Habari za Punde

Zanzibar, Oman zazindua mradi ufadhili elimu ya juu


Na Mwashamba Juma
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Oman jana zilizindua mradi wa Ushirikiano wa Elimu ya juu wa Sultan Qaboos (SQAF) kupitia njia ya mtandao.

Mradi huo unaojumuisha udhamini wa masomo ya juu, uliozinduliwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ali Juma Shamuhuna akishirikiana na Waziri wa Elimu ya Juu wa Oman, Dk. Rawya Saud Al- Busaid utaaza mapema mwaka wa masomo 2013-2014.

Akizungumza na waandishi wa habari, Waziri Shamuhuna alisema Zanzibar itahakikisha mradi huo unafika mbali kama ilivyokusudiwa na serikali mbili hizi, na kusema kuwa kuzinduliwa kwa Mradi SQAF kunaimarisha urafiki uliopo baina ya Zanzibar na Oman.

Aidha aliishukuru serikali ya Oman kwa kukichagua Chuo Kikuu Cha Zanzibar (SUZA) katika kutekeleza mradi wake huo na kuongeza kuwa Zanzibar inaelewa umuhimu wa elimu katika viwango vyote.


Kwa upande wake Waziri wa Elimu wa Oman, Dk. Busaid alisema mradi SQAF ni muhimu katika kuendeleza maendeleo ya kiuchumi na jamii pamoja na kukuza tamaduni za nchi mbili hizo.

Dk. Rawya alisema kuzinduliwa kwa mradi huo kutaboresha mahusiano mema hasa katika nyanja ya elimu baina ya Oman na Zanzibar, sambamba na kurudisha historia ya nyuma baina ya nchi mbili hizi kwa kuendeleza ushirikiano wao wa wa kindugu uliodumu kwa muda mrefu.

Aidha alisema mradi pia utachangia kukuza maendeleo ya SUZA na kuzidisha thamani kubwa ya chuo hicho.

Mfuko wa elimu ya juu wa Sultan Qaboos (SQAF) unatarajiwa pia kutoa taaluma kwa ngazi ya shahada ya kwanza, shahada ya pili na  shahada ya uzamivu (PhD) katika fani za elimu, afya, mazingira, miundombinu na ujasiriamali.

Hata hivyo, Dk. Rawya alisema mbali na Zanzibar kunufaika na mradi wa (SQAF) pia mradio huo umezishirikisha nchi 10 kutoka bara la Amerika, Ulaya, Asia na Afrika zikiwemo Marekani, Uingereza, Poland,  Malta, Uholanzi, Ujerumani, Australia, Finland, Malaysia na Afrika Kusini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.