Na Mwandishi
wetu, China
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, ametoa changamoto
kwa mabalozi wanaoziwakilisha nchi za Afrika nchini China, kuendelea kutangaza
habari njema kuwa bado ni salama kutembelea bara la Afrika pamoja na kuzuka
ugonjwa wa Ebola ambao umeua maelfu ya watu hasa katika nchi tatu za Afrika
Magharibi.
Alisema
Tanzania imetuma madaktari watano kwenda Afrika Magharibi kusaidia kukabiliana
na ugonjwa wa Ebola ambao unaendelea kuua maelfu ya watu katika nchi za Guinea,
Liberia na Sierra Leone.
Mpaka sasa
watu zaidi ya 4,000 wamepoteza maisha kwa ugonjwa huo katika nchi hizo.
Alisema ni
muhimu zaidi kwa nchi za Afrika kuongeza mshikamano na kusaidiana, ili kuongeza
nguvu za pamoja za kukabiliana na ugonjwa huo ambao umeanza kuwa tishio kwa
dunia nzima.
Aliyasema hayo
kwenye nyumba ya kufikia wageni ya serikali ya Diaoyutai mjini Benjing, wakati alipokutana na kuzungumza na mabalozi
wa Afrika wanaoziwakilisha nchi zao nchini China ikiwa ni shughuli yake ya
kwanza ya ziara yake rasmi ya kiserikali
nchini humo.
Alipata nafasi
ya kuwaeleza hali ya kisiasa, kiuchumi na kiusalama barani Afrika hasa katika
nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Jamhuri ya Afrika ya Kati
(CAR), Libya, Sudan Kusini na Somalia na tishio la ugaidi wa makundi mbali
mbali katika nchi za Afrika.
“Lakini
habari kubwa katika Afrika kwa sasa ni ugonjwa wa Ebola. Bara la Afrika
linabaguliwa sasa kwa sababu ya ugonjwa huo. Watu wanafuta mipango yao
kutembelea bara letu, watalii wanapungua. Kwetu sisi ugonjwa huu ni tishio
kubwa kwa maisha ya watu wetu lakini ni tishio kubwa kiuchumi,” alisema.
“Sasa kwa
sababu ugonjwa wa Ebola unaongeza kubaguliwa bara la Afrika, ni wajibu wenu
nyie wawakilishi wetu, mabalozi wetu kutusemea. Elezeni habari njema na nzuri
za Afrika. Waambie hawa wakubwa kuwa bara la Afrika ni bara salama kutembelea
pamoja na kushambuliwa na ugonjwa wa Ebola. Aidha, kwa sababu kuna majaribio ya
dawa nyingi za ugonjwa huo yanafanyika katika nchi mbali mbali ikiwemo China,
waombe wakubwa hawa watusaidie kupatikana kwa dawa hizo,” alisema.
Kuhusu
mchango wa Tanzania katika kukabiliana na ugonjwa wa Ebola, alisema Tanzania
imetuma madaktari wake watano katika nchi zinazokabiliwa na ugonjwa huo kwa
sasa kuongeza nguvu za kukabiliana na Ebola.
No comments:
Post a Comment