Habari za Punde

Kukosekana hekima bunge la Katiba, ni janga la taifa

Na A K Khiari
Wazungu wana msemo mmoja, silence is golden, ukimaanisha kwamba kunyamaza kimya wakati mwengine huwa kama ni dhahabu.
Watu wanaweza kusema, wakanena, wakan’gaka, wakatamka lakini wengine huweza kukaa kimya bila ya kusema chochote. Si kwamba hawana la kusema bali wameangalia hali iliyopo na mazingira yalivyo na kwa kutumia hekima wakaona bora wanyamaze wasiseme. Si kwamba hawawezi kusema, laa hasha basi tu walijiamulia tu kujinyamazia.
Mwanafalsafa wa kigiriki, Plato, nae pia aliwahi kunukuliwa akisema: ‘Wenye hekima husema kwa sababu wana sababu ya kusema, majahili (husema) ili wapate tu na wao kusema’ Yaani almuradi na mimi nimeonekana kusema.
Kunyamaza kimya bila ya kusema wakati wengine wakisema ni moja katika mambo yanayohitajia hekima.
Hekima ni kitu adhimu sana katika maisha ya binadamu na ndiyo maana Allaah Subhaanahu Wata’ala Amesema ndani ya Qur’aan kwamba ‘Humpa hekima amtakae na humuondoshea hekima amtakae na aliyepewa hekima basi amepewa kheri kubwa’ ( Al Baqarah 269).
Nabii Suleiman ‘Alayhis Salaam alipopewa nafasi ya kuchagua jambo lolote kutoka kwa Muumba alichagua hekima, hakuchagua mali wala utajiri au utawala alimuomba Allaah Subhaanahu Wata’ala amjaalie awe na hekima.
Mtume wetu Muhammad, rehma na amani zimwendee, alituruhusu tuwe na husda (kitu ambacho ni haramu kimsingi) katika mambo mawili tu: kwa mtu aliyejaaliwa na Mwenyezi Mungu mali kisha akawa anatumia utajiri wake kwa haki ( huyu tuwe na husda naye kwa kutaka kuwa kama yeye) na yule mtu aliepewa hekima na akawa anaitumia hekima aliyojaaliwa na kuifundisha kwa watu ( huyu pia tunaweza kuwa na husda naye). Bukhaari na Muslim
Kilichonisukuma kuandia waraka huu mfupi ni kwa jinsi ninavyoshuhudia yanayojiri na yanayotokea katika Bunge la Katiba linalofikia tamati huko Dodoma ambapo vitu viwili nilivyogusia hapo juu vilipokosekana.
Madhara ya kusema tu bila ya kuwa na hekima yanaweza kuwa makubwa na tumeona mifano michache ya kauli za waliobahatika kusema katika bunge la katiba ambao ima waliamua kwa maksudi kuiweka hekima pembeni au masikini hawakufahamu kwamba kabla ya kusema unahitajia kuwa na hekima.
Yaa laiti kwamba walioteuliwa wangelikuwa wamepata kheri ya hekima basi tungeliona kheri hii ikitumika Dodoma,.Yaa laiti walioteuliwa wangeliamua kunyamaza basi tungeliweza kuwajua ni wapi waliojaaliwa hekima na wepi waliokosa kheri hii na kuangukia katika kundi ambalo waarabu wana msemo husema atakaposema mtu jahili basi usimjibu kwani jibu lake ni kunyamaza kimya.
Baya zaidi ni kuona mpaka viongozi wa dini ambao tuliwatarajia kuwa mstari wa mbele kuonesha kuwa na hekima nao wametumbukia katika dimbwi la kukosa busara kwa jinsi ya kauli za na matamshi yao. Viongozi hawa wa dini kama wangelitumia fursa ya kuzungumza na kudarisisha Bunge kuhusu hekima basi wangelikuwa wamefanya kazi kubwa sana kwani ndiyo kitu muhimu klilichokosekana kule.
Ni jambo la kusikitisha sana kuona fursa ya kutumia hekima imekosekana bungeni na hali hii inaakisi hali halisi ya wananchi wa nchi hii walivyokosa upeo wa kuwa na hekima. Tukichukulia sampuli chache ya yanayotokea Bungeni basi inatupa picha halisi kwamba Wananchi wetu sasa hawana hekima! Na hili ni janga kubwa kwa taifa!.
Nadhani umefika wakati tuandae mtaala maalum ambapo somo hili la hekima na busara lianzwe kusomesha maskulini, misikitini, madarasani na hata makanisani ili kuweza kukiokoa kizazi chetu na kijacho na janga kubwa la kukosa hekima kwani madhara yake pia yatakuwa makubwa pia kama yanavyoonekana kwenye bunge la katiba!.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.