Habari za Punde

SMZ inahakikisha kwamba huduma za afya zinaimarika


 

  

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

  Zanzibar                                                                                                           9.1.2015

---

SERIKALI  ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikifanya juhudi  kubwa za kuhakikisha huduma za afya zinaimarika licha ya ongezeko la idadi ya watu hapa  Zanzibar ikilinganishwa na idadi iliyopo kabla ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964.
 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kulifungua jengo jipya la upasuaji wa maradhi ya ubongo na  uti wa mgongo lililopo hapo katika hospitali Kuu ya Mnazimmoja mjini Zanzibar ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za maadhimisho ya miaka 51 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
 
Dk. Shein alisema kuwa kabla ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 idadi ya watu wa Zanzibar ilikuwa  ni laki tatu na ishirini ambapo idadi hiyo imeongezeka mara nne ya wananchi wanaoishi Zanzibar ambao wanafika milioni 1.4 hivi sasa jambo ambalo limepelekea utoaji wa huduma uwe tofauti na mara baada ya Mapinduzi.
 
Alisema kuwa azma ya Hospitali ya Manazimmoja kuwa ya rufaa ni ya muda mrefu wazo ambalo limeanza yeye akiwa Naibu Waziri wa Afya na ndipo mchakato ukaanzia hapo na kupita katika vipindi mbali mbali vigumu na hata hivyo mafanikio yameanza kuonekana.
 
Dk. Shein alisema kuwa kuandaa mpango madhubuti katika kuhakikisha hospitali hiyo inakuwa ya rufaa ni jambo ambalo hupelekea mabadiliko makubwa ya mfumo wote wa hospitali ili uende sambamba na utoaji wa huduma za afya.
 
Katika hotuba yake hiyo Dk. Shein pia, alisikitishwa na baadhi ya viongozi ndani ya Mawizara ya Serikali kuwazuia watendaji wao kujiendeleza na masomo kwa lengo la kupata utaalamu zaidi ili kuiedeleza nchi yao.
 

Alisema kuwa kufanya hivyo kunaviza maendeleo ya nchi kwani lengo la serikali ni kupata wataalamu zaidi na iwapo wao wameshinda kazi hizo waiachie Serikali kwani Serikali inathamini na inatambua umuhimu wa kuwapa elimu watendaji wake na iko tayari kuwasaidia kwa hilo.
 
Alisema kuwa jitihada zinahitajika hasa kwa kuhakikisha uongozi bora unapatikana katika kuendesha huduma hizo katika hospitali hiyo kwani matarajio ni kuja kwa wagonjwa kutoka sehemu mbali mbali zilizokuwepo jirani na Zanzibar kwa kutambua kuwa kitengo hicho ni pekee katika ukanda huu wa bara la Afrika.
 
Dk. Shein alisema kuwa sambamba na kuanza kwa tiba ya maradhi hayo pia, Serikali imeamua kwa makusudi kuimarisha huduma za kinga na tiba ikiwa na malengo la kuanzisha kitengo cha kushughulikia maradhi yanayotokana na matatizo ya figo, maradhi ya moyo, saratani pamoja na huduma nyengine.
 
Alisema kuwa kitengo hicho kitakuwa chuo cha kutoa mafunzo kwa vijana wa ndani na nje ya nchi na kuwasisitiza madaktari kutambua kuwa hivi sasa kuna mabadiliko makubwa  katika kuleta maendeleo hasa katika huduma za afya.
 
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ukitaka kuwahudumia wagonjwa vizuri ni lazima huduma za uchunguzi zifanywe vizuri huku akieleza matumaini ya kitengo cha uchunguzi wa maradhi cha hospitali ya Mnazimmoja kupata cheti maalum cha ubora kutoka kwa taasisi husika.
 
Dk. Shein alieleza kufarajika kwake kwa ongezeko la madaktari hapa Zanzibar hivi sasa na kusisitiza kuwa lengo kubwa hivi sasa ni kuongeza madaktari bingwa ili kuongeza kutoa huduma za bora kwa wananchi sambamba na kuipa hadhi Hospitali hiyo ya Mnazimmoja kuwa ya rufaa.
 
Alisisitiza kuwa hospitali hiyo ni lazima ijiendeshe wenyewe  na kuitaka Wizara kuhakikisha kabla ya kikao cha tatu cha Baraza la Wawakilishi Sheria itakayosimamia uendeshaji wa hospitali ya Mnazimmoja iwe tayari  kwani uwezo wa kujiendesha wenyewe upo na kutoa miezi miwili kuhakikisha Sheria hiyo inakuwa tayari.
 
