Habari za Punde

Balozi Seif azindua safari Flydubai

Na Othman Khamis, OMPR
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, amesema mfungamano wa kibiashara uliopo baina ya Zanzibar na Mataifa ya Ghuba na Mashariki ya mbali, utaimarika kufuatia kuongezeka mawasiliano ya anga kati ya pande hizo.

Alisema hayo wakati akizindua safari za anga kati ya Dubai na Zanzibar zilizoanzishwa na kampuni ya kimataifa ya usafiri wa ndege ya Flydubai, hafla iliyofanyika uwanja wa ndege wa Zanzibar.

Alisema wafanyabiashara wa Zanzibar pamoja na mwambao wa Afrika Mashariki, wamekuwa wakilitegemea soko la Dubai ambalo ndilo wanalolitumia kupata biadhaa zao.

Alisema uanzishwaji wa safari hizo za moja kwa moja utakuwa kiungo kizuri kwa wafanyabiashara kuendeleza biashara zao kwa kiwango kikubwa zaidi.


Alisema uimarishaji wa uwanja wa ndege wa Zanzibar unaoendelea, umelenga kutoa huduma zinazokubalika kimataifa.

Alisema mkakati zaidi umewekwa kuhakikisha uwanja huo unakuwa na mazingira rafiki ya kuyashawishi mashirika mbali mbali  ya ndege ya kimataifa kufanya safari zake Zanzibar.

“Uwanja wetu tulilenga utoe huduma za moja kwa moja kati ya Zanzibar na mataifa mengine ya Ghuba, Mashariki ya Kati na Ulaya. Hivi sasa tumeanza kupata faraja kwa kuona mashirika ya ndege ya Ethiopia, Qatar na Oman,” alisema.

Aliipongeza Flydubai kwa uamuzi wake wa kuanzisha safari hizo kati ya Dubai na Zanzibar.

Akitoa taarifa ya kampuni hiyo, Makamu wa Rais wa kampuni hiyo, Sudhir Screedhara, alisema kampuni yake tayari inaendelea kutoa huduma kwa karibu miji 12 ya mataifa ya Afrika.

Alisema mradi wao unaotumia ndege mpya za kisasa  aina ya Boeing zipatazo 100 umewekeza kiwango cha fedha karibu dola za Marekani 60,000,000.

Aliipongeza Zanzibar kwa kukubali kwake kuunga mkono uamuzi wa kampuni hiyo wa kutoa huduma za ndege kati ya Dubai na Zanzibar.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Zanzibar, Dk. Juma Malik Akil, alisema serikali itakuwa makini kuhakikisha miradi yote inayohusu sekta hiyo inasimamiwa vyema.


Alisema Flydubai itasaidia kuongeza idadi ya watalii wanaongia Zanzibar kufikia milioni 2 kati ya mwaka 2015 hadi 2025.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.