Habari za Punde

Ajali za barabarani zaendelea kutesa · Watu 480 wafariki, 4361 wajeruhiwa

Na Salum Vuai
Pamoja na kuwepo sheria nzuri na kanuni za usimamizi wa sekta ya usafiri nchini, bado ajali za barabarani zimeendelea kuongzeka na kupoteza maisha ya wananchi wengi.
Aidha ajali hizo zimekuwa zikisababisha ulemavu wa kudumu kwa watu wengi na kuharibu miundombinu, hali inayoitia hasara kubwa serikali.
Katika kikao cha nne cha kawaida cha Bodi ya Usafiri Barabarani kilichofanyika katika ofisi ya Mfuko wa Barabara Maisara mjini Zanzibar, wajumbe walieleza kusikitishwa kwao na hali hiyo, licha ya kuwepo mikakati mbalimbali kuidhibiti.
Takwimu za kitengo cha usalama barabarani cha Jeshi la Polisi zilizowasilishwa kwenye kikao hicho, zinaonesha kuwa katika kipindi cha miaka minne, 2010/2013 jumla ya ajali 3,217 zilitokea Unguja na Pemba, zikihusisha vyombo mbalimbali vya moto, baiskeli, waendao kwa miguu na wanyama.
Vifo 480 vilitokea kutokana na ajali hizo, ambapo wanaume waliopoteza walikuwa 404 na wanawake 76.

Aidha, watu 4,361 walijeruhiwa, kati yao, wanaume 3346 na wanawake 1015.
Katika kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Bodi Mussa Msheba Suleiman, ilielezwa kuwa, idadi hiyo ya ajali ni ya kutisha kwani inaendelea kupukutisha ya nguvu kazi inayotegemewa na nchi katika kuleta maendeleo. 
Mchanganuo wa takwimu hizo unaonesha kuwa, mwaka 2013, ndio ulioongoza kwa kuwa na ajali nyingi  zilizofikia 836, zikisababisha vifo 126, (wanaume 109 na wanawake 17), na mejeruhi 1,139, (wanaume 824 na wanawake 315).
Kwa mujibu wa takwimu hizo, idadi ya ajali imekuwa ni ya kupanda na kushuka kati ya mwaka 2010, 2011 na 2012.
Mwaka 2010, jumla ya ajali zote ilikuwa 747, vifo 112 (wanaume 92, wanawake 20), na majeruhi 1264, wakiwemo wanaume 920 na wanawake 344.
Mnamo mwaka 2011, jumla ya ajali 809 ziliripotiwa Unguja na Pemba, ambazo zilisababisha roho za watu 106 kupotea, wanaume 90 na wanawake 16.
Ajali hizo za mwaka 2011 ziliacha majeruhi 1,056 wakiwemo wanaume 887 na wanawake 169.
Mwaka 2012 watu 136 walifariki dunia kutokana na ajali 825 zilizotokea, na kati ya hao, wanaume walikuwa 113 na wanawake 23, huku watu 902 wakijeruhiwa (wanaume 715 na wanawake 187).
Wajumbe hao wa Bodi, katika kuelezea ongezeko la ajali nchini, walisema hali hiyo inasababishwa na mambo mengi ikiwemo madereva na wamiliki wa vyombo vya usafiri kuzifumbia macho sheria na kanuni zilizopo.
Kwa upande mwengine, walisema pamoja na jeshi la polisi kujitahidi kuwashika wanaokiuka sheria na kuwafikisha mahakamani, lakini ni hukumu chache sana zinazotolewa kwa wahusika, au kupewa adhabu ndogo kulinganisha na ukubwa wa makosa hao.

Walishauri hatua mbalimbali za kuchukua ili kupunguza idadi ya ajali, ikiwemo Idara ya Usafiri na Leseni kuweka wakaguzi wake barabarani ili kukabiliana na madereva na matingo wakorofi.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.