Habari za Punde

Wanafunzi chuo cha ufundi Kengeja walala mskitini


Na Radhia Abdalla, Pemba
JUMLA ya wanafunzi 104 wa Chuo cha Ufundi Kengeja Wilaya ya Mkoani Pemba,hulazimika kulala katika nyumba za walimu,msikitini na madarasani kufuatia uhaba wa mabweni unaokikabili  chuo hicho.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi chuoni hapo, Kaimu Mwalimu Mkuu wa chuo hicho,  Rashid Ali Said alisema ni wanafunzi 56 tu pekee, ndio wanaolala  kwenye mabweni chuoni hapo.

Alisema chuo hicho kina jumla ya wanafunzi 160,  ambao kati yao,ni wanafunzi 56 wa kike ndio wanaolala kwenye bweni wakati waliobakia wakiendelea kulala katika mazingira yasiyo rasmi.


Alifahamisha kuwa hali hiyo inatokana na uhaba mkubwa wa mabweni jambo ambalo huwakosesha utulivu wa masomo hususani kwa wanafunzi wa kiume.

“Kwa kweli uhaba wa mabweni katika chuo hichi ni changamoto kubwa, ambayo inatukabili na inahitaji kutatuliwa haraka,’’ alieleza Kaimu Mwalimu Mkuu huyo.
Akizungumzia kuhusu uhaba wa walimu pamoja na vifaa vya kufundishia, tatizo hilo ni kubwa na  kwa kiasi kikubwa linachangia kuanguka kwa ufaulu wa masomo kwa wanafunzi.

Alisema chuo hicho ni kimojawapo ambacho  kinaingiza wanafunzi wenye vipaji maalum, lakini  imeonekana  vipaji vya wanafunzi hao hudumaa kutokana na ukosefu wa vifaa vya kufundishia na walimu.

Alisema suala la walimu ni muhimu katika chuo hicho ambacho ndio chachu ya maendeleo ya taifa  kwani kuna mafunzo ya aina mbali mbali yanayotolewa ikiwa ni pamoja na ufundi.

Alisema kukosekana kwa waalimu wa kutosha ni miongoni mwa changamoto kubwa inayopelekea wanafunzi  kutofanya vizuri katika mitihani yao ya taifa, hasa miaka ya hivi karibuni tofauti na  mwanzoni mwa kuanzishwa kwa chuo hicho.

Aliwataja walimu wa masomo hasa ya ufundi ndio ambao kwa sasa wamekuwa tatizo kubwa jambo ambalo linatishia matokeo mabaya kwa wanafunzi.

Mwanafunzi Mariam Salim wa (kidato cha sita) chuoni hapo ameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuwapatia vifaa vya ufundi ili kukabiliana na changamoto iliyopo.

Chuo cha ufundi Kengeja ni miongoni mwa vyuo vikongwe hapa Zanzibar ambacho kwa muda mrefu sasa kinaendelea kukabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na uhaba wa walimu, vitendea kazi na uhaba wa mabweni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.