Habari za Punde

Tibaijuka: Maradhi ya mripuko yakabiliwe kimataifa

Na Anita Jonas, Maelezo
Umoja wa Mataifa umeshauriwa  kuchukua  hatua za haraka kwa maradhi ya mripuko yanayotokea Afrika kama Ebola kwani yanaathiri uchumi wa mataifa yanayohusika.

Ushauri huo ulitolewa na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, wakati wa maadhimisho ya miaka 69 ya Umoja wa Mataifa jana  Jijini Dar es Salaam.

Alisema umoja huo unatakiwa kuchukua tahadhari ya miripuko ya maradhi hatarishi na kuyachukulia kama ni maradhi ya kidunia badala ya kuyaona ni ya Waafrika.

“Kama mataifa yaliyoendelea yasingepuuza mripuko wa  ugonjwa wa Ebola ulipojitokeza  Afrika  hali  isingekuwa  mbaya kiasi hiki, hivyo rai  yangu kwa Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na mataifa yanayohusika kuchukua  tahadhari wakati wote,” alisema.

Aidha alisema kutokana na mabadiliko ya tabianchi, washirika wa maendeleo hawana budi kusaidia mataifa mengine ikiwemo utekelezaji wa mfuko wa kijani wa hali ya hewa.


Akizungumzia hatua ya Rais Kikwete kutoa uraia kwa wakimbizi 162,000 wa Burundi, alisema Tanzania imeonesha ulimwengu kuwa suala la mapambano dhidi ya ukimbizi linaweza kufanyiwa kazi na kuwafanya wakimbizi kuishi maisha kama binadamu wengine.

Naye Mwakilishi wa makazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Alvaro Rodriguez, alisema shirika hilo kwa kushirikiana na serikali na wadau wengine,  limepanga kusaidia na kuimarisha miundombinu ya kiusalama ili kuendeleza amani duniani kwani bila amani maendeleo ni vigumu kupatikana.

Aliipongeza Tanzania katika kutekeleza malengo ya millenia katika sekta ya afya ambapo asilimia 96 ya vituo vyote vya afya nchini vinatoa huduma ya afya ya uzazi kwa mama na mtoto.


Sherehe hizo zimebebwa na kauli mbiu ya ‘Leave no One Behind’ (asiachwe mtu nyuma) ’  ikiwa na lengo la kuleta maendeleo yenye usawa duniani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.