Habari za Punde

Balozi mteule wa TZ nchini Kenya akutana na Dk Shein Ikulu

01
02
  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na  Balozi Mteule wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Kenya Mhe,John Michael Haule
alipofika Kujitambulisha Ikulu Mjini Zanzibar leo Juni 29, 2015.
03
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akibadilishana mawazo na Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Kenya Mhe,John Michael Haule baada ya
mazungumzo yao alipofika Kujitambulisha Ikulu Mjini Zanzibar.


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                       29.06.2015
---
RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Kenya na Tanzania ni nchi zenye uhusiano wa muda mrefu hivyo kuna kila sababu za kuendelea kuimarisha na kuitekeleza Sera ya Demokrasia ya Uchumi  kwa manufaa ya pande mbili hizo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Kenya Mhe. John Michael Haule, ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya kuaga na kupata baraka za Rais.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Haule  kuwa kwa vile Kenya na Tanzania zimo katika mchakato wa kutekeleza Sera ya Demokrasia ya Uchumi ana matumani makubwa kuwa mafanikio makubwa ya kiuchumi yataendela kupatikana baina nchi mbili hizo.

Dk. Shein alisema kuwa mashirikiano katika nyanja mbali mbali za maendeleo hasa ikizingatiwa nchi mbili hizo zimo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki yamekuwa yakiimarika siku hadi siku.


Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa nchi mbili hizo zimekuwa na historia ya kusaidiana pale nchi moja wapo inapopata matatizo, hivyo ana imani kubwa na Balozi Haule kuwa ataendeleza uhusiano na ushirikiano huo kati ya nchi mbili hizo kutokana na utendaji wake wa kazi.

Kwa upande wa Zanzibar, Dk. Shein alimueleza Balozi Haule kuwa kumekuwa na uhusiano wa kidugu na kihistoria kati ya nchi hiyo na Zanzibar hasa ikizingatiwa uhusiano kati ya Zanzibar na Mombasa katika nyakati za ukoloni hatua ambayo imepelekea kuimarika kwa uhusiano huo hadi hii leo na kuweza kuwepo kwa Ubalozi Mdogo huko mjini Mombasa.

Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa Kenya na Zanzibar kumekuwa na uhusiano na ushirikiano mzuri wa kibiashara hasa katika zao la karafuu, ambapo wafanyabiashara wa nchi hiyo wamekuwa wakinunua karafuu kupitia Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC).

Alisema kuwa hatua hiyo imeweza kuondosha tatizo lililokuwepo hapo siku za nyuma ambapo biashara hiyo ilikuwa ikifanywa kimagendo  na baadhi ya watu kati ya Kenya na Zanzibar na kuikosesha Zanzibar kuimarisha pato lake la uchumi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi Haule haja ya kulitangaza soko la Utalii nchini Kenya kwani nchi hiyo nayo imeweza kupata mafanikio katika sekta hiyo.

Nae Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Kenya Mhe. John Michael Haule alimuahidi Dk. Shein kuwa katika utekelezaji wa Kazi zake nchini humo atazidi kujenga uhusiano na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Kenya.

Balozi Haule alieleza kuwa Ubalozi wa Tanzania nchini humo utaimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano ikiwa ni pamoja na kuweka mikakati katika kuhakikisha Sera ya Demokrasia ya Uchumi kati ya pande mbili hizo inaimarishwa.

Katika mazungumzo yake Balozi huyo, alisisitiza haja ya kuimarisha ulinzi katika maeneo ya Utalii hapa nchini sambamba na kuimarishwa kwa usafiri kati ya Kenya na Tanzania ikiwemo Zanzibar ili kutoa usafiri wa uhakika kwa wageni wanaotembelea vivutio vya kitalii vilivyopo katika maeneo hayo.

Aidha, Balozi huyo aliahidi kuendeleza uhusiano na ushirikiano katika nyanja ya uwekezaji na biashara hasa ikizingatiwa kuwa katika nchi za Afrika ya Mashariki nchi ya Kenya inaongoza kwa wawekezaji na wafanyabiashara wake kuekeza hapa Tanzania.

Pamoja na hayo,  mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha mambo mbali mbali ya kimaendeleo yakiwemo ya kiuchumi kati ya Kenya na Tanzania.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.