Na Mwandishi Wetu
MWENYEKITI
wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji (mstaafu) Joseph Warioba, amesema baadhi
ya taasisi za kiserikali, ama moja kwa moja au kwa tafsiri ya mapendekezo yao , zilipendekeza au
kukubali muundo wa serikali tatu.
Kwa
mfano, alisema Baraza la Wawakilishi
Zanzibar lilipendekeza kuwepo mamlaka huru ya Zanzibar, mamlaka huru ya
Tanganyika na mamlaka ya Muungano na iwekwe wazi maeneo, uwezo, nguvu, utendaji
na mipaka ya kila mamlaka.
Akiwasilisha
rasimu ya katiba jana kwa Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba mjini Dodoma,
alisema Baraza la Ofisi ya Makamu wa Rais lilipendekeza, kuhusu muundo wa
serikali kwamba, kuwe na rais mmoja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
wakuu wa serikali za washirika wa muungano wapewe vyeo vingine vinavyoendana na
hadhi na mamlaka zao.
Alisema
baraza hilo
lilisema katika kutaja serikali tatu inabidi zitenganishwe ili serikali ya
Muungano ionekane ndio ya juu.
Huku
akishangiriwa na wabunge, alisema Baraza la
Ofisi ya Waziri Mkuu lilipendekeza, kuwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano, Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, Waziri Mkuu wa Serikali ya Tanganyika na Waziri Mkuu wa Serikali ya Zanzibar .
Aidha
alisema baraza hilo
lilisema mapendekezo hayo ni kwa sababu hakuna umuhimu wa kuwa na marais watatu
katika nchi moja na wala neno Rais halimuongezei hadhi kiongozi yeyote.
Pia
alisema Baraza hilo
lilisema hali hiyo itatoa nafasi kwa Mawaziri Wakuu kuwa watendaji zaidi na
hivyo kusimamia serikali za washirika.
Alisema
Bunge la Jamhuri ya Muungano katika maoni yake lilipendekeza kuwepo Tume ya
Utumishi wa Bunge ambayo inajumuisha, katika wajumbe wake, Spika wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano (Mwenyekiti), Spika wa Bunge la Tanzania Bara na Spika wa Baraza la
Wawakilishi Zanzibar.
Akinukuu
sehemu ya waraka wa Baraza la Wawakilishi uliowasilishwa Tume Februari 2013,
pamoja na mambo mengine, alisema Baraza la Wawakilishi lilitoa maoni
yafuatayo:“Kwa sababu Wazanzibari ni waumini wa Muungano ambao haukuondoa na
hautoondoa uwepo wa Zanzibar kama nchi, ni vyema Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania ijayo iweke wazi kuwa Tanzania ni Jamhuri ya Muungano inayotokana
na Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Hali hii itahakikisha
kuwepo na maeneo maalum ya mamlaka ambayo Zanzibar
ina uwezo nayo kama nchi (yaani, mamlaka ya dola ya Zanzibar ).
“Kwa
sababu inapendekezwa kuwepo na mamlaka ya Zanzibar huru na mamlaka ya
Tanganyika huru ndani ya Jamhuri ya Muungano, mamlaka ya Muungano iwekwe wazi –
maeneo yake, uwezo au nguvu zake, na utendaji wake. Mambo yote hayo yawekwe
wazi na mipaka yake,”alinukuu.
“Uwepo
wa Muungano uonekane katika hali zote
uundwaji wa mamlaka za Muungano, ufanyaji kazi katika mamlaka za
Muungano, ufanyaji wa maamuzi katika mamlaka za Muungano, na uingizwaji na
upunguzwaji katika orodha wa mambo ya Muungano,” anukuu sehemu ya waraka huo wa
Baraza.
Alisema
baada ya kuona takwimu hizo na kuchanganua sababu zilizotolewa na makundi mbali
mbali, Tume iliamua kufanya utafiti wa kina kuhusu muundo wa muungano na
matatizo yake tangu muungano ulipoundwa.
Alisema
katika utafiti huo mambo kadhaa yamejitokeza, ambapo alisema kulikuwa na changamoto nyingi baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana mwaka 1964 na kwamba ujenzi
wa taasisi za kuendesha mambo ya muungano ulikuwa ni changamoto kubwa.
Aidha
alisema Serikali ya Muungano haikuwa na taasisi zake, kwa hiyo ilianza kwa
kutumia taasisi zilizokuwapo katika sehemu zote mbili za muungano.
