HOTUBA YA MAONI YA
KAMATI YA MAENDELEO YA WANAWAKE NA USTAWI WA JAMII KUHUSIANA NA MAKADIRIO YA
MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA AMALI KWA MWAKA WA FEDHA
2013/2014.
Mheshimiwa Spika
Kila sifa njema zinamstahikia Mwenyezi Mungu
aliyetujaalia afya na uzima, tukaweza kuendelea na majukumu yetu ya kila siku
na kuniwezesha kusimama mbele za Baraza lako tukufu kuwasilisha maoni ya Kamati
ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa Jamii kwa bajeti ya Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Amali kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Mheshimiwa Spika
Napenda kukushukuru kwa dhati kunipa fursa hii
adhimu ya kuwasilisha maoni ya Kamati ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa
Jamii. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja watendaji wake wote wa Wizara
kwa mashirikiano yao katika kipindi chote cha kazi za Kamati.
Mheshimiwa Spika
Kamati ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa Jamii
imekuwa ikifanya kazi zake na Wizara kwa mashirikiano makubwa. Kamati ilipitia
Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa umakini na kuishauri Wizara
na Serikali kikamilifu.
Mheshimiwa Spika
Baada ya utangulizi, naomba kuanza kutoa maoni ya
Kamati katika Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kuangalia
utekelezaji wa Wizara katika Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Elimu, Idara zake mbali
mbali na sehemu nyingine ambazo Kamati zimeona kuna umuhimu mkubwa wa kuzitolea
maoni yake.
Mheshimiwa Spika
Ofisi ya Mkaguzi Mkuu
wa Elimu
Ofisi ya Mkaguzi Mkuu
wa Elimu ni chombo
muhimu ambacho kina jukumu la kuzikagua skuli zote za Serikali na Binafsi ili
kuhakikisha kuwa elimu bora inatolewa kwa mujibu wa mitaala na mihutasari
inayokubaliwa na Wizara.
Mheshimiwa Spika
Ubora na mafanikio ya elimu yanategemea sana
utendaji nzuri wa Ofisi hii. Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na
ongezeko kubwa la matokeo mabaya ya mitihani kwa wanafunzi wa Zanzibar katika
ngazi tofauti hasa hasa ya kidato cha nne. Kamati haifurahishwi na matokeo hayo
kwa vile yanatoa taswira kuwa katika muda mfupi ujao nchi yetu itakosa
wataalamu mbali mbali, kutokana na wanafunzi wetu wengi kushindwa kufanya
vizuri hali inayopelekea wengi wao kushindwa kuendelea na masomo katika ngazi
za juu.
Mheshimiwa Spika
Kamati yetu imesikitishwa sana na hali mbaya ya
Ofisi za ukaguzi kwa upande wa Unguja na Pemba, kwani majengo hayaridhishi na
ni machakavu, finyu na yamekosa rasilimali za kutosha kama vitendea kazi na
fedha katika kutekeleza majukumu yao mbali mbali. Mheshimiwa Spika, Wafanyakazi wa ofisi hii ni kama waliotelekezwa
katika mazingira yasiyoridhisha na ule umuhimu wa kazi wanazozifanya haulingani
na mazingira waliyopo. Hivyo, Kamati inashauri kuboreshwa kwa Ofisi ya Mkaguzi
Mkuu wa Elimu Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika
Kamati inaishauri Serikali kuipa umuhimu Ofisi hii
kwa kuipatia fedha za ruzuku kwa kiwango cha kutosha. Ofisi imekuwa inaongezewa
fedha kupitia bajeti ya wizara kwa miaka mitatu mfululizo ambapo bajeti ya
mwaka wa fedha 2011/2012 iliingiziwa shilingi za kitanzania milioni thamanini
(80,000,000), mwaka wa fedha 2012/2013 zilingizwa milioni tisini (90,000,000)
na katika mwaka huu wa fedha ruzuku kwa ajili ya uendeshaji zinatarajiwa
kuingizwa jumla ya shilingi milioni mia moja na sita (106,000,000). Ongezeko
hilo ni faraja kwa Ofisi hii lakini jee ongezeko hilo linaenda sambamba na
mahitaji au majukumu ya Ofisi?
Mheshimiwa Spika
Aidha, Kamati inaishauri Wizara kuharakisha matayarisho
ya Rasimu ya Uanzishwaji wa Sheria ya Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Elimu ili kuipa
uwezo wa kisheria ofisi hiyo na hatimaye kupata uwezo mkubwa wa kuyafanyia kazi
yale mapungufu wanayoyatoa wakaguzi wetu wa elimu katika maskuli.
Mheshimiwa Spika
Bodi ya Huduma za
Maktaba
Bodi ina
jukumu la kuhakikisha kuwa inatoa na kuendeleza huduma za maktaba visiwani
Unguja na Pemba. Kamati inaipongeza Bodi kupitia Shirika la Huduma za Maktaba kuimarisha
huduma za Maktaba Unguja na kupelekea kuongeza idadi kubwa ya watumiaji wa
maktaba hasa baada ya kufunguliwa kwa jengo jipya la Maktaba kuu lilioko
Maisara. Hata hivyo bado kuna upungufu wa vitabu vya fani mbali mbali ikiwemo
ya sayansi na Kamati inaiagiza uongozi wa maktaba na wizara kuongeza bidii ya
kupata vitabu hivyo.
