Habari za Punde

Wajasiriamali Pemba waomba msaada wa vitendea kazi

Na Zuhura Juma, PEMBA
WAJASIRIAMALI wa kikundi cha uzalishaji chumvi cha masumbuko salt, kiliopo Masota Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba, wameiomba Serekali, kuwasaidia vitendea kazi pamoja na soko la uhakika la kuuzia bidhaa zao.
Wajasiriamali waliyaeleza hayo, wakati walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, katika mashamba yao ya utengenezaji wa Chumvi, Masota.
Walisema kuwa ukosefu wa mashine ya kuvutia maji chumvi kutoka baharini hadi kwenye mabwawa yao ni tatizo kubwa linalorudisha nyuma maendeleo ya biashara yao.
Walisema kuwa, pindi serikali ikiwasaidia mashine hiyo, wataweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo, hususan kwa wanachama wao, ambao biashara ya Chumvi ndio moja ya njia ya kuwapatia maendeleo.
“ Maji yanapotoka huku juwa likiwa kali, imekuwa ni tatizo kwetu, tukiwa na mashine ambayo tutakayoweza kuyavuta maji hayo kutoka sehemu moja na kuyaleta katika mabwawa yetu, tutaweza kupunguza ugumu wa tatizo letu”walisema wanaushirika hao.
Mkuu wa kikundi hicho, Hamad Omar Faki alisema wamekuwa wakichukuwa muda mrefu katika kuifanya kazi hiyo ya chumvi, kwa kutumia nguvu za mikono kwa kuyavuta maji ili yajae katika mashimo yao, jambo ambalo huchukuwa muda mrefu.

‘Tunapata shida sana katika kufanya chumvi hii, kwa sababu tunavuta maji kwa kutumia mikono yetu kwa hiyo tunapoteza muda mrefu mpaka kuimaliza ‘ alieleza Mkuu huyo.
Nae fundi wa uzalishaji chumvi kutoka katika ushirika huo, Said Shamata alisema ushirika wao umekuwa ukikosa hydrometer ambayo hutumika kupimia maji hayo, wakati yanapokuwa katika mashimo hayo jambo ambalo ni kikwazo kikubwa katika kutekeleza shughuli hiyo.
‘’Hydrometer ni muhimu sana kwetu kwa sababu tunapima maji, ili tujue kiwango gani tumefikia na kuweza kuyachanganya maji haya kwa kiwango kinachohitajika’’alisema.
Alisema kuwa ili chumvi iweze kuangusha inatakiwa ifikie nukta ishirini na nne (24) ambazo zinapimwa kwa hydrometer na inaweza kuchukuwa muda wa siku sita mpaka kufikia siku kumi na mbili kukamilika.
Kwa upande wake mshika fedha wa kikundi hicho, Said Abdalla Faki alisema tokea kuanzishwa kikundi hicho ni mafanikio madogo ambayo wanayapata kwa kutokuwepo kwa soko la uhakika la kuuzia chumvi hiyo.
‘’Hatuna soko kama siku hizi chumvi polo shilingi elfu sita kwa sababu jua kali na inakuwa elfu nane mpaka tisa kwa kipindi cha mvua’’.alieleza mshika fedha.
Hata hivyo waliwataka wananchi kujishuhulisha katika kazi mbali mbali za ujasiria mali, kwa kuachana na tabia ya kukaa mitaani, kikundi cha Masumbuko Salt kilianzishwa mwaka 2009 kikiwa na wanachama tisa, wanaume sita na wanawake watatu.

                                                                          

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.