Alisema
hata uamuzi wa kuifanya Tanzania
kuwa nchi ya demokrasia ya chama kimoja ulichukuliwa wakati nchi ikiwa na vyama
viwili; TANU na ASP kwa hivyo kila upande uliendesha mambo yake kutumia itikadi
na sera zake.
Alisema
changamoto hizo hazikuzuia kuimarika kwa muungano kwa sababu utashi wa kisiasa
wa waasisi wa muungano ulikuwa mkubwa.
Jaji
Warioba alisema baada ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuvunjika, baadhi ya mambo
yaliyokuwa chini ya Jumuiya hiyo yaliwekwa kwenye orodha ya mambo ya muungano,
matokeo yake, nchi ilionekana moja, yenye mshikamano, utulivu na amani.
“Wakati
huo, viongozi na watumishi wa umma na kwenye chama cha siasa walipangiwa kazi
sehemu yoyote ya nchi bila kujali sehemu wanayotoka. Kwa muda mfupi nchi
ilionekana kuwa kweli ni taifa moja,lakini hali hiyo haikudumu kwa muda mrefu,utaifa
wa nchi mbili ukaanza kujitokeza. Viongozi na watumishi wa umma kutoka upande
mmoja wa muungano wakaonekana hawapendi kwenda kufanya kazi upande wa pili wa muungano,”
alisema.
“Pia
majina ya sehemu mbili za Muungano yakabadilishwa. Badala ya Tanzania Bara na
Tanzania Visiwani tukaanza kutumia Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar, ili
kulinda Zanzibar
isionekane imemezwa. Ni wakati huo, lugha ya Tanganyika kuvaa Koti la Muungano
ilianza kusikika,” alisema.
Alisema
1984, kulitokea kile kilichoitwa “kuchafuka kwa hali ya hewa ya kisiasa Zanzibar ”, ambapo msingi wake ilikuwa ni mpango wa baadhi
ya viongozi wa Zanzibar kutaka serikali tatu,
ingawa jaribio hilo halikufanikiwa, Zanzibar ilitunga katiba mpya
mwaka huo huo.
Alisema
kwa maana nyingine, Zanzibar ikaanza kutumia bendera ya taifa iliyo tofauti na
mwaka 1992, ikajiunga ilijiunga na (OIC) na Bunge lilipitisha azimio la
kuzitaka serikali zote mbili kushirikiana katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo na matatizo mengine
ya muungano na kutoa taarifa bungeni katika kipindi cha mwaka mmoja.
Alisema
mwaka 1993, wakati wa mkutano wa bajeti, wabunge kutoka Tanzania Bara (G55)
walipeleka bungeni hoja ya kuundwa kwa serikali ya Tanganyika, hoja ambayo
ilipitishwa, hata hivyo Novemba 1993 kikao maalum cha CCM kilichofanyika Dodoma
kilifikia muafaka kwamba azimio hilo la
bunge lisitekelezwe.
Alisema
Tume yake iliamua kufanya uchambuzi wa kina kuhusu baadhi ya malalamiko, hasa
malalamiko ya Zanzibar kwa sababu malalamiko ya Tanzania Bara kuhusu Muungano
yanatokana, kwa kiwango kikubwa na hatua zilizochukuliwa kwa upande wa Zanzibar .
Alisema
kama malalamiko ya Zanzibar yakipatiwa ufumbuzi, malalamiko ya Tanzania Bara
nayo yatakuwa yamepatiwa ufumbuzi.
Alisema
katika kuchambua malalamiko ya Zanzibar kwamba Tanganyika imevaa koti la
Muungano, Tume imebaini kwamba muundo wa sasa wa muungano umeifanya Serikali ya
Muungano, kwa kiwango kikubwa, kushughulikia zaidi mambo ya Tanzania Bara, hasa
mambo ya maendeleo ikiwemo kilimo, elimu, afya, maji, nishati na madini,
ujenzi, uchukuzi, maliasili na utalii.
Alisema
wakati wa kikao cha bajeti, bunge la muungano hutenga siku mbili au tatu za
majadiliano kwa wizara zinazosimamia mambo hay ya Tanzania Bara wakati mambo ya
Muungano kama vile ulinzi, mambo ya nje na mambo ya ndani hutengewa siku moja
au nusu siku.
“Sheria
nyingi zinazotungwa na bunge zinahusu mambo ya Tanzania Bara. Maswali ya wabunge
kuhusu mambo ya maendeleo pia yanahusu Tanzania Bara na ziara za wabunge
kukagua miradi ya maendeleo zinahusu Tanzania Bara katika mambo yasiyo ya
Muungano,” alisisitiza.
Alisema
hali hii ndiyo imeifanya Tanganyika
ionekana imevaa koti la muungano.
Akizungumza
kwa kujiamini alisema hata Rais wa Jamhuri hafanyi ziara za kukagua miradi ya
maendeleo na kutoa ahadi kwa upande wa Zanzibar .
“Sura
ya Serikali ya Muungano inaonyesha kuegemea zaidi upande wa Tanzania Bara.
Kati ya Wizara 24 ni wizara mbili tu ndizo zinazoshughulikia mambo ya Muungano
pekee. Wizara kumi zinashughulikia mambo ya Tanzania
Bara na Wizara kumi na mbili zinashughulikia mambo mchanganyiko ambayo mengi ya
mambo hayo yanahusu Tanzania
Bara. Kwenye utawala, viongozi wakuu wengi wa Wizara wanatoka Tanzania Bara,”
alisema.
Alisema
hivi sasa ni Katibu Mkuu mmoja tu ndiye anayetoka Zanzibar
na kwamba hali hiyo inatokana na ukweli
kwamba serikali ya Muungano inashughulikia zaidi mambo yasiyo ya Muungano na
ndiyo imeifanya Tanganyika
kuonekana imevaa koti la Muungano.
Alisema
eneo jingine lenye matatizo ni mgongano kati ya katiba ya Muungano na katiba ya
Zanzibar .
Alisema
ibara ya 132 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984
imeweka masharti kwamba sheria zinazotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano
hazitatumika Zanzibar
hadi zipelekwe Baraza la Wawakilishi.
Alisema
jambo hilo limeleta
mgongano wa katiba na juhudi zilizofanywa na pande zote mbili hazikufanikiwa
kuondoa mgongano huo.
Katika
muafaka wa mwaka 1994, alisema serikali zote zilikubaliana kwamba Zanzibar ifanye
mabadiliko kwenye katiba yake ili mgongano huo uondolewe lakini adi sasa
muafaka haujatekelezwa.
Aidha
alisema mabadiliko ya katiba ya Zanzibar katika ibara
ya kwanza yaliyofanywa mwaka 2010 yametamka wazi kwamba Zanzibar
ni nchi kati ya nchi mbili zinazounda Muungano wakati katiba ya Jamhuri
inaelekeza kwamba Tanzania
ni nchi moja.
Alisema
mabadiliko ya katiba ya Zanzibar pia yamehamisha
baadhi ya madaraka ya Serikali ya Muungano kwenda Zanzibar .
Kwa
mfano, alisema katiba ya Jamhuri inampa
Rais wa
Jamhuri madaraka ya kuigawa nchi katika maeneo lakini katiba ya Zanzibar imeyahamisha madaraka hayo kwenda kwa Rais wa Zanzibar .
Alisema
wakati wa kukusanya maoni ya wananchi, Tume ilibaini haitakuwa rahisi kubadili katiba
ya Zanzibar kuifanya Zanzibar kuonekana kuwa sehemu ya Jamhuri ya
Muungano badala ya kuwa na sura ya nchi.
Mabadiliko
ya aina hiyo alisema yatahitaji kura ya
maoni kama katiba ya Zanzibar inavyoelekeza na kwamba ni dhahiri uwezekano wa
kufanya mabadiliko kwenye katiba ya Zanzibar ili Zanzibar iwe sehemu ya nchi
moja badala ya kuwa nchi, ni mdogo sana .
hatutaki tatu wala nne , kila mtu ababe mzigo wake, tuachieni nchi yetu , tushirikiane kama marafiki na ndugu tu au majirani , Wajumbe wa znz msikubali kuyumbishwa mara hii tunajua akina vuai na kundi lake si wenzetu hao , lakini msitetereke mliobaki mpiganie uhuru wetu mpaka upatikane , angalia kule krimea wameamua tu kupiga kura ya maoni wamepiga na kuchukua nchi yao , hao ndo wanaume, sio sisi mayakheeee tunabakia kupiga makofi bila kujua kinachoshangiliwa
ReplyDelete