Habari za Punde

120 m/- zahitajika kumalizia jengo la mitihani Uweleni



Na Haji Nassor, Pemba
ZAIDI ya shilingi 120 milioni, zinahitajika kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa jengo maalum la kufanyia mitihani la ghorofa moja na vyumba vitano vya madarasa katika skuli ya sekondari ya Uweleni Mkoani Pemba.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Mwalimu anaeshughulikia majenzi skulini hapo, Mohamed Ussi Shaame alisema kwa sasa wameshatumia shilingi 22 milioni, kwa ajili ya msingi.

Alisema kati fedha hizo walizotumia, shilingi 3.5 milioni ambapo ilikuwa ni saruji paketi 200, walipewa msaada na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), miezi michache iliopita.

Ussi alieleza, fedha nyengine walizotumia hadi kufikia hatua hiyo ya msingi, ni shilingi milioni 2, kwa hatua ya wali kutoka mfuko wa Maendeleo ya Jimbo na baadae shilingi 8 milioni.


Aidha alisema, hata Mwalikishi wa jimbo la Mkoani, Abdalla Mohamed Ali, amechangia shilingi 500,000 katika ujenzi huo unaoendelea skulini hapo.

Mwalimu huyo anaesimamia majenzi, alifahamisha kuwa, fedha zote hizo hawakukabidhiwa taslimu, bali ni vifaa mbali mbali kama vile kokoto, mawe, nondo na mchanga.

Hata hivyo, alisema waalimu, wazazi na wanafunzi, nao hawako nyuma katika kuendeleza ujenzi wa jengo hilo, ambalo ni agizo la Wizara ya Elimu la kila skuli kuwa na kumbi maalum za kufanyia mitihani.
Alifafanua, kila mwalimu kwa hiari yake kila mwisho wa mwezi wamewakua wakichangia shilingi 1,500 pamoja na michango ya miradi midogo midogo ya skuli.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa skuli hiyo,  Shehe Hassan aliwaomba wale wote waliosoma skulini hapo, kuaona umuhimu wa  kuchangia ujenzi huo, ili umalizike kwa wakati.

Akizungumzia mikakati ya kuzipata fedha hizo wanazozihitaji,Mwalimu huyo alisema ni pamoja na kusaka wafadhili wa nje.

Mkakati mwengine, ni kuwatafuta wafadhili wa ndani ikiwa ni pamoja na Wabunge, Wawakilishi na wafanyabiashara wenye nia kusaidia pamoja na kufikisha kilio chao serikali kuu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.