Habari za Punde

Miti shamba yachangia watoto kuzaliwa wafu Kivunge

Na Fatma Kassim
Imebainika wazazi wengi wanaofika hospitali ya Kivunge kujifungua wanapata watoto wafu kutokana na matumizi ya kupindukia ya dawa za miti shamba.

Matumizi ya dawa hizo pia wakati mwengine husababisha kuzaliwa watoto wakiwa na afya dhaifu na kupata magonjwa ya kudumu.

Matatizo mengine ni kuongezeka kasi ya uchungu kwa mjamzito na kusababisha mtoto kufia tumboni, kuzaliwa akiwa amechunika ngozi, wakati mwengine husababisha kuchanika fuko la uzazi na baadae mama hushuka kizazi.

Asha Haidar  mwenye umri wa miaka 32 mkaazi wa  Pitanazako wilaya ya kaskazini ‘A’ mkoa wa kaskazini Unguja, alifikishwa hospitali ya Kivunge Disemba 6 na anasema lipotoka nyumbani  tayari alikuwa amepewa dawa na mama yake kwa lengo la kukazisha uchungu ili akifika hospitali ajifungue mara moja.

“Na dawa za miti shamba nimeanza kutumia tangu ujauzito wangu una miezi minne na nimetumia dawa hizi kwa lengo la kuondoa maumivu nnayoyapata tumboni pamoja na mtoto wangu awe na afya njema na wakati nimeanza uchungu nikiwa nyumbani nimepewa dawa na uchungu ulikuwa na kasi,” alisema.


Aidha alisema aliugua kwa siku nzima bila kujifungua na siku ya pili kwa jitihada za madaktari alijifungua mtoto akiwa tayari ameshafariki tumboni.

Mama wa Asha, Mwatima Ali, alisema ni utamaduni wao kutumia dawa za asili kwa sababu zinaimarisha afya ya mjamzito na wakati wa kujifungua hujifungua mara moja.

Dk. Khamis Hamad Ali, alisema jamii katika mkoa huo imekuwa na hamasa ya matumizi ya dawa za miti shamba kwa wajawazito tangu mimba ikiwa changa, tatizo linalosababisha kujifungua watoto wakiwa wameshafariki.

“Jamii imekuwa na utamaduni wa matumizi ya dawa za miti shamba ambapo matumizi yake kwa kiasi kikubwa yanakiathiri kiumbe kikiwa tumboni na hatimaye kujifungua wakiwa wameshakufa,” alisema.

Katika kubabiliana na tatizo hilo, alibainisha kuwa wamekuwa wakiwaelimisha wajawazito athari za matumizi ya dawa hizo kwa afya za watoto tangu wanapohudhuria kliniki athari za matumizi ya dawa hizo.

Alisema wamekuwa wakiwaelimisha wakunga wa jadi hasa kwenye mikutano ya afya za vijijini ambapo hutumia fursa hiyo kuwaeleza athari za matumizi ya   dawa hizo pamoja na umuhimu wa mjazito kuzalia hospitalini na wasiwazalishwe na wakunga wa jadi.

Alisema tangu Disemba 1 hadi 10 jumla ya watoto watatu wamezaliwa wakiwa wafu kutokana na matumizi ya dawa za miti shamba.

  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.