Mheshimiwa Spika
Kamati ina masikitiko makubwa kwa upande wa Pemba,
maktaba iliyopo Chake chake ndio maktaba pekee inayotegemewa kwa Pemba mzima na
kumekuwa na msongamano mkubwa katika maktaba hiyo kutokana na ufinyu wa nafasi
hali inayopelekea kutokuwepo kwa huduma bora kwa watumiaji wa maktaba hiyo.
Mheshimiwa Spika, pamoja na hali hiyo Wizara kwa upande wa Pemba imejitahidi kupeleka vitabu katika
skuli zilizopo vijijini. Kamati yetu inapongeza sana jitihada za Wizara kuweza
kupeleka vitabu katika skuli zilizopo vijijini kwa kutumia mpango wa visanduku,
mpango huo umesaidia kuwajenga wanafunzi kuwa na tabia ya kupenda kujisomea na
Kamati inashauri mpango huo uendelezwe na kuweza kufikishwa katika vijiji mbali
mbali.
Mheshimiwa Spika
Kamati inaitaka Serikali kuzingatia na kuipa
umuhimu ujenzi wa tawi la maktaba pemba na kuhakikisha kuwa inaitilia Wizara, fedha za
kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Upanuzi na Uimarishaji wa Huduma za
Maktaba. Mradi utekelezaji wake ulianza tangu mwaka wa fedha 2010/2011 na hadi
sasa umekuwa unasuasua. Kamati yetu
ina hamu kubwa ya kuona ujenzi wa maktaba Pemba unafanyika kupitia mradi huo.
Mheshimiwa Spika Kamati imebaini kuwa skuli nyingi Pemba zimekosa
huduma za maktaba, ambapo kwa sasa ni skuli tano mpya na tatu kongwe zina
huduma hiyo. Kamati inaishauri Wizara kufanya mpango wa kuanzisha maktaba kwa
kila wilaya ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za maktaba kwa wananchi wa
kisiwa hicho.
Idara ya Elimu ya
Maandalizi na Msingi.
Tunaipongeza Serikali yetu kwa kuona umuhimu
mkubwa wa kuweka elimu ya maandalizi kuwa elimu rasmi katika mfumo wetu wa
elimu Zanzibar na kwa kuzingatia kuwa, elimu ya maandalizi ndio msingi wa
kumjenga mtoto kwa ajili ya elimu ya awali.
Mheshimiwa Spika, bado hakuna chuo kinachowaendeleza walimu wa
maandalizi katika ngazi ya stash-hada na shahada Zanzibar, hali inayoashiria
kuwa, bado Wizara ina jukumu kubwa la kujipanga katika kuendeleza elimu hii kwa
kuwaendeleza walimu wake.
Kamati yetu inaishauri Wizara kuipitia Sera yao ya
Elimu ili kuweza kuandaa mpango maalum na kamili wa namna ya kuiimarisha na kuwaendeleza
walimu wa maandalizi.
Mheshimiwa Spika, Idara pia inaratibu vyuo vya Qur-ani na madrasa
lakini mpaka sasa hakuna mtaala unaofahamika katika kutoa mafunzo katika vyuo
vya Qur-ani na Madrasa. Kamati yetu inaishauri Wizara ikishirikiana na ofisi ya
mufti kuvisamimia vyuo vya Qur-an na madrasa kwa kuwa na muongozo maalum wa
kuendesha vyuo vya Qur- ani na pia kuwepo na Utaratibu wa kufanyiwa ukaguzi wa
vyuo na kuviandalia mazingira mazuri ya kujisomea.
Mheshimiwa Spika, imekuwa ni utamaduni wetu wazanzibar kuwapeleka
watoto wetu katika vyuo vya Qur-ani kama ni sehemu ya mwanzo ya kujifunza mtoto
hata kabla ya kupelekwa katika skuli za maandalizi lakini cha kusikitisha ni kuwa,
kutokana na elimu hiyo kutupwa na kudharaulika watoto wamekuwa hawapendi kwenda
madrasa kutokana na mazingira mabaya ya vyuo hivyo, Kamati yetu inasisitiza
tena kuwepo kwa mazingira bora katika vyuo na madrasa zetu ili kuwatia hamu
watoto wetu kusoma elimu ya dini.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa elimu ya msingi nayo inakabiliwa na
changamoto ya upungufu wa walimu. Kamati yetu iliarifiwa kuwa kwa upande wa
Pemba shule za Micheweni,Wete,Chakechake na Mkoani zina upungufu mkubwa wa
walimu ambao husababishwa na ongezeko kubwa la maskuli majimboni usioenda
sambamba na ajira mpya za walimu,walimu wengi wanaostaafu ni wa skuli za
msingi,idadi ya wanafunzi kuwa kubwa na walimu wengi wa msingi wanapoenda kuongeza
kiwango cha elimu huwa hawapendi kurudi kusomesha skuli za msingi au hukimbilia
kada nyengine.
