Habari za Punde

Watengeneza matofali hatarini kupoteza maisha.

Na Zuhura Juma,  PEMBA
WACHIMBAJI wa Matofali katika Kware ya Uwandani, Wilaya ya Chakechake, wamesema  kuwa wako hatarini kupoteza maisha yao kutokana na Vumbi linalowaingia Vifuani na Machoni mwao,   na kuiomba Serikali kupitia Wizara husika  kuwatafutia ajira mbadala, ili kuendeleza  Maisha yao.
Kilio hicho kilitolewa na wachimbaji hao, wakati walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari, machimboni kwao Uwandani-Pemba.
Walisema kuwa  kutokana na Vumbi hilo linalowaingia vifuani mwao pamoja na machoni, imekuwa ni kikwazo kikubwa kwao kilichokuwa hakina mtetezi.
Walifahamisha kuwa  kutokana na kukosa ajira mbadala ambayo itawaepusha na madhara hayo, imewabidi kuendelea kufanya kazi hiyo, ili kujikimu kimaisha na Watoto wao.
Mmoja wa Wachimbaji hao, Juma Khamis Othman, mkaazi wa Vitongoji kibokoni, alisema kuwa kazi hiyo wameianza kwa muda mrefu, ambayo huifanya kila siku, hivyo vumbi hilo huwaingia sana na kuwaathiri kidogo kidogo.

“Tunakaa hapa kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa 12 jioni, na wengine tupo kwa muda mrefu, na vifua vinatuuma lakini hatuna la kufanya, kwa sababu tunataka kula na watoto”, alifahamisha.
Alisema kuwa, kutokana na ugumu wa maisha wanalazimika kuendelea kuchimba Matofali hayo, ingawa wanaathirika Kiafya, hivyo wanaiomba  Serikali kuwapatia ajira mbadala ili kuepukana na athari hizo.
Nae, Mbarouk Suleiman Omar, mkaazi wa Vitongoji Kisiwani Pemba, alisema kuwa Macho yao pia huwauma pamoja na kutoka Machozi kila wakati, kutokana na kukosa Miwani ambayo huvaliwa wakati wa uchimbaji.
“ Yaani ni dhiki tupu ya kuchimba Matofali, lakini hatuna la kufanya, kwani ikiwa hatukufanya hivi basi hatuli wala watoto hawasomi”, alieleza Mbaruok.
Kwa upande wake, Suleiman Omar Khalfan, mkaazi wa Vitongoji Kibokoni ,alisema  ili Taifa liweze kuwa na Vijana wenye nguvu na kuweza kulipeleka mbele, Serikali hainabudi kuwatafutia ajira, kwani kazi hiyo hupoteza nguvu nyingi kwa Vijana hao.   
“Kazi tunayoifanya ni ya nguvu sana, itafikia kipindi tutakuwa hatuwezi na sisi tuna watoto  hali hii itapelekea Watoto wasisome kwani itakuwa hatuna pesa za kuwahudumia na wao watafuata kuchimba kama sisi”, alisema Mchimbaji huyo.
Wachimbaji hao ambao huchimba matofali zaidi ya 5000 kwa mwezi, hiyo ni kutokana na ugumu wa Ardhi katika sehemu ya uchimbaji, ambapo Tofali moja huuzwa kwa Tshilingi 400/=.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.