Habari za Punde

Nyaraka Muhimu za Historia ya Zanzibar, Zaibiwa

Na Mwinyi Sadallah – Mwananchi

NYARAKA ZA siri za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zilizokuwa zimehifadhiwa katika Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu za Taifa (Zanzibar National Archives), zimeibiwa.

Kwa mujibu wa habari mtu ambaye anatuhumiwa kuratibu mpango wa wizi wa nyaraka hizo ni Humoud Abdalla Al Rashid, Ofisa Mwandamizi wa Ubalozi wa Oman, uliopo Zanzibar.

Akiwasilisha ripoti ya Kamati Teule ya kuchunguza wizi wa nyaraka hizo katika Baraza la Wawakilishi, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mahamoud Mohammed Mussa alisema tukio la wizi huo lilianza kujulikana kuanzia Julai mwaka 2013 na Baraza kulazimika kuunda Kamati ya Uchunguzi.

Mahamoud alisema nyaraka hizo zilikuwa zimehifadhiwa kwenye masanduku katika chumba maalumu, lakini wafanyakazi walikula njama za kuziiba kwa kushawishiwa na maofisa wa ubalozi huo.

Aliwambia Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wezi hao walitumia mbinu mbalimbali za ushawishi wa fedha na zawadi za chakula ikiwemo tende. Mpango wa wizi wa nyaraka hizo ulifanyika kwa siri kubwa.

Mahamoud alisema miongoni mwa nyaraka zilizoibiwa ni pamoja na nyaraka za kumbukumbu za Utawala wa Sultani Sayyid Barghash Bin Said.

Nyaraka nyingine zilizoibiwa ni waraka uliyotumika kupiga marufuku biashara ya utumwa kufanyika Zanzibar mwaka 1873, na kumbukumbu za ujio wa wamisionari Zanzibar, ambao walifanya kazi ya kueneza ukristo Afrika Mashariki.

Hata hivyo, alisema kwamba baada ya kamati kugundua mpango wa wizi wa nyaraka hizo uliyoratibiwa na Ofisa wa Ubalozi wa Oman, Humoud Abdalla AL Rashid hatua za kumkamta na kumfugulia mashitaka zimekwama kutokana na kuwa na kinga ya kidiplomasia, ya kutoshtakiwa.

Alisema kwamba ofisa huyo, kabla ya kufanikisha wizi wa nyaraka hizo alikuwa akenda kila mara akiwa na zawadi za chakula na kujenga uhusiano mkubwa na wafanyakazi wa taasisi hiyo kwa madhumuni ya kuendeleza hifadhi za kumbukumbu hizo.

Aidha, alisema pamoja ofisa huyo wa ubalozi kufunguliwa kesi katika Kituo cha Polisi cha Mazizini, Zanzibar, Jeshi la Polisi limekwama kumkamata kutokana na mkataba wa Vienna wa mwaka 1961 na sheria No. 5 ya kinga na fursa 1986 kuweka kinga ya wanadiplomasia kukamatwa na kufunguliwa mashtaka.

Mahamoud alisema kamati yake imegunduwa kuwa Waziri wa Kazi na Utawala wa SMZ, Haroun Ali Suleiman amelidaganya Baraza la Wawakilishi kutokana na kauli yake aliyotoa kuwa Humoud hakuwa ofisa mwanadamizi wa ubalozi, bali alifika Zanzibar kama mfanyakazi kufanikisha shughuli za matengenezo ya jengo moja la historia.

Alisema kitendo cha waziri kinakwenda kinyume na masharti ya kanuni ya 59 (3) ya kanuni za kudumu za Baraza la Wawakilishi ambazo zinakataza mjumbe yeyote kutoa maelezo ya uongo au ya kubahatisha..

1 comment:

  1. nyie hamna serikali mna mashaka tu hapo, ngoja tusikie na huyo rais kaibiwa

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.