Habari za Punde

Vitambulisho vya taifa kutumika uchanguzi mkuu 2015. ikwete awataka watendaji NIDA kuwa waadilifu


Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
RAIS wa Tanzania, Dk. Jakaya Mirisho Kikwete ameiagiza Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kuhakikisha wananchi wanapata vitambulisho kabla ya mwaka 2015 kwa sababu uchaguzi mkuu ujao watu watatumia vitambulisho vya taifa kupiga kura.

Dk.Kikwete aliyasema hayo jana wakati wa uzinduzi wa mfumo wa usajili na utambuzi wa watu na utoaji vitambulisho katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam.

Aliwataka watendaji wa Mamlaka hiyo kuwa waadilifu na wazalendo wa kweli ili kila muombaji wa kitambulisho apate kile anachostahiki kupata.

Epukeni makosa ya kumpa kitambulisho asiestahiki kuweni macho na watu wa aina hiyo,” alitahadharisha Rais Kikwete.

Alisema serikali haitaki kuona matatizo inayoyapata katika utoaji wa hati za kusafiria (paspoti) yanajitokeza katika utoaji wa vitambulisho vya taifa kwa sababu paspoti za Tanzania zimekuwa zikikamatwa mara kwa mara zikiwa mikononi mwa watu wasiohusika.

“Kwa sababu kule kwenye paspoti watu wasiohusika wanapatiwa paspoti kwa sababu watu wanatoa kitu chochote,” alisema Rais Kikwete, akiwa na maana ya rushwa.


Hata hivyo, alionya kuwa serikali haitakuwa na msalia mtume na mtumishi yoyote wa NIDA atakaekamatwa akitoa kitambulisho kwa mtu asiestahiki na kusisitiza kuwa kutoa kitambulisho kwa mtu asiehusika ni kosa kubwa la jinai.

Aidha aliwataka Watanzania kuacha kutoa taarifa za uongo kwa sababu kufanya hivyo ni kosa huku akiwataka viongozi wa dini, asasi za kiraia na waandishi wa habari kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa vitambuliso hivyo.

Aidha alisisitiza haja kwa wananchi kushirikiana kwa pamoja na serikali na wasivutane kama ilivyotokea katika matukio yaliyopita ya kitaifa.

Alisema kufanikiwa zoezi hilo kunahitimisha ndoto ya miaka mingi waliyokuwa nayo wa Tanzania ya kupata utambulisho wao.

Alisema serikali inapowatambua wananchi wake popote walipo duniani inakuwa rahisi kuwahudumia na kuongeza kuwa suala la serikali kuwajua watu wake sio jambo la hiari tena.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, alisema hatimae Watanzania nao wameungana na nchi nyengine za Afrika Mashariki kupata utambulisho wao.

Alisema lengo la NIDA ni kuhakikisha linatoa vitambulisho kwa Watanzania wote waliofikisha umri wa kuanzia miaka 18, wageni wanaoishi nchini pamoja na wakimbizi.

Alisema vitambulisho hivyo vitarahisisha ufanyaji kazi wa taasisi nyengine kama RITA, Ofisi ya Mrajisi wa vizazi na vifo Zanzibar, Idara ya Uhamiaji, polisi na taasisi nyengine, lakini pia vitasaidia kujenga utawala bora wa kimamlaka.

Aidha alisema itaisaidia serikali kufahamu raia wake walipo, anafanya nini na anamiliki kitu gani pamoja na kurahisisha utambuzi wa watu.

Vitambulisho hivyo vimetengenezwa kwa teknolojia ya kisasa ya smart card na havitaweza kughushiwa.

Viongozi kadhaa walikabidhiwa vitambulisho vyao katika hafla hiyo akiwemo mwenyewe Rais Kikwete, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, Rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Amani Karume na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa.

Wengine ni  Rais mstaafu wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi, Mama Fatma Karume, Mama Salma Kikwete, Mawaziri wakuu wastaafu, Dk. Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Warioba, mke wa Waziri mkuu mstaafu wa awamu ya tatu, Esta Sumaye, Anna Mkapa, mwanasiasa mkongwe Kingunge Kumbale Mwiru, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na viongozi wengine na wawakilishi kutoka mikoa mbali mbali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.