Alisema kuwa kuwepo kwa sheria na kanuni katika hospitali hiyo kutasaidia kuendesha hospitali hiyo na kuondosha mchanganyiko wa mambo kwa.
 
Dk. Shein alisema kuwa lengo la serikali kwa muda mfupi ujao ni kuhakikisha kuwepo kwa ‘E- Health’  ‘E-Education’ na mchakato wake umekuwa ukiendelea na kueleza kuwa mtandao wa mawasiliano utasaidia kwa kiasi kikubwa kwani hizo zote ni kazi za pamoja kati ya wananchi na serikali kwani lengo ni kupata wataalamu zaidi.
 
Sambamba na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Profesa Mahmoud Kuresh akiwa mwakilishi wa Taasisi ya elimu ya maradhi ya ubongo na uti wa mgongo ‘NED’ kwa kuunga mkonno katika kuhakikisha kitengo hicho cha upasuaji kinajengwa hapa Zanzibar na kuweza kutoa huduma
 
Nae Waziri wa Afya Mhe. Rashid Seif alisema kuwa ndani ya miaka 51 ya Mapinduzi ya Zanzibar kuna mambo maendeleo mengi ya kujivunia na kutoa pongezi kwa washirika wa maendeleo kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.
 
Nae Profesa Mahmoud alieleza juhudi zilizochukuliwa katika kuhakikisha ujenzi wa jengo hilo unafanikiwa pamoja na kupatikana kwa vifaa vyake huku akieleza kuwa kuwepo kwa huduma hizo hapa Zanzibar kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa huduma za afya na kuijengea sifa Zanzibar katika ukanda huu wa bara la Afrika.
 
Alisema kuwa kituo hicho ni cha pekee katika ukanda huu na kusema kuwa huduma za mafunzo nazo zitatolewa ili kuhakikisha Zanzibar inapata wataalamu wazalendo wa kufanya pasuaji hizo.
 
Profesa Mahmoud alisema kuwa uanzishwaji wa kituo hicho ilikuwa ni ndoto ya muda mrefu lakini hivi sasa tayari kituo hicho kimeshaanza kufanya kazi na tayari kimeshaaza kufanya upasuaji kwa wagonjwa wa maradhi hayo hapa nchini.
 
Profesa Mahmoud ambaye alikuja hapa nchini akiwa na madaktari bingwa kutoka Spain na Marekani kwa ajili ya kufanya upasuaji kwa watoto wenye maradhi ya vicha maji na baada ya kuwafanyia watoto wengi ambao walikuwa zaidi ya 30 ndipo akaona haja ya kuwepo huduma hizo hapa nchini na ndipo alipoanza mcahkato kwa kuashirikiana na madaktari wenzake hao.
 
Nae Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Mnazimmoja Dk. Jamala Taibu alitoa pongezi kwa Taasisi ya NED pamoja na juhudi za Dk. Shein katika kuhakikisha kada ya afya inapata wataalamu pamoja na madaktari bingwa ili kuimarisha sekta ya afya hapa nchini.
 
Mapema Dk.  Mohamed Saleh Jidawi alisema kuwa zaidi ya Tsh. Milioni 600 zimetumika katika ujenzi wa jengo hilo lenye vyumba viwili vya operesheni, wodi nne, ukumbi wa mikutano pamoja na sehemu nyengine ambapo kwa upande wa vifaa vyote vimetolewa kwa msaada na NED
 
Alisema kuwa madaktari hao kutoka Spain ambao walikuja kutoa huduma hizo za watoto wenye vicha maji mnamo mwaka 2004 na kuwafanyia upasuaji watoto 580 kati ya watoto 2623 waliofanyiwa uchunguzi na kusema kuwa hatua hiyo imesaidia kwa kiasi kikubwa kuokoa fedha za Serikali kwani kama si upasuaji huo ingelibidi wapelekwe nje ya nchi na kutumia fedha nyingi.
 
Aidha alisema kuwa katika ujenzi huo Serikali imechangia asilimi 40 na asilimi 60 zimetolewa na taasisi hiyo ya NED. Aidha, alitumia fursa hiyo kuipongeza Kampuni ya RANS ya hapa Zanzibar iliyoshinda tenda na hatimae kujenga jengo hilo jipya la kisasa.
 
Katika ufunguzi huo viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad,  Mawaziri, Manaibu Waziri, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, wawakilishi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Wafanyakazi wa Wizara ya Afya na viongozi wengine wa Serikali na wananchi.
 
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.