Habari za Punde

Wanaushirika 'Tuungane' waiomba serikali iwapatie mashine ya kukamulia asali

Na Zuhura Juma, PEMBA
 
WANAUSHIRIKA wa kikundi cha ufugaji wa nyuki cha ‘Tuungane Cooperative’, kiliopo katika Shehia ya Tumbe Magharibi Wilaya ya Micheweni Pemba, wameiomba Serikali kuwapatia mashine ya kukamulia Asali, ili iweze kufikia kiwango.
 
Walisema kuwa kuendelea  kukamua kwa mikono  ni jambo ambalo linawapa ugumu wa kuendeleza ufugaji huo, kwani haifikii kiwango kinachotakiwa.
 
Wakizungumza na Mwandishi wa habari hizi kijijini kwao walisema  ili kuweza kutoa Asali yenye kiwango, ni vyema Serikali kuwatafutia mashine ya kukamulia na kuacha kutumia mikono yao.
 
Katibu wa kikundi hicho, Mbarouk Juma Mbarouk, alisema kuwa  Asali inapokamuliwa kwa kutumia mikono, inakuwa ni rahisi kuharibika, jambo ambalo si katika malengo yao.
 
“Malengo yetu ni kukamua Asali yenye kiwango, ili idumu kwa muda mrefu, kwani kitu chochote unachotumia mikono ni rahisi kuharibika”, alisema Katibu huyo.
 
Nae, Mwenyekiti wa Kikundi hicho, Massoud Salim Said, alieleza kuwa  lengo la Ufugaji huo ni kupunguza Umasikini katiaka jamii, ingawa wanakwama kutokana na kutokuwepo kwa msukumo katika vikundi vyao.
“Ili kuweza kujikwamua na Umasikini, Serikeli hainabudi kutupa msukumo kwa vikundi vya Ushirika, ambavyo vijana wengi tumejikita huko”, alieleza Mwenyekiti huyo.
 
Kwa upande wa Mshika fedha, Moza Mwazanije Hamad, alisema changamoto nyengine  ambayo hurejesha nyuma ufugaji huo ni ukosefu wa Soko, jambo ambalo hutumia Soko la ndani zaidi kuuza bidhaa hiyo.
 
“Tunatumia Soko la ndani kuuzia bidhaa hii, kazi ngumu kipato kidogo kwani vifaa vinavyotumika kufanyia Asali, vyote tunanunua”, alieleza Mshika fedha.
 
Aliiomba Serikali kuwapatia kipima Asali, ili kuweza kujua kiwango kilichofikia kila baada ya muda kabla ya kuvunwa kwa Asali hiyo.
 
“Huwa hatujui kama ishapea au la, hivyo tukipata kipima Asali itakuwa kila baada ya muda tunaipima na itakuwa tunaivuna kwa kupea kabisa”, alisema.
 
Mjumbe wa kikundi hicho, Siwajibu Massoud Faki, alieleza kuwa kuna maadui ambao huingia katika Masanduku ya Ufugaji huo, jambo ambalo hupelekea kuharibika kwa Asali yao.
 
“Tuna maadui kama Sisimizi, Koyokoyo pamoja na Panya  ambao huingia kwenye Masanduku na kutuharibia, hivyo tunaiomba Serikali itupatie dawa”, alieleza mjumbe huyo.
 
Alisema  ili ufugaji huu uweze kukamilika, wanahitaji kuwa na Masanduku ambayo hugharimu Tshilingi 4,000/= kwa moja, Nta pamoja na masufuria ambayo yote yanahitaji fedha, jambo ambalo ni kikwazo kikubwa kwao.
 
Kikundi cha Tuungane Cooperative, kina wanachama 20  Wanawake nane na Wanaume 12, ambapo kimeanzishwa mwaka 2011, kwa lengo la kujikwamua na Umasikini.
 

           

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.