Habari za Punde

Jamii ihamasishwe kuthamini na kuenzi utamaduni wa Zanzibar

Mwashungi  Tahir                  Maelezo

Katibu Mtendaji Baraza la  Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) Mwanahija Haji Juma  amesema kwamba jamii inahitaji kuhamasishwa  kuthamini na  kuenzi Utamaduni wa Zanzibar ili uweze kuimarika na kukua  zaidi .

Hayo ameyasema leo huko katika Ukumbi wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Kampasi ya Vuga alipokuwa akifungua Kongamano la Tamasha la 20 la Utamaduni la Mzanzibari lililohudhuriwa na wanafunzi wa Vyuo  Vikuu mbali mbali nchini.

Amesema Kongamano hilo  ambalo ni mfululizo wa  Tamasha la Zanzibar lililozinduliwa rasmi na Makamu wa Pili wa Rais tarehe 21 katika Ukumbi wa Salama Bwawani  linasisitiza kuendelezwa, kuenziwa na kuthaminiwa  na watu wote.

“Tamasha hili lilianzishwa nakuszinduliwa rasmi na Rais wa awamu ya tano Mh. Salmin Amour Juma  mwaka 1994  katika Uwanja wa Amani,”alisema Katibu Mtendaji.

Aidha alisema lengo kuu la Tamasha hilo linalofanyika kila mwaka ni kulinda, kuenzi na  kuwahamasisha wananchi  kuelewa Utamaduni wao kwa undani zaidi kwani ni kioo cha wananchi.


Amesema Utamaduni ni mfumo wa maisha wa jamii husika na sio  ngoma pekee kwani yapo  mambo mengi katika  utamaduni  yakiwemo mavazi, vyakula , malezi , kusoma vitabu vya historia, kutunga mashairi na  mengineo.

Nae Mkuu wa Idara ya Kiswahili wa SUZA Dkt. Maulid Omar amesema iko haja ya wananchi kufahamu changamoto zinazokabili Utamaduni wa Zanzibar kwani  baadhi ya mambo  yanaingizwa  kuharibu utamaduni huo.

Mada mbili ziliwasilishwa na kujadiliwa katika Kongamano hilo ambazo ni athari za Utalii katika kuendeleza Utamaduni  iliyotolewa na Bi. Mwanahamisi Hassan  wa Idara ya sayansi jamii  SUZA na  mada ya pili  iliyotolewa na Mhadhiri Msaidizi Omar Salum Mohd ilizungumzia mshikamano wa Utamaduni na Uislamu.

Kongamano hilo lilifungwa  na Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili  Bi. Mwanahija  Haji Juma na kauli mbiu ya  Tamasha la  mwaka huu  ni Utamaduni kwa Furaha, Amani na Utulivu

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.