ambaye Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Abdalla Mwinyi Khamis alisema kuwa hatua hiyo ya uzinduzi wa ‘Combine Havester’ mpya ni miongoni mwa ahadi alizozitoa Dk. Shein kwa wakulima.
 
Alisema kuwa Dk. Shein amekuwa bingwa wa kutimiza ahadi zake ikiwemo hiyo ya mashine hizo pamoja na nyengine kadhaa ambazo hivi sasa zinaendelea na nyengine tayari zimeshatekelezwa ikiwemo miradi mbali mbali ya maendeleo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Affan Othman Maalim alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuwatimizia ahadi aliyoahidi Mei 23 mwaka jana kuwa atahakikisha wanavuna kwa kutumia vifaa hivyo.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa katika mapinduzi ya kilimo, serikali imedhamiria katika kuwasaidia wakulima wake kilimo cha uhakikika ikiwa ni pamoja na pembejeo, mbolea, mbegu, dawa za kuulia magugu na utaalamu.

Pamoja na hayo, Katibu Mkuu huyo alitoa maelezo juu ya jitihada kubwa zilizofanywa na mafundi wa matrekta katika kuziunga ‘Combine harvester’ hizo mpya kwa kushirikiana na wataalamu kutoka China ambako ndiko zilikonunuliwa  kazi ambayo waliifanya kwa muda wa siku mbili tu.

Alisema kuwa wataalamu hao kutoka China walitoa pongezi za pekee kwa mafundi hao kutokana na uweledi wao mkubwa na kusema kuwa hawajawahi kwenda nchi hata moja na kukuta utaalamu kama waliokuta kutoka kwa mafundi hao wazoefu na wenye ujuzi mkubwa.

Aidha Katibu Mkuu huyo aliwasilisha ombi la mafundi hao kwa Dk. Shein.
 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.