Na Mwantanga Ame
Serikali imesema migogoro inayojitokeza katika sekta ya afya kutokana na kuwepo wadau
wengi, ndio sababu ya kuanzisha sheria mpya ya wauguzi na wakunga, ambapo
mswada wake uliwasilishwa jana.
Waziri Afya,
Mhe. Rashid Seif, alisema hayo jana wakati akiwasilisha mswada huo, katika
kikao cha Baraza la Wawakilishi.
Alisema sekta ya afya kumekuwa na wadau wengi
walioamua kujiunga pamoja nao, lakini kulikuwa na migogoro iliyokuwa
ikijitokeza kwa taasisi hiyo, hivyo serikali inapanga kuiondoa.
Alisema sheria
hiyo mpya itatoa fursa ya kuwatambua waunguzi katika sekta ya umma na binafsi,
kwani mabadiliko ya sekta ya afya ni kukuza utoaji huduma kwa wananchi.
Nae
Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleao ya Wanawake na Ustawi wa Jamii ya Baraza la
Wawakilishi, Mhe. Mgeni Hassan Juma, alisema mabadiliko ya kiuchumi, ongezeko
la watu na kutanuka taaluma ya uuguzi na ukunga, kumesababisha kufutwa sheria
ya zamani ili kwenda na wakati.
Alisema baraza
la wauguzi, litazingatia maadili ya wauguzi na wakunga na kuleta ufanisi zaidi
kwa vile litasimamia kikamilifu utendaji wa taasisi hizo.
Wakichangia
mswada huo, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, wameitaka serikali kuviangalia
baadhi ya vipele viliomo ndani ya mswada huo.
Mwakilishi
wa Chambani, Mhe. Mohammed Mbwana Hamad, alisema kifungu 15(3) kinachoelezea
masharti ya mtu anaetoka nje ya nchi kutaka kusajiliwa, kimeweka masharti yanayoweza
kusababisha udanganyifu kwa baraza litakaloundwa kusimamia sheria hiyo.
Alisema
kifungu 15 (3) (a) kimeeleza mtu atakaetoka nje ya nchi atalazimika kuwasilisha
ushahidi utakaoliridhisha baraza kuwa amesajiliwa na anastahiki kusajiliwa kuwa
muuguzi au mkunga katika nchi yake na kifugu kidogo cha (b) kinamtaka mtu huyo
kuwasilisha ushahidi kuwa amehitimu na kufaulu mafunzo ya uuguzi.
Alisema hofu
yake ipo zaidi katika kifungu cha 4 ambacho kinaeleza pindipo ikitokea kutokuwepo
kwa lolote kati ya yalioelezwa katika kifungu kidogo cha (a) na (b) na kifungu
kidogo cha (3), baraza hilo litamfanyia mtihani na muombaji naye atapaswa
kufaulu mtihani huo.
Alisema hiyo
ni kasoro inayoweza kutumiwa vibaya na wageni watakaotaka kufanya kazi za aina
hiyo nchini kwani wanaweza kutumia mwanya huo kufanya udanganyifu katika vyeti.
Alisema
serikali inapaswa kuchukua tahadhari hiyo, kwa sababu baadhi ya watu wana uwezo
wa kutumia mitandao kutengeneza vyeti bandia.
Alisema
katika kukabiliana na hali hiyo, baraza hilo linatakiwa kuwa na sifa za ziada katika uthibitishaji wa
wanaoomba kufanya kazi hiyo.
Naye Mwakilishi
wa Kiwani, Mhe.Hija Hassan Hija, alisema atakuwa mgumu kupitisha mswada huo
kama haujaelezea wazi hadhi watakayopewa wakunga wa jadi.
Alisema wakunga
wa jadi bado wana hadhi na haiwezekani kutohusishwa ndani ya sheria hiyo kwa
vile wanaendelea kufanya kazi hiyo.
Mhe. Mwakilishi
wa Wanawake, Mhe. Asha Bakari Makame, alisema mswada huo utaondoa matatizo
mengi yanayowakabili wafanyakazi wa sekta ya afya.
Wanu Hafidh
Ameir, aliiomba serikali kufikiria kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa
kuwapatia vifaa wauguzi.
Mwakilishi
wa Kitope, Mhe. Makame Mshimba Mbarouk, aliwataka watendaji wa taasisi hiyo
kutumia vyema sheria hiyo, kwa kuwa imejengeka tabia ya kuziweka makabatini
sehria badala kuzitumia.
Mapema
Spika wa Baraza la Wawakilishi, Mhe. Pandu Ameir Kificho, alimuapisha Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Mhe. Said Hassan Said, na kuwaomba wajumbe kumpa ushirikiano.
Alisema
uteuzi wa Mwanasheria huyo utasaidia
shughuli za baraza hilo na wako tayari kushirikiana nae.
Wajumbe wa
Baraza hilo walisimama kwa dakika moja kuomboleza kifo cha aliyekuwa Spika wa pili
wa baraza hilo, Ali Khamis, aliyefariki dunia Septemba 8, mwaka huu akiwa na
miaka 100.
No comments:
Post a Comment