Habari za Punde

Dkt. Mvungi Asafirishwa Afrika ya Kusini kwa Matibabu Zaidi.





JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
TUME YA MABADILIKO YA KATIBA
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Alhamisi, Novemba 7, 2013

Tume ya Mabadiliko ya Katiba inapenda kuwafahamisha wananchi kuwa Mjumbe wake Dkt. Sengondo Mvungi aliyekuwa akipata matibabu katika Kitengo cha Mifupa Muhimbili (MOI) amesafirishwa leo (Alhamisi, Novemba 7, 2013) saa 5:45 asubuhi kwenda nchini Afrika Kusini kwa uchunguzi na matibabu zaidi.

Akiwa nchini Afrika Kusini, Dkt. Mvungi atapata matibabu katika Hospital ya Milpark iliyopo jijini Johannesburg.

Itakumbukwa kuwa Dkt. Mvungi alivamiwa nyumbani kwake Kibamba, wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na watu waliomjeruhi vibaya kichwani usiku wa kuamkia siku ya Jumapili, Novemba 3, 2013. Tukio hilo la uvamizi linaendelea kuchunguzwa na vyombo vya ulinzi na usalama nchini.

Tangu siku alipojeruhiwa, Dkt. Mvungi alikuwa akipata matibabu katika Kitengo cha Mifupa Muhimbili (MOI). Hata hivyo, Madaktari waliokuwa wakimtibu MOI, walishauri afanyiwe uchunguzi na matibabu zaidi. 

Dkt. Mvungi ameondoka na ndege ya kukodi ya Shirika la Ndege la Flightlink na ameambatana na Dkt. Mugisha Clement Mazoko kutoka MOI; Muuguzi Bi. Juliana Moshi; na mtoto wa kaka yake Bw. Deogratias Mwarabu. Serikali inagharamia gharama zote za matibabu ya Dkt. Mvungi.

Tume inawaomba wananchi wote waendelee kumuombea kwa Mungu Dkt. Mvungi ili aweze kurejea katika hali yake ya kawaida na hatimaye kuendelea majukumu yake.

Mwisho.

Imetolewa na:
Ndg. Assaa A. Rashid,
Katibu,
Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
Dar es Salaam
Alhamisi, Novemba 7, 2013

0757 – 500800 /  0714 662482 / 0717 084 252 /

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.