Habari za Punde

Watoto 1,500 kurejeshwa skuli




Na Husna Mohammed
WATOTO 1,500  kutoka Unguja na Pemba walioacha masomo na kujishughulisha na ajira mbaya wanatarajiwa kurejeshwa skuli mapema mwezi ujao.
Kati ya watoto hao wamo wengine walio katika hatari ya kuacha skuli ambao wamekuwa wakitoroka mara kwa mara na kujishughulisha na ajira kwa ajili ya kuipatia kipato cha kujiendesha  familia zao.
Ofisa wa mradi wa Save the Childreen, Hashim Pondeza, alisema hayo jana katika kituo cha Elimu Mbadala Rahaleo mjini hapa, katika mafunzo ya waandishi wa habari juu ya kuelimisha jamii dhidi ya madhara ya ajira mbaya kwa watoto.
Ofisa huyo alisema kufuatia utafiti uliofanywa na taasisi mbalimbali zinazotekeleza mradi wa Save the Childreen umebaini kuwa kati ya watoto hao 1,500 wanaume ni 984 na 516 ni wanawake.

Aliyataja maeneo ambayo watoto hao wanatoka kuwa ni Micheweni na Majenzi katika Wilaya ya Micheweni, Kiuyu Minungwini na Kangagani Wilaya ya Wete  ambapo jumla ya watoto 582 wamekwamuliwa katika ajira mbaya baada ya utafiti uliofanywa na Jumuiya ya Pemba Island Releef Organization (PIRO).
Aidha alisema katika Mkoa wa Kusini Pemba, imeweza kuwanasua watoto 500 katika vijiji vya Ndagoni, Wesha, Vitongoji, Uwandani kufuatia   utafiti uliofanywa na jumuiya ya Kupunguza Umasikini na kukuza Hali ya Uchumi (KUKAHAWA).
 Akizungumzia kwa upande wa kisiwa cha Unguja, Pondeza alisema jumuiya COWPS na Chama cha Waandishi wa Habari wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA), ambao walifanya utafiti katika Mikoa ya Kusini na Kaskazini, alisema watoto 320 kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja kwenye vijiji vya Mkokotoni, Nungwi, Pwani Mchangani na Kijini Matemwe wameweza kugundulikana kuacha masomo.
“Watoto hawa wote tumeweza kuwanasua na ajira mbaya ambapo wameacha masomo na wengine wako katika hatari ya kuacha masomo tutawasaidia kwa sare za skuli na baadhi ya vifaa vya masomo ili waendelee na masomo yao, zoezi ambalo litanza mapema mwezi ujao,” alisema.
Alisema pamoja na mambo mengine, mradi huo pia utasaidia familia zenye mazingira magumu kwa ajili ya kuwapa mitaji ili waweze kusaidia familia zao badala ya kutegemea watoto wao.
Naye Ofisa kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali katika Idara ya Elimu Mbadala na  watu wazima, Halima Tawakali , alisema lengo la wizara ya elimu ni kuhakikisha kuwa watoto wote wanapata elimu.
Alisema taratibu zote za kuwarejesha watoto hao maskulini zimeshakamilika ikiwa ni pamoja na kuzungumza na walimu wa skuli husika kuwapokea na kuwapa mashirikiano.
Aidha alisema pamoja na hayo lakini pia Wizara imeandaa mpango wa kuwaelewesha wanafunzi kwa kuwapa ushauri nasaha sambamba na kuandaa fomu za kufuatilia maendeleo ya ufahamu na elimu kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.