Na Miza Kona. Maelezo.
Wananchi wametakiwa kuwa na mwamko wa kuisoma sheria ili
waweze kuijua na kupata haki zao pamoja na kuepukana na vitendo mbali mbali
vinavyokwenda kinyume na sheria.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Huduma
za Sheria Bi Harusi Miraji Mpatani wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa
habari huko ofisini kwake Migombani Zanzibar.
Amesema wananchi wamekuwa ni wagumu wa kufuata sheria kutokana na uelewa mdogo
waliokuwa nao wa kutojua haki zao za msingi jambo linalopelekea kwenda kinyume
na sheria hizo pamoja na kuwepo kwa kesi nyingi zikiwemo za udhalilishaji na
ukatili dhidi ya wanawake na watoto.
Amesema kituo cha Huduma za Sheria kipo kwa ajili ya
kuwasaidia Wazanzibar kuweza kuelewa na kujua haki zao pamoja na masuala ya
sheria na haki za binadamu kwa kuwapatia elimu sahihi na ufafanuzi wa sheria
hizo.
Amefahamisha kuwa kituo pia kinatoa msaada wa sheria na
huduma kwa wananchi wasiojiweza wakiwemo Walemavu, Masikini ,Wanawake na Watoto
pamoja na kuwaelimisha wananchi na kutatua migogoro.
“Elimu ya vitendo vya udhalilishaji wa watoto inaendelea
kutolewa lakini bado vitendo hivyo vinazidi kuongezeka vijijini hivyo jamii iwe
na mwamko wa kuwafichua na kuwachukulia hatua wale wote wanaofanya vitendo
hivyo”, ameeleza Mkurugenzi huyo.
Akizungumzia kuhusu ucheleweshaji wa kesi mahakani Mkurugenzi
huyo amesema kuwa kuna kesi nyingi mahakamani ambazo bado hazijatolewa hukumu
kutokana na kukwama kwa kesi hizo mahakamni
hapo na nyengine kukosa ushahidi hivyo kituo kinafuatilia tatizo hilo kwa wahusika na
kulitafutia ufumbuzi.
Ameeleza kituo kina miradi miwili inayosimamia haki za
watoto katika Wilaya ya Kaskazini A na Wilaya ya Maghariri Unguja chini ya
ufadhili ya Umoja wa Ulaya (EU) pamoja na Save The Children ambayo inapinga
unyanyasaji wa watoto na kusimamia haki za binadamu.
Bi Harusi amefahamisha kuongezeka kwa watumiaji wa kituo hicho
ni faraja kubwa ambayo inapelekea kupata matumaini mazuri ya maendeleo ya
utoaji wa huduma za kituo kwani katika mwaka 2013 wateja waliofika kituoni hapo
ni 3000 lakini kwa mwaka jana zaidi ya wateja 4000 walifika kupata huduma
katika kituo hicho.
Aidha Bi Harusi amewataka wananchi kufuatilia Katiba iliyopendekezwa
ili waweze kuielewa na kufanya maamuzi sahihi wakati ukifika pamoja na kutumia
kituo hicho cha sheria kwani kinatoa huduma zake bure ili kuwasaidia wananchi
kupata haki zao.
Kituo cha Huduma za Sheria kinatarajia kuazimisha miaka 23
tangu kuanzishwa kwake na kauli mbiu ni “Kutojua Sheria Sio Kukaa kimya”.
No comments:
Post a Comment