Habari za Punde

Wauza gongo waandamana kwa DC




Joseph Ngilisho,Manyara
WANAWAKE wafanyabiashara wa pombe za kienyeji Wilayani Hanang  Mkoani Manyara,wameandamana hadi kwa Mkuu wa Wilaya hiyo wakimuomba aondoe amri ya kupiga marufuku kutengeneza pombe kwa kutumia nafaka.

Wanawake hao zaidi ya 300 waliandamana jana hadi kwa mkuu wa wilaya hiyo, Christina Mndeme,wakidai kuwa amri hiyo imewaathiri kwani wanaitegemea biashara hiyo kwa ajili ya kuendesha maisha yao ikiwemo kuwasomesha watoto wao.

Wakizungumza mbele ya Mkuu wa wilaya, wanawake hao walidai kuwa hivi sasa maisha yao yamekuwa magumu kwani wanategemea biashara hiyo kwa ajili ya kuendeshea maisha yao hivyo wanaomba waendelee nayo.

“Mkuu hivi sasa maisha yetu yamekuwa magumu, tunaomba tuendelee na biashara hii kwani wengine tunaitegemea kwa ajili ya kusomesha watoto wetu wanaoingia kidato cha kwanza,” walisema wanawake hao.


Walimuomba Mkuu huyo wa wilaya waendeleze biashara hiyo kwa muda wakati huu ambao wanawapeleka watoto wao shule,halafu wataachana na biashara hiyo pindi hali ya chakula itakapokuwa nzuri kwenye wilaya hiyo.

Hata hivyo,Mkuu huyo wa wilaya aliwapokea wanawake hao na kuwataka wabuni vyanzo vingine vya biashara ili waweze kujiingizia kipato kuliko kutegemea biashara hiyo ya kutengeneza pombe kwa kutumia nafaka.

“Hivi sasa sehemu kubwa ya wilaya yetu ina upungufu mkubwa wa chakula hivyo siyo vizuri tukatumia mtama au mahindi kidogo tuliyonayo kwa ajili ya kutengeneza pombe za kienyeji, kisha tuwe na njaa,” alisema.

Alisema agizo lake la kupiga marufuku utengenezaji wa pombe za kienyeji kwa kutumia nafaka litaendelea wilayani humo,kwani ameshawaagiza viongozi wote wahakikishe nafaka haitumiki kutengenezea pombe za kienyeji.




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.