Habari za Punde

Tanzania yajivunia amani Comoro

 Na Said Ameir, Comoro
TANZANIA imempongeza Rais wa Muungano wa Comoro, Mhe. Dk. Ikililou Dhoinine, kwa kuimarisha umoja na mshikamo miongoni mwa wananchi wa nchi hiyo ambapo hivi sasa Comoro imekuwa na utulivu na amani.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, alisema  ni jambo la kujivunia kuona wananchi wa visiwa huvyo wako katika utulivu, amani na wamekuwa bega kwa bega na serikali yao chini ya uongozi wa Rais Dhoinine.

Akizungumza katika hafla ya chakula cha jioni kilichoandaliwa kwa heshma yake na mwenyeji wake, Rais wa Muungano wa Comoro, Dk. Shein alisema ziara yake nchini humo ina lengo la kuimarisha ushirikiano wa kihistoria na kindugu uliopo baina ya  wananchi wa Tanzania na Comoro.

Alimueleza Rais Dhoinine na wageni waliohudhuria hafla hiyo kuwa amefurahishwa na namna serikali na wananchi wa Comoro wanavyothamini uhusiano wao na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na ushirikiano na ndugu zao wa Zanzibar.

“Najisikia niko nyumbani kwa sababu uhusiano wetu umeimarishwa zaidi na mahusiano ya wananchi wake kwa karne nyingi, mahusiano ambayo yamekuwa katika masuala ya kijamii, utamaduni, biashara na mambo mengine mengi,” alibainisha Dk. Shein.

Aliongeza kuwa Zanzibar na Comoro zina mazingira yanayofanana na hata changamoto zinazokabiliana nazo, hivyo ushirikiano katika kukabiliana nazo ni jambo jema linaloweza kuleta mafanikio kwa faida ya ustawi wa watu wa Zanzibar na Comoro.

Alimueleza Rais Dhoinine kuwa Zanzibar na Comoro zina malengo mamoja ya kuleta maendeleo na ustawi kwa wananchi wao kwa hivyo hiyo ni fursa kwa Zanzibar na Comoro kushirikiana kwa pamoja kutimiza lengo hilo. 

Alimshukuru Rais wa Comoro kwa kumualika kutembelea nchini mwake ambapo viongozi hao wawili walipata fursa ya kufanya mazungumzo ambayo yamefungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Comoro.  

Kwa upande Rais wa Comoro, Mhe. Dk. Ikililou Dhoinine, alieleza ziara ya Dk. Shein nchini humo kuwa imegusa hisia za wananchi wa Comoro kwa kuwa wananchi wa Comoro na Zanzibar wana uhusiano wa damu na kuifananisha hafla hiyo kuwa ni muungano wa kifamilia.

“Tunafahamu fika uhusiano wa mioyo na damu inayowaunganisha watu wetu, uhusiano unatokana na historia, lugha, mila na utamaduni, kutembeleana mara kwa mara na wananchi wengi wa visiwa kubadilishana makazi katika visiwa hivi,”alisema.

Alimshukuru Rais wa Zanzibar kwa kukubali mwaliko wake wa kutembelea Comoro.

Mapema marais hao walifanya mazungumzo rasmi ikulu ambayo yalikuwa juu ya namna ya kukuza ushirikiano kati ya Zanzibar na Comoro ikiwemo kuangalia maeneo mapya ya ushirikiano kwa manufaa ya pande mbili hizo.

Kwa mujibu wa ratiba ya ziara hiyo, Dk. Shein anatarajiwa kutembelea kiwanda cha samaki na baadae kwenda mji wa Mitsamihouli ambako wakaazi wake wengi wana mafungamano na wananchi wa Zanzibar. 

Akiwa huko atashiriki sala ya adhuhuri na baadae kupata chakula cha mchana kilichoandaliwa na wananchi wa Mitsamihouli kwa heshma yake na ujumbe wake.


Baadae atatembelea ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Comoro ambako atapata fursa ya kuzungumza na Watanzania wanaoishi nchini humo na pia kuzindua tovuti ya ubalozi.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.