Habari za Punde

NGO zisizofuata sheria kufutwa


Na Mwashamba Juma
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itazifutia usajili Jumuiya zote za kiraia zinazokwenda kinyume na sheria na katiba ya nchi.

Mrajis Mkuu wa serikali Abdulla Waziri, alisema hayo huko ofisini kwake Forodhani katika hafla fupi ya kuwakabidhi hati ya usajili Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria Zanzibar “Paralegal.”

Mrajis huyo alisema lazima sheria ifanye kazi, ili kuziwajibisha Jumuiya zote ambazo zinavunya shria za nchi na kwenda kinyume na katiba zao katika ufanisi wa malengo yake. 

“Hatuwezi kuwa na Jumuiya nyingi za kiraia ambazo zinakwenda kinyume na sheria, licha yakuwa zimesajiliwa kisheria”, alisema Mrajis huyo  wa serikali.


Alisema watafanya uchambuzi dhidi ya Jumuiya zote za kiraia ambazo haziwajibiki katika kuwasilisha ripoti zao za kila mwaka kwenye ofisi yake na kuziwajibisha.

Alizitaka jumuiya hizo kuwajibika katika kutekeleza majukumu yao kwa wanachama wao na walengwa wao, sambamba na kuachana na tabia yakujiona kuwa wako juu ya sheria kwa kutowajibika kisheria.

Alisema uwajibikaji na utekelezaji wa majukumu kwa Jumuiya hizo ni hatua moja wa kufikia malengo waliyoyakusudia, hivyo alizitaka jumuiya hizo kuondokana na dhana ya kutegemea wafadili na badala yake wawajibike kwa wanachama wao  ili maendeleo yao yatokane na bidii zao.

Mrajis huyo alisema kukabidhiwa kwa hati ya usajili kwa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria imekuja kufuatia kukamilisha mashari ya usajili, na kuwa jumuiya halali yenye katiba.

Aidha alizitaka Jumuiya za kiraia kuwasilisha ripoti zao za kila mwaka ili kuisaidia serikali kuweza kutathmini kwa kiasi gani jumuiya hizo zinatoa mchango kwa jamii, pamoja na kuitaka Jumuiya ya wasaidizi wa sheria kuwa mfano mzuri katika uwajibikaji wa majukumu yake hasa katika ufanisi wa kazi zake.

Nae Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Ramadhan Khalfan Khamis alisema lengo la kuanzishwa kwa Jumuiya hiyo ni kutokana na uhaba wa wanasheria nchini ambao hawamudu kuwafikia wananchi wote kwa kutoa msaada wa sheria.

Aidha Ramadhan alisema kuwepo kwa wasaidizi wa sheria kutawasaidia wananchi kuwashauri kisheria, pamoja na kuwa nao karibu kwa kuwapa msaada wa sheria.

Hata hivyo Mwenyekiti huyo aliiomba ofisi ya mrajisi mkuu wa serikali kuwa karibu zaidi za Jumuiya za kiraia  kwa lengo la kufuatilia kwa karibu zaidi utendaji wao.

Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria Paralegal imesajiliwa chini ya sheria ya Jumuiya za kiraia, sheria namba 6 ya mwaka 1995 sheria za Zanzibar.

Kwa sasa Jumuiya hiyo ina wanachama 65 kwa Unguja na Pemba na wanachama wengine zaidi ya wanachama 30 wako masomoni kukamilisha mafunzo ya wasaidizi sheria Paralegal.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.