Habari za Punde

Elimu SACCOS Zanzibar Yafanya Mkutano wao Mkuu wa 15.

Na Ramadhani Ali na Maelezo
                          
Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mohdraza Hassan Daramsi ameahidi  kushirikiana na Ushirika wa Akiba na Mikopo wa Elimu Zanzibar (Elimu SACCOS) kufanya Biashara pamoja ili kuinua  hali za maisha ya wananchama wake.

Raza ametoa ahadi hiyo alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa 15 Elimu Saccos katika Ukumbi wa wa Judo Amani nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Katika kuimarisha mashirikiano hayo Mwakilishi huyo ambae ni mfanyabiashara maarufu Zanzibar amewaeleza wanachama hao kuwa yuko tayari kutoa mikopo na vifaa vya ujenzi wa nyumba bila riba.

Amewataka wanachama hao, ambao wengi ni walimu kutoka Skuli za Mikoa yote mitano ya Zanzibar, kuitumia fursa hiyo ili waweze kujenga nyumba bora za kuishi.

‘’Jiandaeni mimi niko tayari kutoa kila msaada unaohitajika kwa Saccos hii ili kuhakikisha hali za maisha ya walimu zinaimarika,‘’ alisisitiza Mwakilishi huyo.

Raza amewashauri viongozi wa Saccos hiyo kuwa  wakweli na wa wazi katika kusimamia Elimu Saccos bila kuingiza masuala ya siasa na Dini huku wakielewa kuwa uongozi ni dhamana hivyo unahitaji kutumia hekima.

Aliwakumbusha wanachama hao kuwa  unapoingiza  siasa, dini ama ukabila katika vikundi vya kiuchumi huwezi kupiga hatua ya kimaendeleo na hatimae ni kufilisika.

Amewapongeza viongozi Elimu Saccos kwa kusimamia mabadiliko makubwa ya uendeshaji wake kwa kuondosha mfumo wa riba na kuelekeza nguvu  kujiendesha kwa kufanya biashara.

Katibu Mkuu wa Elimu Saccos Bi. Salma Simai Rajab alisema  tayari Ushirika huo umetoa mikopo ya kawaida, dharura na vifaa kwa wanachama 1,640 yenye thamani ya  zaidi ya shilingi bilioni moja na ina akiba isiyopungua milioni 67.

Bi. Salma alisema Ushirika wa Elimu Saccos ulianzishwa mwaka 1997 ukiwa na wanachama 61 na hivi sasau  inawanachama 2534. Idadi ya wanachama imekuwa ikiongeza kila mwaka kutokana na juhudi za viongozi kuwahamasisha walimu kujiunga na mahitaji ya walimu kwa jumla.                                         

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.