Habari za Punde

Dk. Shein:Kuweni majasiri kuripoti unyanyasaji. Ushirikiano, uwajibikaji ndio silaha ya udhalilishaji


Na Khamis Amani
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, imewataka wananchi kuwa na ujasiri wa kuviripoti vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia, ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Serikali imefahamisha kuwa, vitendo vya aina hiyo havitoi taswira nzuri katika utamaduni na ustaarabu wa nchi, hivyo wananchi wanapaswa kubadilika, kuachana na muhali na badala yake wafuate sheria ili kukabaliana na vitendo hivyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, aliyasema hayo bustani ya Victoria Vuga Mjini Zanzibar jana, katika maadhimisho ya siku ya sheria Zanzibar.

Katika maadhimisho hayo yaliyobeba ujumbe wa 'Kutokomeza unyanyasaji wa kijinsia', Dk. Shein alisema, kwa mujibu wa taarifa na takwimu zilizopo suala  la unyanyasaji wa kijinsia limekua ni tatizo linaloendelea kuongezeka katika jamii, licha ya jitihada mbali mbali za kulikemea na kulipiga vita zinazochukuliwa na serikali na washirika wengine.


Hata hivyo, Dk. Shein alifahamisha kuwa, jamii  haipaswi kukata tamaa kwani hatua zilizochukuliwa zinatia moyo katika kulishughulikia na ni wajibu wa jamii kuendelea kuongeza jitihada ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu.

"Nawasihi wananchi wasikubali kurubuniwa na yeyote yule kwa ajili ya kuwaficha watenda maovu haya, tukumbuke kuwa kuwaficha watu wa aina hii kunahatarisha maisha ya watu wanaoishi karibu nao au jamii yote kwa ujumla," alitanabahisha Dk. Shein.

Alisema katika tafiti zilizofanywa na taasisi mbali mbali za kimataifa zimethibitisha kuwa, tatizo la unyanyasaji wa kijinsia ni tatizo lililoenea duniani kote ambapo waathirika wake wakubwa ni wanawake na watoto.

Alisema Zanzibar ikiwa ni sehemu ya dunia, ni dhahiri inakabiliwa na kazi kubwa ya kupambana na tatizo hilo, ambalo litakuwa kubwa zaidi ikiwa kutakosekana ushirikiano katika kukabiliana nalo.

Katika kukabiliana nalo, Dk. Shein aliwataka wananchi kuwa na imani na taasisi zao na kuweza kujitokeza bila ya woga katika kutoa maelezo yatakayosaidia kupatikana kwa ithibati itakayosaidia kupata ukweli, ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Kwa upande wa serikali, Dk. Shein alisema imechukua hatua mbali mbali za kuvizuwia vitendo hivyo ikiwemo kuimarisha ustawi wa haki za watoto na wanawake nchini, ikiwa ni pamoja na kutunga sheria ya hifadhi ya mtoto nambari 6/2011, kwa lengo la kuzipa nguvu sheria zinazolinda haki zao hivi sasa na zile zilizokuwepo kabla.

Aidha alisema serikali imeweka mipango maalumu ya kuwasaidia wanawake na watoto, na kupitia Wizara ya Ustawi wa Jamii, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto pamoja na Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika.

Alisema serikali imeanzisha vituo maalumu vya kushughulikia vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia na kutoa ushauri nasaha katika hospitali ya Mnazimmoja, Chake Chake, hospitali ya Cottage Kivunge na Makunduchi.

Hivyo alitoa wito kwa wananchi kuzitumia huduma za vituo hivyo vinavyojulikana kama vituo vya mkono kwa mkono, ambavyo vina wataalamu wa kushughulikia kesi za aina hiyo wakiwemo madaktari, polisi, wanasheria na watoa ushauri nasaha.

Alisema umefika wakati kwa vyombo vya sheria ikiwemo mahakama, waendeshaji mashitaka, polisi na wananchi kwa ujumla kuwa pamoja na kujenga ushirikiano ulio imara zaidi kwa lengo la kutokomeza unyanyasaji wa kijinsia.

Mapema Dk. Shein alizindua jarida la mahakama na kuipongeza mahakama kwa juhudi zake za kutoa elimu ya sheria kwa wananchi mbali mbali wa Unguja na Pemba, ambalo litaweza kusaidia kueneza taaluma ya sheria kwa wananchi.

Mapema Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu alisema vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia hasa ulawiti na ubakaji wa watoto wadogo vimekithiri kwa kiasi kikubwa nchini.

Alisema hilo linathibitishwa na takwimu za miaka mitatu kutokea mwaka 2009 ambapo kesi 38 zilifunguliwa mahakamani, kesi 50 zilifunguliwa mwaka 2010 na mwaka jana 2012 zilifunguliwa kesi 77, ambapo asilimia tatu tu ya kesi hizo washitakiwa wake waliadhibiwa na asilimia 97 wameachiwa.

Alisema hali hiyo haitii moyo kabisa na inawakatisha tamaa wananchi juu ya udhaifu wa uendeshaji wa kesi hizo, na kuwaomba majaji na mahakimu kumuweka Mwenyezi Mungu mbele wakati wa kuhukumu kesi za aina hiyo na nyenginezo, kwani mwisho wa siku wataulizwa juu ya hukumu walizozitoa.

Nae Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar, Awadh Ali Said alisema athari za matendo ya unyanyasaji wa kijinsia haziishii kwa matokeo yaliyo dhahiri ya kimwili na kiheshima tu, bali pia huambatana na athari za muda mrefu za kisaikolojia ambazo huwa jinamizi linalomuandama muathirika na hata familia yake daima.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mashitaka Zanzibar (DPP), Ibrahim Mzee Ibrahim alisema utokomezaji wa unyanyasaji wa kijinsia ni lazima uanzie kwenye malezi yanayopatikana kwenye familia, ambazo ndio chuo kikuu cha malezi na maadili katika jamii yoyote, na kufahamisha kuwa familia zikiharibika na jamii nayo huharibika.

Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Massoud kupitia hotuba yake aliyosomwa na Mwanasheria wa ofisi yake, Hamisa Mmanga amezishauri taasisi zinazohusika kusimamia kikamilifu sheria za nchi ili kutokomeza unyanyasaji wa kijinsia unaoongezeka siku hadi siku.

Maadhimisho ya siku ya sheria Zanzibar yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa serikali, Majaji wa Mahakama Kuu, Mahakimu, Makadhi wa mahakama za Kadhi, Waendesha Mashitaka, Mawakili wa kujitegemea na wadau wa sheria.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.