Habari za Punde

KILELE SIKU YA MTOTO WA AFRIKA

Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora (THBUB) inaungana na Watanzania wote katika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika yenye kauli mbiu “Haki za Mtoto; Tulipotoka, Tulipo na Tuendako.”                                                                                             

Kupitia kauli mbiu ya mwaka huu, THBUB inaendelea kuhamasisha jamii kuheshimu na

na kulinda haki za mtoto kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Sheria, Seraa na Miongozo mbalimbali inayolinda haki za mtoto nchini.

Maadhimisho ya mwaka huu yanalenga kuwaelimisha na kuwakumbusha wazazi na walezi kwenye jamii pamoja na watoa huduma wote, wajibu wao katika kutekeleza haki ya 5 za mtoto  zikiwemo Haki ya kuishi kwa mtoto bila ya kukatishwa uhai wake, haki ya kuendelezwa kielimu,  utamaduni na vipaji vya mtoto, haki ya kulindwa dhidi ya ukatili wa aina yoyote, haki ya kushiriki kutoa maoni kwenhye masuala yanayomuhusu kulingana na umri wake na  haki ya kutobaguliwa kutokana na hali yake.

THBUB inatambua na kuunga mkono juhudi mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kulinda haki za watoto pamoja na kuridhia Mikataba ya Kikanda na Kimataifa, kutunga Sera na Sheria ya Mtoto ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Zanzibar ambazo zinalinda haki za watoto.

Pamoja na jitihada mbalimbali zilizochukuliwa bado zina zipo changamoto kadhaa ambazo zinarudisha nyuma juhudi za uapatikanaji wa haki za watoto.

Changamoto hizo ni pamoja na watoto kubakwa, kulawitiwa, kuolewa wakiwa na umri mdogo, kuteswa, kufanyishwa kazi ngumu, kukatishwa masomo, kuuliwa kwa imani za ushirikina, kushirikishwa kwenye ngono, watoto wenyeulemavu kufichwa n.k hali inayoathiri ukuaji wao.

Hivyo, Tume inatoa mapendekezo yafuatayo.

i.    Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali iendelee kutoa elimu ya haki za matoto na ukatili wa kijinsia na madhara yake.

ii.     Jamii iwafichue watu wote wanashiriki kufanya ukatili dhidi ya watoto.

iii.  Jamii iwafichue wazazi/walezi wote wanaokatisha masomo watoto kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kuwalazimisha  kuolewa.

iv.  Serikali iendelee kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayemuajiri mtoto na kumazimisha kufanya kazi ngumu.

v.  Wazazi na walezi wahakikishe wanawatunza, kuwalinda na kuwapatia watoto mahitaji yao ya msingi. Aidha, wahakikishe watoto wote wanahudhuria shule na hawawatumii kama vitega uchumi vya familia kwa kuwafanyisha kazi ngumu, zisizofaa na zinazowaathiri.

“Haki za Mtoto; Tulipotoka, Tulipo na Tuendako”

Imetolewa na:

Mathew P. M. Mwaimu (Jaji Mstaafu)

MWENYEKITI

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA






No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.