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inaiomba Serikali kuisaidia Wizara
katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbali mbali zinazoikabili Idara ya Elimu
ya Msingi pamoja na kufanya haraka ajira za walimu katika skuli za msingi.
Mheshimiwa Spika.
Kuhusu Utekelezaji wa
Miradi ya Maendeleo ya Wizara.
Wizara imekuwa ikitekeleza miradi mbali mbali kwa
ufanisi lakini Kamati imekuwa na masikitiko makubwa juu ya utekelezaji usio wa
ufanisi kwa Mradi wa Upanuzi wa Huduma za Maktaba,Mradi wa Uimarishaji wa Elimu
ya Ufundi na Mradi wa Ujenzi wa Vyuo vya Kiislamu ambapo miradi yote hiyo inatekelezwa
na Serikali pekee.
Mheshimiwa Spika.
Katika miradi hiyo Kamati yetu imebaini uingizwaji
wa fedha usio wa kuridhisha. Hivyo, Kamati yetu inaitaka Serikali katika bajeti
ya mwaka huu wa fedha (2013/2014) kuingizia fedha Wizara ipasavyo ili iweze
kutekeleza miradi yake mbali mbali kwa ufanisi.
Mheshimiwa Spika
Elimu Mjumuisho.
Kamati yetu inaipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo
ya Amali kupitia Kitengo chake cha Elimu Mjumuisho, kuweza kuwahudumia wanafunzi
wenye mahitaji maalum ya kielimu, wakiwemo watoto wenye ulemavu na watoto
walioko katika mazingira hatarishi katika skuli zilizopo Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika, Hata hivyo Kamati inaishauri Wizara kuongeza
malipo ya motisha ( posho) kwa walimu wanaosomesha wanafunzi wenye mahitaji
maalum kwani walimu hao wamekuwa wanafanya kazi ngumu sana kutokana na ukubwa
wa madarasa ya wanafunzi hao.
Mheshimiwa Spika, walimu hao ingawa wamekuwa wanapewa motisha
kutokana na kazi ngumu wanayoifanya lakini Kamati yetu kwa upande wa Pemba
ilibaini kuwa kiwango cha motisha wanayolipwa cha shilingi elfu tano (5000/)
katika Skuli za Michakaini na Pandani ni kidogo na cha muda mrefu tokeo mwaka
1991. Kiukweli hakilingani na ugumu wa kazi pamoja na mabadiliko ya gharama za
maisha, hivyo Kamati inaishauri Wizara kufikiria kuwaongezea kiwango ili kuwapa
moyo kutokana na kazi ngumu na ya thamani wanayoifanya.
HITIMISHO:
Sekta ya Elimu ni sekta muhimu ambapo kuboreshwa
kwa sekta hii kutapelekea mafanikio ya sekta nyenginezo. Kamati yetu imegundua changamoto nyingi katika sekta hii muhimu
ikiwemo kutopewa kipao mbele kwa
watumishi wake. Taaluma ya elimu bado haijapewa kipaumbele, walimu wetu
wamekosa chombo huru cha Sheria ambacho kitaweza kusimamia maadili na taaluma
ya ualimu.
Aidha, walimu wetu wamekuwa na maslahi duni na
ualimu umekuwa unashuka hadhi yake. Kamati yetu inaiomba Serikali kusimamia
sekta ya Elimu ipasavyo pamajo na kuwepo chombo huru cha kusimamia maslahi yao
ili tuone hadhi ya elimu inarudi tena Zanzibar.
Mheshimiwa Spika
Baada ya maoni hayo ya Kamati, sasa napenda
kuwatambulisha wajumbe wa Kamati ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa Jamii kama
ifuatavyo:-
1.
Mhe. Mgeni Hassan Juma Mwenyekiti
2.
Mhe. Hassan Hamad Omar Makamo
Mwenyekiti
3.
Mhe. Ali Salum Haji Mjumbe
4.
Mhe. Abdi Mosi Kombo Mjumbe
5.
Mhe. Farida Amour Mohamed Mjumbe
6.
Mhe. Mwanaid Kassim Mussa Mjumbe
7.
Mhe. Mohammed Mbwana Hamad Mjumbe
Nachukua fursa hii kuwapongeza sana wajumbe wa
Kamati na kuwaomba kuendelea na kujituma katika kuendeleza majukumu yetu. Pia
nawapongeza makatibu wetu wawili wa Kamati ambao wamekuwa wakitusaidia kwa
karibu katika kutekeleza kazi zetu. Nao ni:-
1.
Ndg. Maryam Rashid Ali Katibu
2.
Ndg. Asha Said Mohamed Katibu
Mheshimiwa Spika naunga mkono hoja hii mimi binafsi na kwa niaba
ya Kamati ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa Jamii tunaunga mkono hoja.
Ahsante sana kwa kunisikiliza na naomba kuwasilisha.
Ahsante.
…………..
Mhe. Mgeni Hassan Juma,
Mwenyekiti,
Kamati ya Maendeleo ya Wanawake na Ustawi wa
Jamii,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment